Wasomi someni hii likizo
Wasomi njie mefanya, yalo masomo shuleni,
Wasomi mi nawaonya, sasa mlipo nyumbani,
Wasomi sije changanya, yalo mbi ya majutoni,
Wasomi wote wa Kenya, hino likizo someni.
Wasomi sitawasinya, swala nyeti pulikeni,
Wasomi sitadanganya, inna tu niwambieni,
Wasomi mweze kumanya, lilo bora aushini,
Wasomi wote wa Kenya, hino likizo someni.
Wasomi livu mepenya, jinoe zenu bongoni,
Wasomi ujinga ponya, kwa kusoma vitabuni,
Wasomi ndo nawakanya, somo sitie kapuni,
Wasomi wote wa Kenya, hino likizo someni.
Wasomi kusoma fanya, utepetevu mwacheni,
Wasomi sende kuhanya, msitomwe kaburini,
Wasomi zidi tekenya, mabuku nambari wani,
Wasomi wote wa Kenya, hino likizo someni.
Wasomi lojitawanya, somea penu kyamboni,
Wasomi mweze gawanya, wakaa kudurusuni,
Wasomi ndo kubiginya, ya masomo ya usoni,
Wasomi wote wa Kenya, hino likizo someni.
Wasomi sije pokonya, ya wavyelenu mapeni,
Wasomi stiwe rumenya, kasahau masomoni,
Wasomi kutosengenya, huluka njema fwateni,
Wasomi wote wa Kenya, hino likizo someni.
Wasomi siwe ja panya, kwonja mihadaratini,
Wasomi mwendee nyanya, kwa wosia fuadini,
Wasomi shwari kusanya, mwitimize ya ruyani,
Wasomi wote wa Kenya, hino likizo someni.
Wasomi mlo Ugenya, Nakuru na Mombasani,
Wasomi kosa kang’anya, siwe chozi karibuni,
Wasomi mweze kuponya, yalo mawi epukeni,
Wasomi wote wa Kenya, hino likizo someni.
Wasomi wino kifinya, ndo tapasi mitihani,
Wasomi ninafunganya, bakini kwa tumaini,
Wasomi naomba mwanya, nifikile tamatini,
Wasomi wote wa Kenya, hino likizo someni.
JAMES MUTWIRI WANJAGI
‘MALENGA MSIFIKA NA MSIKIVU’
CHUKA, THARAKA-NITHI
Buriani mbunge Kiaraho!
Siamini haya mimi, mbunge wangu Kiaraho,
Yamekwama hata ndimi, umechukuliwa roho?,
Nadondokwa basi nami, kifo wewe umechoho?,
Ulazwe pema peponi, waliokowema wao.
Kazi ulitufanyia, barabara zikafika
Masomo litupatia, hadi ziliaminika,
Wananchi l’wafikiria, usawa ulisikika,
Ulazwe pema peponi, waliokowema wao.
Wakazi wote poleni, nawafariji kwa beti,
Nyuso zenu za huzuni, kwenu mgumu wakati,
Nguvu awape subhani, ameondoka sauti,
Ulazwe pema peponi, waliokowema wao.
Ndugu pia familia, rambirambi nazituma,
Alipendwa na mamia, jinsi alivyojituma,
Mioyoni atasalia, kwa jamiii ya mulima,
Ulazwe pema peponi, waliokowema wao.
Mchangamfu alikuwa,maisha yake furaha,
Kiongozi wa usawa,wakaazi wake raha,
Ewe dadii wa pawa,Mbunge wa nasaha,
Ulazwe pema peponi, waliokowema wao.
