Mashairi

Jihadharini wamefunga

April 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 4

Nimeuchukua wino, karibuni kikaoni
Nataka maelewano, wamerejea nyumbani
Kataa mahusiano, uepuke gerezani
Jihadhari wamefunga, abadani waepuke

Usiwaone warembo, ukasahau sheria
Samaki kunasa chambo, hamna kufurahia
Usivutie urembo, mwishowe uje kulia
Jihadhari wamefunga, zipu usiifungue

Hata akikupa namba, mwenzangu usimchati
Usije kumpa mimba, mwishowe ‘jipate korti
Usimtoe ushamba, utakosa kisimati
Jihadhari wamefunga, sheria mdomo wazi

Usijitie tabuni, dhibiti zako hisia
Usiende gerezani, uhusiano hatia
Muda wapo likizoni, hatia kuwawazia
Jihadhari wamefunga, majuto ni mjukuu

Nafika takhmisa, hapa wino naufunga
Nafahamu sijakosa, kutetea vijulanga
Uamuzi wenu Sasa, kuunga ama kupinga
Jihadhari na wa shule, usijitie tabuni

EZEKIEL J. NZEKE
‘USTADH KARMA’
‘MIKOBA YA BABU’
CHUO KIKUU CHA MURANG’A

Makinika Likizoni!

Macho yangu nainua, kumshukuru Karima,
Muhula umefikia, hatima kiwa salama,
Wasomi meachilia, nyumbani tumewatuma,
Likizoni kitulia, wanafunzi makinika,

Ninaitoa wosia, kishairi ninasema,
Likizoni kitulia, na kutenda yalo mema,
Wazazi kutumikia, mtii wanayosema,
Likizoni kitulia, wanafunzi wajibika,

Wazazi nanyi sikia, watoto mkiwatuma,
Tabidi kukadiria, kuwakumbusha kusoma,
Msisahau kutoa, mwongozo ulio mwema,
Likizoni kitulia, wanafunzi durusuni,

Kabumbu kishabikia, na hata beti kutuma,
Na mechi kishangilia, msisahau kusoma,
Wachezaji hawa jua, donge nono wanachuma,
Likizoni kitulia, kumbuka wewe msomi,

Anasa kikimbilia, pabaya utajitoma,
Msukumo rika pia, tahadhari ja ukoma,
Mtegoni sije ngia, karaha ukaichuma,
Likizoni kitulia, shikilia maadili,

Mitandaoni kingia, wasapu jumbe kutuma,
Fesibuku kupekua, runingani macho pima,
Matumizi kupimia, uraibu sije kwama,
Likizoni kitulia, jipangieni ratiba,

Kalamu naachilia, mengine sitayasema,
Shairi kikariria, tapata niliyosema,

Januari kifikia, turudi shule salama,
Likizoni kitulia, tutende wema daima,

FRANKLIN MUKEMBU
‘Mawimbi Ya Nchi Kavu’
KAJUKI-NITHI

Kwaheri Baba

Hali imenifikia, kwaheri watupungia,
Kalamu pukutikia, muhali nikatungia,
Machozi tiririkia, huzuni kuniingia,
Akuweke Bwana Mungu, kwa haiba na uzuri!

Mnamo ya Jumamosi, Migori nilipoenda,
Sikuwa na wasiwasi, haliyo ni ya kuenda,
Siri huficha mikosi, mabaya yakituponda,
Akuweke Bwana Mungu, kwa haiba na uzuri!

Ukanitaja mi Juma, wewe ni kitambulisho,
Mimi huwa maamuma, Okal ukamilisho,
Upweke tena ni nyuma, niandike ukumbusho,
Akuweke Bwana Mungu, kwa haiba na uzuri!

Msiba menitawala, kutunga sina timamu,
Natembea bila kula, mdomoni sina hamu,
Chukuliwa halahala, kwangu kunao ugumu,
Akuweke Bwana Mungu, kwa haiba na uzuri!

Wema wote wa johari, upole bila ushari,
Utukufu wa hariri, waridi afu uturi,
Utuzwe vya kifahari, haliudi hali shwari,
Akuweke Bwana Mungu, kwa haiba na uzuri!

JUMA OKAL,
‘MALENGA USTADH’
MIGORI -KENYA

Kusomesha mke!

