Wafugaji wa maeneo kame wabuni mbinu za kulinda mifugo dhidi ya ukame
KIANGAZI kikali kilichoshuhudiwa nchini kati ya mwaka 2021 na 2022 kiliacha majeraha makubwa kwa wakulima na wafugaji, hasa katika maeneo kame na nusu-kame (ASAL), huku mali ya mabilioni ya pesa ikipotea kutokana na vifo vya mifugo.
Ukame huo ulitajwa kuwa mbaya zaidi katika kipindi cha zaidi ya miaka 40, na kwa wafugaji wengi ulikuwa pigo lisilosahaulika.
Elisha Shapara, mfugaji kutoka kijiji cha Oloirimirimiri katika eneo la Nairraballa, Kaunti ya Kajiado, ni miongoni mwa waliopoteza mifugo bila msaada wowote, kutokana na uhaba wa maji na malisho.
“Upungufu wa maji na malisho ndio changamoto kubwa katika maeneo kame,” anasema Shapara, ambaye hufuga ng’ombe, mbuzi na kondoo.
Kwa muda mrefu, wafugaji katika maeneo ya ASAL wamekuwa wakitegemea malisho ya asili. Hata hivyo, mabadiliko ya tabianchi yamevuruga mifumo ya hali ya hewa, na kufanya mbinu hizo za jadi kutokuwa za kutegemewa tena.
Ili kupunguza hasara, Shapara sasa amebadili mkakati. Ameanza kulima nyasi zinazostahimili ukame kama Boma Rhodes na Maasai lovegrass katika sehemu ya shamba lake. Nyasi hizi huvunwa na kuhifadhiwa kama majani makavu (hay), ambayo hutumika kulisha mifugo wakati wa kiangazi.

“Tunapata mafunzo ya jinsi ya kuhifadhi nyasi kama hay ili kuhakikisha mifugo hawakosi chakula wakati wa ukame. Kabla ya hapa, tulikuwa tunapoteza mifugo wengi sana,” anaeleza.
Mbinu kama hizi sasa zinaenea kwa kasi katika kaunti za Kajiado, Narok, Laikipia na Samburu, ambako wafugaji wanazidi kuwekeza katika uzalishaji na uhifadhi wa malisho kama njia ya kukabiliana na athari za tabianchi.
Juhudi hizi zinaungwa mkono na serikali pamoja na washirika wa maendeleo, wakiwemo mashirika yasiyo ya kiserikali na sekta binafsi, wanaohamasisha kilimo endelevu, huduma za mifugo na upatikanaji wa masoko.
Mojawapo ya mipango muhimu ni mradi wa Kenya Pastoral Market Development (KPMD), ulioanzishwa mwaka 2023.
Mradi huu unatekelezwa katika kaunti za Kajiado, Narok na Samburu kwa lengo la kuunganisha wafugaji na masoko ya ndani na kimataifa.
Kupitia mradi huo, vituo vya kukusanya na kuhudumia mifugo vimeanzishwa karibu na jamii za wafugaji, ili kurahisisha biashara na kuboresha ubora wa mifugo kabla ya kuuzwa.
Aidha, huduma za afya ya mifugo zimeimarishwa, ikiwa ni pamoja na utoaji wa chanjo dhidi ya magonjwa hatari kama homa ya miguu na midomo (FMD), caprine pleuropneumonia (CCPP) na peste des petits ruminants (PPR).

Kulingana na Profesa Ruth Kiraka, msimamizi wa KPMD, afya ya mifugo ni nguzo muhimu katika ustahimilivu wa wafugaji.
“Chanjo na huduma bora za mifugo zinasaidia kupunguza vifo, hasa wakati wa ukame ambapo mifugo huwa dhaifu,” anasema.
Kwa upande wake, mfugaji Simon Shapara anakumbuka jinsi ukame wa 2021–2022 ulivyomkosesha karibu kila kitu. Wakati huo alikuwa na ng’ombe 50 pamoja na mbuzi na kondoo 150. Hata hivyo, alipoteza zaidi ya nusu ya mifugo wake.
“Nilipoteza ng’ombe 28 na mbuzi na kondoo 70. Ilikuwa hali ya kusikitisha sana,” anakumbuka.
Hata hivyo, hali imeanza kubadilika. Kupitia huduma bora za mifugo na upatikanaji wa masoko, ameanza kujijenga upya na kuongeza idadi ya mifugo wake.
Kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, Chuo Kikuu cha Strathmore na kampuni ya LiveMo wanaendelea kuhamasisha wafugaji kuhusu umuhimu wa kulima nyasi zinazostahimili ukame, kuhifadhi malisho, na kuhakikisha mifugo inapokea chanjo kwa wakati.
George Ndung’u kutoka LiveMo anasisitiza kuwa uzalishaji na uhifadhi wa malisho ni nguzo muhimu ya kukabiliana na ukame.
“Ghala moja lina uwezo wa kuhifadhi hadi marobota 20,000 ya hay, ambayo ni akiba muhimu wakati wa kiangazi,” anasema.
Kwa wafugaji wengi, kila robota ya hay iliyohifadhiwa leo ni kama bima dhidi ya majanga ya kesho.
Mbali na kulinda mifugo, mbinu hizi pia zimeanza kuboresha kipato chao, na kuwawezesha kukidhi mahitaji ya familia hata wakati wa changamoto za tabianchi.