WACHIRA ROMEO MUGO
MALENGA LANGU JICHO’
CHUO KIKUU CHA MURANG’A
Talaka ya usaliti
Ninatunga kwa uchungu, moyo wangu unalia
Watu hawa walimwengu, ‘wawezi kuvumilia
Jihadharini wenzangu, msije kuambulia
Talaka ya usaliti, huwa kama donda ndugu
Unapopata mchumba, wanafiki wanafika
Namba yake wanaomba, huku wakichekacheka
Ukiondoka kwa nyumba, kuharibu wanafika
Talaka ya usaliti, huwa kama donda ndugu
Juzi kwenye ‘levisheni, nimekiona kisanga
Mke kachomwa usoni, akidaiwa kupanga
Kwa uchungu wa moyoni, ikaja isiyo kinga
Talaka ya usaliti, huwa kama donda ndugu
Wote hung’aa usoni, huwezi kuwatambua
Ukiwaweka moyoni, nyumaye wakutimua
Unabaki na huzuni, ‘wazo mengi kutatua
Talaka ya usaliti, huwa kama donda ndugu
Huu ni wosia wangu, haswa kwa vijana wote
Katika ndoa wenzangu, weka ‘aminifu wote
Uongo huwa mchungu, bila faida yoyote
Talaka ya usaliti, huwa kama donda ndugu
WANJIRU SAMUEL
‘MALENGA MHENGA’
CHUO KIKUU CHA KITEKNOLOJIA CHA MURANG’A
Haki zetu tadai
Ninadai haki zangu, kama Mkenya halali,
Siombi kwa mikono, wala siombi kwa hali,
Katiba imethibitisha, si jambo la kubadili,
Heshima na usawa, viwe nguzo za kweli,
Haki zetu zilindwe, tusinyimwe kiholela.
Haki ya kuishi salama, bila hofu na dhuluma,
Polisi walinde watu, sio kuwaumiza nyuma,
Sheria iwe mlinzi, si chombo cha mateso suma,
Kila mmoja aheshimiwe, maskini hata tajiri huma,
Haki zetu zilindwe, tusinyimwe kiholela.
Haki ya elimu bora, kwa mtoto wa kila kaya,
Si matajiri tu wapate, na maskini wakose haya,
Shule ziwe na walimu, vitabu pia vya kutosha,
Elimu iwe silaha, ya kujenga taifa bora,
Haki zetu zilindwe, tusinyimwe kiholela.
Haki ya afya njema, hospitali ziwe wazi,
Dawa zipatikane, si ahadi zisizo na kazi,
Madaktari wahudumu, kwa moyo bila ubaguzi,
Afya ni msingi wa taifa, si biashara ya miradi,
Haki zetu zilindwe, tusinyimwe kiholela.
Haki ya kazi na ajira, vijana wasikae bure,
Jasho lao liheshimiwe, wapate riziki halali bure,
Rushwa ikomeshwe, isiwe njia ya kupata nafasi,
Kila bidii ithaminiwe, bila ubaguzi wa nafasi,
Haki zetu zilindwe, tusinyimwe kiholela.
Tuungane wakenya wote,kudai yaliyo kweli
Kwa amani na mshikamano,bila chuki na gadhabu,
Haki si ombi la huruma,ni wajibu wa Kila hali,
Tutetee kwa nguvu ,hadi haki iwe hali,
Haki zetu zilindwe,tusinyimwe kiholela.
MALENGA DENNIS KIOKO
MALENGA CHIPUKIZI
CHUO KIKUU CHA KITEKNOLOJIA CHA MURANG’A
Utabadilika lini?
Kila nikikutazama , ninabaki na kimako,
Ulianza tangu zama, kuiweka mirundiko,
Kuketi na kusimama, chaguo labaki lako,
Utabadilika lini?
Moyo wangu wazizima, nionapo mambo yako,
Japo binti warindima, kwa shauo na vicheko,
Umrudie Rahima, acha tabia za fuko,
Utabadilika lini?
Ulikuwa wa heshima, umezipa gawanyiko,
Vilabuni umekwama, na kuweka dhihiriko,
Na kulewa hujakoma, wala huna mshtuko,
Utabadilika lini?
Danguroni ni daima, waendekeza kituko,
Kila pembe unavuma, na kupewa nyingi heko,
Binti siyo chanda chema, megeuka mbwa koko,
Utabadilika lini?