Sitachelea kusema, mambo yanoendelea,
Muda wangu wa uzima, mengi nimetionea,
Kuwaonya sitakoma, waume kuwatetea,
Ukosomesha mkeo, mwishowe atakuacha.

Sijakuwa sakubimbi, ni mafunzo naeneza,
Ningekuwa na filimbi, hakika ningepuliza,
Nikomeshe tabia mbi, maovu kuyafukuza,
Ukisomesha mkeo, kwingine tapata jiko

Usije kulialia, mambo yakenda mrama,
Kopi nayokuambia, uerevuke mapema,
Masomo kigharamia, ‘tafanyaje akihama?
Ukisomesha mkeo, utafanya kazi bure.

Usikuwe mfadhili, wewe siyo mhisani,
Fikiria mara mbili, usiliye kama nyani,
Kiharibu yako mali, utajutiya mwishoni,
Ukisomesha mkeo, mwingine tamnyakua.

Kitanda nacholalia, hujui wake kunguni,
Mke uficha tabia, akioleka mwanzoni,
Tajiri kimchumbia, atakuacha gizani,
Ukisomesha mkeo, atafuata mwenye mali.

Nomba radhi kina mama, kutoboa hino siri,
Tena sitasemasema,nyinyi viumbe wa heri,
Sita beti nitakoma, mzidi kutafakari,
Ukisomesha mkeo, faidako ni kilio.

Shem Nyang’echi Abuga
‘Prof-Mkereketwa’
Naivasha

Niko Kadi

Nandaa haya makala, kote yapate kutamba,
Sitaraji mjadala, ndo mwenende kinichimba,
Uchaguzi ndo aula, matayarisho twaamba,
Magenz nawahimiza, “Niko kadi, tuko kadi.”

Niko kadi sijalala, nang’uruma kama simba,
Nawe sichelewe bila, ya silaha ninakwomba,
Ili twambae madhila, tuteue murwa memba,
Magenz nawahimiza, “Niko kadi, tuko kadi.”

Vituo vingi mahala, vilo karibu na nyumba,
Kadi ziko kwa jumla, twendeeni kujipamba,
Liwe la lila na fila, vitambulisho ndo dimba,
Magenz nawahimiza, “Niko kadi, tuko kadi.”

Magenz mso holela, nasihi kukaza kamba,
Msijifanye mafala, mwendeni mso kimba,
Kwendea kadi si hila, pateni bila kuyumba,
Magenz nawahimiza, “Niko kadi, tuko kadi.”

Shughulini hino kila, kijana pasi kugomba,
Hata walofungwa jela, usajili uwe chemba,
Twenende hii hafla, tujazaneni sambamba,
Magenz nawahimiza, “Niko kadi, tuko kadi.”

Iwe faradhi ja sala, twaa kadi ya kufumba,
Nawakanya mlungula, pia yalo kujigamba,
Mliobeba himila, ya voti sigonge mwamba,
Magenz nawahimiza, “Niko kadi, tuko kadi.”

Wongozi ulo fadhila, kwunda usiyojigamba,
Wa kwinua masuala, ya ajira na mashamba,

Jitokeze kama swila, kura mpya pate umba.
Magenz nawahimiza, “Niko kadi, tuko kadi.”

Mjipe hi shangwe ala, kuchagua alo bomba,
Wa miradi tolatola, Kenya iwe wani namba,
Sajiliwa hu’ muhula, e vijana wa wajomba,
Magenz nawahimiza, “Niko kadi, tuko kadi.”

Tuwezeshe ewe Mola, ulo pekee Muumba,
Voti tuso gulagula, belele tweze kusomba,
N’tie nanga halahala, nitamatishe kulumba,
Magenz nawahimiza, “Niko kadi, tuko kadi.”

JAMES MUTWIRI WANJAGI
‘MALENGA MSIFIKA MSIKIVU’
CHUKA, THARAKA-NITHI

Mapenzi ni kitu gani?

Kwanza nilivumilia, kidhani utarejea,
Zote pande nangalia, mwishowe nimefikia,
Majuto yamenijia, moyo unaning’inia
Mapenzi ni kitu gani?

Ahadi uliotoa, kwa kinywa ukanambia,
Ukasema karibia, unipende narudia,
Leo ninasimulia, kinyume umenendea,
Mapenzi ni kitu gani?

Ulonadi liridhia, moyoni nikakutia,
Sura yako livutia,wengine nikachukia,
Nikaongeza hisia, liazizi kanijua,
Mapenzi ni kitu gani?

