Mwanamume kiwete ashtakiwa kumlima rungu chokoraa aliyeishia kufariki
MWANAMUME mwenye umri wa miaka 59 anayeishi na ulemavu amekiri kortini alimuua kijana wa kurandaranda mitaani, almaarufu chokoraa, Desemba mwaka uliopita katika barabara ya Gaberone.
Joseph Ochieng almaarufu Kamrudu aliungama mbele ya hakimu mwandamizi Geoffrey Onsaringo kwamba “alimtandika rungu la kichwani marehemu baada ya kumshambulia.”
Ochieng aliungama kwamba usiku wa Desemba 5, 2025 akiwa amelala kwenye kiti chake cha magudurumu alishtushwa na kichapo kichwani.
“Nilishtushwa usingizini na kichapo kichwani. Niliamka na kujifunua uso. Nilimwona kijana barobaro amesimama karibu nami ameshika rungu akijiandaa kunishambulia tena,” Ochieng alieleza korti.
Alisema alisukuma kiti chake cha magurudumu karibu na mshambulizi wake kisha akamnyang’anya hilo rungu.
Mshtakiwa aliyekiri shtaka la kuua bila ya kukusudia aliungama “nilimnyang’anya hilo rungu mshambulizi wangu. Kwa nguvu zangu zote nilimtandika rungu la kichwa akaanguka kwenye lami.”
Ochieng alisema mhasiriwa alianguka kwa kishindo kwenye lami.
Mhasiriwa hakusimama tena, hakimu alielezwa.
Mshtakiwa alisema alishtuka mno kisha akaamua kukaa karibu na mwili wa chokora huyo.
“Polisi wakiwa wanashika doria walipitia kwenye barabara hiyo kisha wakanipata nikilinda hiyo maiti. Nilikamatwa na kupelekwa rumande kisha hatimaye nikashtakiwa,” Ochieng alimweleza hakimu.
Mshtakiwa aliomba msamaha akisema, “Chokora huyo ndiye alinishambulia bila sababu lakini nilipojikinga dhidi ya shambulizi hilo matokeo yakawa ya kuhuzunisha.”
Mshtakiwa aliomba msamaha na kumsihi hakimu “ampe fursa ya kubadilika zaidi.”
Mshtakiwa huyo alieleza mahakama amejifunza mambo mengi na kugundua kwamba “hasira ni hasara.”
Kiongozi wa mashtaka aliomba hilo lichukuliwe kuwa kosa la kwanza kutendwa na mshtakiwa.
Hakimu aliamuru mshtakiwa azuiliwe hadi Aprili 29, 2026 atakapopitisha adhabu.
Pia aliomba afisa wa urekebishaji tabia amhoji mshtakiwa na kuwasilisha ripoti yake Aprili 29, 2026.
Mshtakiwa alipelekwa kuzuiliwa katika gereza la Viwandani.
Alikamatwa Desemba 5, 2025 baada ya kisa hicho. Amekuwa ndani wakati huu wote.