Habari Mseto

Pasta Muiru apambana kuokoa mali yake ya Sh216m isipigwe mnada

Na SIMON CIURI April 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MIAKA miwili baada ya kuibuka wa tano katika uchaguzi wa urais wa mwaka wa 2007, mchungaji Pius Muiru, mwanzilishi wa kanisa la Maximum Miracle Centre, aliingia katika Equity Bank, barabara ya Tom Mboya jijini Nairobi na kuchukua mkopo wa Sh216 milioni.

Mchungaji Muiru, aliyepata kura 9,000 katika uchaguzi wa Desemba 27, 2007, alipata mkopo huo mwaka wa 2010.
Vyanzo vinaeleza kuwa mali aliyoweka dhamana ilikuwa ya takriban Sh960 milioni.

Hata hivyo, mkopo huo sasa umegeuka kuwa jinamizi kwa mhubiri huyo aliyewahi kuwa na wafuasi wengi na ushawishi mkubwa.

Anajulikana kama mmoja wa waanzilishi wa uinjilisti kupitia redio na televisheni nchini, akitumia kauli mbiu yake maarufu “Kuna Nuru Gizani”.

Sasa, Muiru amewasilisha kesi mahakamani akitaka kuzuia mali yake nyingi, ikiwemo ardhi na majengo ya kupangisha katika kaunti za Nairobi na Kiambu, kupigwa mnada. Anamiliki mali hiyo pamoja na mkewe, Lucy.

Anadai kuwa deni lililosalia ni Sh27 milioni pekee, lakini benki inapinga madai hayo.

Ameeleza mahakama kuwa tangu janga la Covid-19 mwaka wa 2020, huduma za kanisa lake zilipungua, na hivyo kuathiri uwezo wake wa kulipa mkopo.

Kupitia hati ya kiapo, anahofia kuwa benki inaweza kuuza mali hiyo bila msingi wa kisheria.

Ameomba mahakama itoe amri ya kuzuia hatua hiyo hadi kesi itakaposikilizwa na kuamuliwa.

Muiru na mkewe wanasema tayari wamelipa jumla ya Sh350.6 milioni, wakidai kuwa benki iliongeza deni kwa njia isiyo halali kwa zaidi ya Sh122.8 milioni.

Kulingana nao, salio halisi linapaswa kuwa takriban Sh27.9 milioni.

Kwa upande wake, Equity Bank imeambia mahakama kuwa mlalamishi alishindwa kulipa mkopo kati ya mwaka 2011 na 2016, hali iliyosababisha riba na adhabu kuongezeka.

Benki hiyo pia imesema haijaanza rasmi mchakato wa kuuza mali hiyo, hivyo kesi hiyo imewasilishwa mapema.

Mahakama, kupitia Jaji M. Muigai, imesitisha kwa muda uuzaji wa mali hiyo hadi kesi itakaposikilizwa Julai 8, 2026 mbele ya Jaji Njoki Mwangi.

Wakati huo huo, matatizo ya mchungaji huyo hayaishii hapo. Katika kesi nyingine ya awali, alimfungulia kesi mchungaji mwenzake Andrew Mkare kuhusu umiliki wa ardhi ya kanisa eneo la Watamu.

Hata hivyo, mahakama ilitupilia mbali kesi hiyo baada ya kubaini kuwa Mkare alinunua ardhi hiyo kwa fedha zake binafsi.

Muiru alidai kuwa ardhi hiyo ilinunuliwa kwa fedha za kanisa, lakini mahakama ilitupilia mbali madai hayo.

Katika uamuzi wake, jaji alibaini kuwa Mkare aliwasilisha ushahidi kuwa alinunua ardhi hiyo kwa fedha zake binafsi pamoja na mikopo kutoka benki na chama cha akiba.

Mahakama pia ilibaini kuwa hakukuwa na ushahidi wa michango kutoka kwa waumini kuelekea ununuzi wa ardhi hiyo.