Hivi leo ninalia, uchungu umenitia,
Mapenzi ninalilia, ja mtoto wa hatia,
Nakaa kifikiria, moyo wangu kijutia,
Mapenzi ni kitu gani?

Kooni menifikia, sina la kujivunia,
Kiwa ungezingatia, penzi kuliangazia,
Leo nisingekulia, pumzi zikanishia,
Mapenzi ni kitu gani?

Dhiki umeniletea, nimekonda angalia,
Sina wa kunitetea, wahaka menivamia,
Penzi halijasalia, leo ninakuchukia,
Mapenzi ni kitu gani?

COLLINS O. KONGOTI
‘MWANAHABARI MSTAAFU’
MWALIMU – MATUNGU, KAKAMEGA

Mzalendo chukua kura

Amkeni sasa vijana, nchi hii ni yenu sote,
Msibaki tu mitaani, mkisubiri bahati itote,
Wakati ndio huu bwana, kucha kumekucha pote,
Mzalendo jitokeze, mapema chukua kura.

Kadi yako ndio silaha, ya kuleta mabadiliko,
Usiweke kando kando, chukua hatua kwa akili,
Jiandikishe kwa furaha, popote palipo kituo,
Mzalendo jitokeze, mapema chukua kura.

Uchaguzi unakuja, mwaka ujao si mbali,
Tusijae kwa mivutano, tuchague kwa busara,
Tutumie akili na hekima, viongozi wa kweli,
Mzalendo jitokeze, mapema chukua kura.

Usisubiri dakika ya mwisho, foleni ziwe ndefu,
Jisajili mapema leo, uepuke upungufu,
Chukua hatua sasa, tuchangie kwa amani,
Mzalendo jitokeze, mapema chukua kura.

Sauti yako ina nguvu, usidharau uwezo wako,
Chagua uongozi mwema, utatue changamoto,
Usiwe tu mtazamaji, simama kwa ajili yako,
Mzalendo jitokeze, mapema chukua kura.

Kenya yetu ni moja, tuitunze kwa upendo,
Kura yako ni umoja, inayovunja kila vizuizi,
Simama sasa kwa tija, dhihirisha vitendo,
Mzalendo jitokeze, mapema chukua kura.

DENNIS KIOKO
‘MHARIRI CHIPUKIZI’
CHUO KIKUU CHA KITEKNOLOGIA CHA MURANG’A

Yamekwisha!

Yamekwisha amaliza, taabu msalabani,
Yamekwisha nawajuza, tumetolewa dhambini,
Yamekwisha yote y’ giza, situnang’aa nuruni,
Yamekwisha yamekwisha, ameyamaliza kristu.

Yamekwisha kutabika, sisi sasa ni washindi,
Yamekwisha kuzunika, hizo ni kale vipindi,
Yamekwisha kuteseka, moyo wangu ni kilindi,
Yamekwisha yamekwisha, ameyamaliza kristu.

Yamekwisha uraibu, hatupo tena mateka,
Yamekwisha ya taabu, maisha tusiyotaka,
Yamekwisha ya aibu, ushindi ametupaka,
Yamekwisha yamekwisha, ameyamaliza kristu.

Yamekwisha utengano,umenoga urafiki,
Yamekwisha baya neno, na sasa ametubariki,
Yamekwisha ushindano, huisababisha chuki,
Yamekwisha yamekwisha, ameyamaliza kristu.

Yamekwisha ya mauti,uchungu wa jehenamu,
Yamekwisha ya kuchiti,ameimaliza hamu,
Yamekwisha sasa fiti,furaha ipo kwa ghamu,
Yamekwisha yamekwisha, ameyamaliza kristu.

Yamekwisha kufitini, ametupa ya ukweli,
Yamekwisha ya kuzini, metuahidi asali,
Yamekwisha ya utani, yupo yeye natujali,
Yamekwisha yamekwisha, ameyamaliza kristu.

Yamekwisha alisema, mwenyewe alihaidi,
Yamekwisha alitema, ametupa mpya kadi,

Yamekwisha yeye mwema, utukuke ewe dadi,
Yamekwisha yamekwisha, ameyamaliza kristu.

WACHIRA ROMEO MUGO
’MALENGA LANGU JICHO’
CHUO KIKUU CHA MURANG’A