Habari za Kitaifa

Serikali kutumia ruzuku ya Sh17 bilioni kulinda Wakenya dhidi ya bei ya juu ya mafuta

Na EDWIN MUTAI April 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SERIKALI inapanga kutumia ruzuku ya Sh17 bilioni kuwalinda Wakenya kutokana na ongezeko la bidhaa za mafuta katika siku 60 zijazo endapo vita vya Mashariki ya Kati vitaendelea zaidi ya Mei na Juni.

Waziri wa fedha, John Mbadi alifichua kuhusu mipango ya kutathmini upya ushuru wa bidhaa ikiwa ruzuku hiyo haitatosha kuzuia ongezeko la bei ya bidhaa za petroli, dizeli na mafuta ya taa zitakazotangazwa katika muda wa wiki mbili zijazo.

Hatua ya kurekebisha ushuru wa bidhaa wa asilimia 10 kwa bidhaa za mafuta inaonekana kuwa na umuhimu katika kusaidia kuzuia ongezeko linalotarajiwa la bei za mafuta kwenye ratiba ya Aprili 15 hadi Mei 14.

Tangazo la Mbadi limejiri wakati kampuni za kuuza mafuta tayari zikitangaza kuwa bei za mafuta huenda zikapanda kwa angalau Sh20 kutokana na ada ghali zinazotozwa shehena mbili za petroli iliyoagiziwa nje ya mkataba kati ya serikali.

“Katika ratiba mpya ya bei, hata hivyo, bei ya bidhaa, bima, tishio la vita na ada zinatarajiwa kuongezeka kutokana na vita. Tutabadilisha VAT ili bei zisiwe ghali kupindukia,” Bw Mbadi alieleza wabunge jana.

Kurekebisha ushuru wa bidhaa pamoja na ruzuku ya Sh17 bilioni ni mbinu ambazo serikali inapanga kutumia kuwalinda wateja katika miezi michache ijayo.

Ruzuku hiyo huenda isitoshe kuzuia ongezeko la bei ya mafuta, suala linalosisitiza sababu ya serikali kugeukia ushuru wa bidhaa.