Habari

TUKO KADI! Wanasiasa sasa wang’ara na kampeni iliyoanzishwa kuwarai vijana kujisajili kama wapiga kura

Na BENSON MATHEKA March 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

WIMBI la kampeni ya Niko Kadi lililoanzishwa na vijana kote nchini sasa limegeuka uwanja wa mvutano mkali wa kisiasa, huku waanzilishi wake wakilalamikia kile wanachokitaja kama wanasiasa “kudandia” juhudi zao kwa manufaa ya kisiasa.

Kampeni hiyo, iliyopata umaarufu mkubwa hasa mitandaoni miongoni mwa Gen Z, ilianza kama njia ya kuwahamasisha vijana kujisajili kama wapigakura na kushiriki kikamilifu katika masuala ya kitaifa.

Hata hivyo, kadri umaarufu wake unavyoongezeka, ndivyo mvutano kati ya vijana na wanasiasa unavyozidi kushika kasi.

Kiongozi wa vijana wa Niko Kadi Ademba Allans amemkosoa vikali Rais William Ruto kwa kile alichokitaja kama “wizi wa ubunifu” baada ya rais kutumia kauli hiyo hadharani.

Akizungumza katika mahojiano na runinga kadhaa nchini wiki hii, Allans alisema wazi kuwa kampeni hiyo haikulenga kuunga mkono serikali bali kuikosoa.

“Ilikuwa wizi wa fikra wakati rais alisema ‘Niko Kadi’. Bro( kaka), uko kadi ya nini? Sisi tuko hapa kukuondoa,” alisema Allans.

Kauli hiyo inaonyesha wazi msimamo wa baadhi ya vijana wanaohusisha Niko Kadi na kampeni pana ya kutaka mabadiliko ya uongozi nchini.

Allans alifichua kuwa wanasiasa kadhaa wamekuwa wakijaribu kuingilia kampeni hiyo kwa njia ya ufadhili, jambo alilolikataa vikali.

“Tumepigiwa simu na wanasiasa wengi wakitaka kutusaidia. Wengine wanataka hata kutuletea malori ya kampeni. Hatutaki msaada wao. Lori lolote litakalokuja kwenye mkutano wetu tutalifukuza,” alisisitiza.

Kulingana na mwanaharakati Sophie Njehia vijana wanapaswa kulinda uhuru wa kampeni hiyo na kuepuka kutumiwa kisiasa.

Kauli zake zilionyesha kutoridhishwa na baadhi ya viongozi wanaojaribu kutumia kampeni hiyo kujinandi ilhali hawana imani na mwelekeo wake.

Hata hivyo, licha ya upinzani huo, baadhi ya wanasiasa wameendelea kujiingiza waziwazi katika kampeni ya Niko Kadi.

Aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua alizua mjadala baada ya kujiunga na vijana katika mji wa Nyeri, akihamasisha usajili wa wapigakura.

Akiwahutubia wanahabari, Gachagua alisema vijana wako katika njia sahihi na wanapaswa kuendelea kujisajili kwa wingi ili kufanikisha mabadiliko waliyoyataka wakati wa maandamano ya mwaka 2024.

“Kura hii ya vijana itawawezesha kufanikisha yale waliyotaka wakati wa maandamano ya Gen Z, walitaka uwazi, uwajibikaji, elimu bora na huduma nzuri za afya,” alisema.

Wazazi wahamasishe wanao

Aliongeza kuwa wazazi pia wana jukumu la kuwahamasisha watoto wao kujisajili kama wapigakura, akisisitiza umuhimu wa ushiriki wa vijana katika uchaguzi ujao.

Hata hivyo, hatua ya Gachagua imeibua ukosoaji kutoka kwa baadhi ya viongozi, akiwemo aliyekuwa waziri Moses Kuria. Kupitia mitandao ya kijamii, Kuria alimshutumu Gachagua kwa kugeuza kampeni hiyo kuwa ya kikanda badala ya kuwa ya kitaifa.

“Kampeni hii ilikuwa ya vijana wote, lakini sasa imeelekezwa kuwa ya eneo moja. Hii inaua ujumbe wake wa kitaifa,” alisema Kuria.

Alionya kuwa kuipatia sura ya kikanda kunaweza kuwatenga vijana kutoka maeneo mengine na kudhoofisha lengo kuu la kampeni hiyo, ambalo ni kuunganisha vijana kote nchini.

Mvutano huu pia umechangiwa na kauli za kisiasa kutoka pande mbalimbali, huku baadhi ya viongozi wakitumia Niko Kadi kama jukwaa la kushambulia au kujipanga kisiasa kabla ya uchaguzi mkuu ujao.

Kwa upande wa waanzilishi, msimamo unabaki kuwa kampeni hiyo ni ya wananchi wa kawaida na si ya wanasiasa. Allans alisisitiza kuwa wanaungwa mkono na Wakenya wa kawaida pamoja na kumbukumbu ya vijana waliopoteza maisha wakati wa maandamano ya 2024.

“Sisi tunadhaminiwa na Wakenya, tunadhaminiwa na wale waliokufa mwaka 2024 na imani kwamba lazima kuwe na mabadiliko,” alisema.

Kadri kampeni hiyo inavyozidi kusambaa kote nchini, imeendelea kuvutia maelfu ya vijana wanaojitokeza kujisajili kama wapiga kura. Lengo la waanzilishi ni kufikia zaidi ya vijana 1,000 katika kila eneobunge kila siku, jambo linaloonyesha ukubwa wa hamasa iliyopo miongoni mwa kizazi kipya.

Hata hivyo, changamoto kubwa inayobaki ni jinsi ya kulinda uhalisia na malengo ya kampeni hiyo dhidi ya ushawishi wa kisiasa. Wengi wanaona kuwa iwapo wanasiasa wataendelea kujiingiza bila mipaka, kuna hatari ya kupotosha ujumbe wa awali wa harakati hiyo.

“Kwa sasa, Niko Kadi imebaki kuwa alama ya nguvu ya vijana katika siasa za Kenya—lakini pia imegeuka kuwa kivutio kipya cha wanasiasa wanaotaka kujinadi na nguvu hiyo. Swali linalosalia ni ikiwa vijana watafanikiwa kulinda sauti yao, au kama itamezwa na siasa za kawaida zinazoikumba nchi kila msimu wa uchaguzi,” asema mchanganuzi wa siasa Tom Maosa.

Anasema vijana wamerushia changamoto Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kwamba wako tayari kujiandikisha kote nchini na kwamba inafaa kuwa tayari kwa hilo bila utepetevu au ubaguzi wa aina yoyote.