Akili MaliMakala

Vita vya Mashariki ya Kati vyayumbisha sekta ya maua Kenya

April 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SEKTA ya maua nchini Kenya inakabiliwa na pigo kubwa kufuatia mzozo unaoendelea kati ya Iran na Israel, ambao umevuruga usafirishaji wa anga na biashara za kimataifa.

Katika kipindi cha wiki tatu zilizopita pekee, sekta hiyo imekadiria hasara ya karibu Dola za Amerika milioni 4.8 (zaidi ya Sh620 milioni), hali inayotia hofu kwa wadau wanaotegemea mauzo ya nje.

Changamoto kuu inayokumba wauzaji wa maua nje ya Kenya ni ucheleweshaji wa mizigo, unaosababisha bidhaa kuharibika au kupoteza ubora wake kabla ya kufika sokoni.

Hali hii imechangia si tu upotevu wa moja kwa moja wa takribani Dola milioni 2.1 za maua yaliyochelewa kufika, bali pia kushuka kwa bei ya maua yenye thamani ya Dola milioni 2.7 kutokana na kupungua kwa ubora wake.

Sekta ya maua, ambayo inategemea sana ubichi wa bidhaa na ratiba madhubuti za usafirishaji, iko katika hatari kubwa pindi tu kunapotokea hitilafu kwenye mifumo ya usafiri.

Maua ni zao linalohitaji kufikishwa sokoni haraka; hivyo kuchelewa hata kwa saa chache kunaweza kubadilisha kabisa thamani yake.

Mojawapo ya kampuni inayokuza maua ya kuuza ng’ambo Kenya. Picha|Sammy Waweru

Kulingana na Baraza la Maua Kenya (KFC), mzozo huo umeathiri pakubwa masoko muhimu ya Mashariki ya Kati, ambayo ni sehemu muhimu ya mauzo ya maua ya Kenya.

“Mbali na kuwa soko lenyewe, mataifa ya Gulf pia hutumika kama vituo vya usafiri vinavyounganisha Kenya na masoko ya Ulaya na kwingineko. Mvutano unaoendelea kati ya Israili na Iran umepelekea kufungwa kwa baadhi ya anga, kubadilishwa kwa njia za ndege, pamoja na kuongezeka kwa tahadhari za kiusalama,” KFC inasema.

Barazaza hilo la maua nchini linasema matokeo yake ni kupungua kwa nafasi ya mizigo kwenye ndege na kusababisha ucheleweshaji mkubwa wa usafirishaji.

Aidha, KFC inakadiria kuwa uwezo wa usafirishaji wa anga nchini umeshuka kwa hadi asilimia 30, huku kimataifa ukipungua kwa kati ya asilimia 18 hadi 20.

“Wauzaji wengi sasa wanaripoti kucheleweshwa kwa mizigo kwa hadi saa 48, kufutwa kwa safari za ndege na mabadiliko ya mara kwa mara ya ratiba,” inadokeza.

Maua yanapochelewa kufika sokoni, mara nyingi hukosa minada yenye bei nzuri au hukataliwa kabisa kutokana na kushuka kwa ubora. Pale yanapokubaliwa, huuzwa kwa bei ya chini, jambo linaloongeza hasara.

Mbali na hilo, KFC inasema gharama za usafirishaji zimepanda kwa kasi, ambapo kwa sasa wauzaji wanalazimika kulipa zaidi ya Dola 5.30 kwa kilo.

Mashada ya maua kwenye maonyesho awali Nairobi. Picha|Sammy Waweru

Hata soko la Ulaya, ambalo ndilo kuu kwa maua ya Kenya, limeathirika kutokana na ndege kulazimika kutumia njia ndefu zaidi ili kuepuka maeneo yenye migogoro, hali inayoongeza gharama na muda wa safari.

Kwa mashamba yanayotegemea sana masoko ya Mashariki ya Kati, athari zimekuwa mbaya zaidi. “Baadhi yao yameripoti kuporomoka kwa mapato kwa hadi asilimia 75, huku hasara za kila wiki zikikadiriwa kuzidi Dola milioni 1.3 iwapo hali itaendelea kuwa hivyo,” KFC inaonya.

Kutokana na hali hiyo, Baraza la Maua Kenya linashinikiza serikali kuharakisha kurejesha fedha za Ushuru (VAT) zinazodaiwa wauzaji nje ya nchi, ambazo zinafikia karibu Sh10 bilioni.

Hatua hiyo inaonekana kuwa muhimu kusaidia biashara hizi kupata mtaji wa kuendesha shughuli zao wakati huu mgumu.

Licha ya changamoto hizo, uzalishaji wa maua nchini bado uko imara. Tatizo kubwa linaloikumba sekta kwa sasa si uzalishaji, bali ni uwezo wa kuyafikisha maua hayo sokoni kwa wakati ufaao na kwa ubora unaohitajika.

Mwaka 2024, sekta ya maua ilichangia takribani Dola milioni 835 (Sh108.59 bilioni) katika mapato ya mauzo ya nje na kuajiri mamia ya maelfu ya watu.

Hivyo basi, athari za mzozo huu hazigusi tu biashara, bali pia maisha ya wafanyakazi wengi na uthabiti wa uchumi wa taifa kwa ujumla.