Kimataifa

Khamenei mpya ni majeruhi – Ufichuzi

Na REUTERS April 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

DUBAI, MILKI YA KIARABU:

KIONGOZI mpya wa kidini nchini Iran, Mojtaba Khamenei, angali anauguza majeraha mabaya ya uso na mguu aliyopata kwenye mashambulizi yaliyomuua baba yake mwanzoni mwa vita, watu watatu walio karibu naye walieleza Reuters.

Uso wa Khamenei uliharibiwa katika shambulizi lililofanyika makazini mwa kiongozi wa kiroho, baba yake Mojtaba, jijini Tehran naye akajeruhiwa vibaya kwenye mguu mmoja au miwili, duru zote tatu zilisema.

Kiongozi huyo mwemye umri wa miaka 56 hata hivyo anapata nafuu kutokana na majeraha yake na angali imara kiakili, kulingana na watu waliochelea kutajwa kutokana na uzito wa suala hili.

Anashiriki mikutano na maafisa wakuu kielektroniki mbali na kushiriki katika kufanya maamuzi kuhusu masuala makuu vikiwemo vita na majidiliano; walisema wawili miongoni mwao.

Suala kuhusu iwapo afya ya Khamenei inamruhusu kuendesha masuala ya kitaifa limejiri wakati wa tishio kuu zaidi kwa Iran katika miongo kadhaa, huku mazungumzo ya ngazi za juu kuhusu amani na Amerika yakianza katika jiji kuu la Pakistani, Islamabad, Jumamosi.

Maelezo ya wandani wa Khamenei yanatoa taswira ya kina kuhusu hali ya kiongozi huyo kwa majuma kadhaa.

Reuters haikuweza kuthibitisha maelezo yao kwa njia huru.

Mahali alipo Khamenei, hali yake na uwezo wa kutawala ungali kitendawili kwa umma, pasipo picha, video wala sauti yake iliyorekodiwa tangu shambulizi la angani na uteuzi wake uliofuatia kuchukua nafasi ya baba yake mnamo Machi 8.

Umoja wa Mataifa (UN) nchini Iran haukujibu maswali ya Reuters kuhusu kina cha majeraha ya Khamenei wala sababu ya kutojitokeza kwenye picha au sauti zozote zilizorekodiwa.

Khamenei alijeruhiwa Februari 28, siku ya kwanza ya vita vilivyoanzishwa na Amerika na Israeli, katika shambulizi lililomuua baba na mtangulizi wake Ayatollah Ali Khamenei, aliyetawala tangu 1989.

Mkewe Mojtaba na shemeji zake wawili ni miongoni mwa jamaa wengine wa familia waliouawa katika shambulizi hilo.

Hakuna taarifa rasmi kuhusu kiwango cha majeraha ya Khamenei.

Hata hivyo, msomaji wa habari katika runinga ya kitaifa alimtaja kama “janbaz”, jina linalotumika kwa wale wanaojeruhiwa vibaya vitani, baada ya kutajwa kiongozi wa kiroho.