Wakujuao wahema, kwazo nyingi sikitiko,
Vijusi umevitema, havipo tumboni mwako,
Watoa bila huruma, hujui kwetu ni mwiko?
Utabadilika lini?
Usoni umeparama , kwa kuweka michubuko,
Weupe waupa tama, haujali michujuko,
Kila akikutazama, wala huna tamaniko,
Utabadilika lini?
Alivyokufunda mama, tangu upo kwa mbeleko,
Nasaha umezichoma, hipendezi miondoko,
Binti sifa ulochuma, zinaalika maziko,
Utabadilika lini?
MIRUMBE NICKSON PETER
‘USTADHI BABU KIJANA’
Malkia wa nyikani!
Lau kunako mkinda, kikwi kwakwa husikika,
Itakuwa ni vinanda, na nyimbo za kutukuka,
Leo siku ya kalenda, kwa malkia wa nyika,
Ibada bora kutenda, bam’bam ni sadaka!
Aula nilizotunda, imara nimechuchuka,
Ngazi niliyoipanda, nimeweza kuinuka,
Aidha ulonifunda, imenipa kulimka,
Lisilo budi kutenda, bam’bam ya fanaka!
Injini heri kulinda, kwa kani kukurupuka,
Vipo vingi vya kupenda, ja milo ya malaika,
Ikama za kukuzinda, jaza akupe Rabuka,
Desturi ni kutenda, yanayoleta baraka!
Zumaridi yakulanda, zubarijadi na laka,
Auta pamwe migunda, iliyosiwa nafaka,
Malkia pia rinda, na nyoya la kuandika,
Amri yako kutenda, na lugojo kwa labeka!
Lakabu umeiwanda, za diwani kusomeka,
Ikisiri kila nyanda, insafu kusifika,
Kauli ulivyotanda, ladu za kutamanika,
Insi kwao kutenda, yale ya kunyiririka!
Ahadi ni kama nyonda, heri ikatimizika,
Wendo unapozienda, basi mbali utafika,
Aini kwa mai funda, zilungo kulainika,
Ndipo jema ukitenda, ngozi itatebwereka!
Yakini tamati kinda, jaaza imeniika,
Ila hapa parapanda, lahani zinainika,
Kingo ufu mziwanda, sanati kukamilika,
Afadhali kuyatenda, ustawi kuuteka!
VALENTINE OMONDI IBN-ALI
‘AL-USTAADH SHUARAI’
NAKURU
Sauti Yangu
Mimi mtoto mdogo,nabeba ndoto moyoni,
Nakosa fursa nyingi,naziona mbali sana,
Ninalia kimya kimya,navumilia uchungu,
Sauti yangu sikika, geuza maisha yangu.
Nimesoma kwa bidii,nikatumia juhudi,
Vyeti mimi navishika,lakini kazi ni shida,
Muda unaendelea,tumaini lapungua,
Sauti yangu sikika, geuza maisha yangu.
Serikali nisikie,kilio changu sikia,
Ninayo nguvu ya kazi, ninayo akili pia,
Ninapokosa ajira, kesho inadidimia,
Sauti yangu sikika, geuza maisha yangu.
Nataka kazi halali, nijenge yangu maisha,
Nisaidie wazazi, na waishi kwa faraja,
Bila ya kazi sahihi, ndoto zangu zafifia,
Sauti yangu sikika, geuza maisha yangu.
Sitaki na uhalifu, na sitaki njia mbaya,
Ninahitaji nafasi, nionyeshe na uwezo,
Ajira ni suluhisho,la shinda zao vijana,
Sauti yangu sikika, geuza maisha yangu.
Mwisho wangu nimefika,naenda nikitumai,
Kesho itakuwa bora,hiyo nafasi kipewa,
Nchi yangu niipende,kwa kazi pia na jasho,
Sauti yangu sikika, geuza maisha yangu.
FRIDAH MAKENA
‘Mwanga wa Jamii’
Tharaka _ Nithi