Auawa kinyama washukiwa wakirekodi
JUMAPILI Aprili 7 2024 katika kijiji cha Sino K’Agolla, Rachuonyo Kusini, Kaunti ya Homa Bay, ilianza kama siku nyingine yoyote.
Maisha yaliendelea kwa utaratibu na hakukuwa na dalili kuwa ifikapo jioni, mtu mmoja angekuwa ameuawa na jamii nzima kubaki katika mshtuko mkubwa kutokana na ukatili wa tukio hilo.
Collins Okiro, 30, alikuwa nyumbani na mkewe, Bi Quinter Awino, wakati wanaume wawili walipofika katika boma lao.
Hawakuwa wageni kwani mmoja wao alikuwa binamu yake, Suleiman Onyango Kabasa, huku mwingine akifahamika kwa familia.
Hawakutiliwa shaka.
Walimwita Okiro, wakasalimiana kwa ufupi na kukataa kupewa uji kabla ya kuondoka naye.
Aliondoka nao kwa utulivu kuelekea gari lililokuwa likisubiri.
Huo ndio ulikuwa mwisho mkewe kumuona akiwa hai.
“Nilikuwa jikoni. Mwanzoni nilidhani ni mpangaji wa shamba letu, lakini baadaye nikagundua ni Onyango, binamu wa mume wangu na afisa wa Jeshi la Ulinzi Kenya. Walikataa hata kuketi na wakaondoka naye. Hiyo ndiyo ilikuwa mara ya mwisho kumuona,” alisema.
Baadaye, mwili wa Okiro ulipatikana katika boma la jirani umbali wa kilomita chache kutoka nyumbani kwake.
Baada ya uchunguzi, Onyango alikamatwa kufuatia video iliyosambaa mtandaoni ikimuonyesha yeye na nduguye Robinson Kabasa wakimpiga Okiro kabla ya kutupa mwili wake.
Robinson na mtu aliyerekodi video bado wanatafutwa.
Onyango alifikishwa mahakamani na kukana mashtaka ya mauaji.
Akitoa ushahidi, Bi Awino alisema baada ya mumewe kuondoka, alitarajia angerudi mchana, lakini hakurejea.
Alipoanza kumtafuta, mwanamke mmoja alimweleza kuwa alimsikia Okiro akipiga mayowe akiomba msaada na kuuliza kwa nini alikuwa akiuawa.
Mashahidi wengine, akiwemo Linet Akoth, walithibitisha kusikia kilio hicho.
Akoth alisema Okiro alikuwa amefungwa mikono na miguu, kufunikwa macho na kuvuliwa nguo kabla ya kushambuliwa kikatili.
Video iliyowasilishwa mahakamani inaonyesha Okiro akiwa amelala chini bila msaada huku akipigwa. Robinson anaonekana akimkanyaga usoni huku Onyango akimpiga kwa nguvu.
Licha ya kuomba msaada, hawakumhurumia na alipigwa hadi sauti yake ilipodhoofika na hatimaye kukoma.
Video nyingine inaonyesha akiwa hoi akiingizwa ndani ya gari kabla ya kupelekwa eneo jingine.
Mashahidi walisema waliambiwa Okiro ni mwizi, lakini kilichotokea hakikiwa cha kawaida.
Baada ya kugundua amefariki, waliutupa mwili wake katika boma la jirani na kutoroka.
Ripoti ya uchunguzi wa maiti ilionyesha alikuwa na majeraha makubwa kichwani, mguuni na dalili za kunyongwa.
“Alikuwa uchi na mwili wake ulikuwa baridi, ukiwa umejaa siafu,” alisema Awino.
Kesi hiyo sasa inaendelea katika Mahakama Kuu ya Homa Bay mbele ya Jaji Olga Sewe. Upande wa mashtaka unaongozwa na Wakili wa Serikali Gloria Ongubo, huku utetezi ukiwakilishwa na Wakili Linda Agwanda.
Familia imekataa makubaliano ya kupunguza mashtaka, ikitaka haki kamili ipatikane.
Kesi hiyo imeibua maswali mengi, hasa kwa nini washukiwa wengine bado hawajakamatwa.
Familia inasema haitaridhika na chochote isipokuwa haki kamili kwa mpendwa wao.