Akili MaliMakala

Uyoga wamkomboa

Na SAMMY WAWERU April 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

WAKATI janga la Covid-19 lilipotikisa uchumi na kusambaratisha ajira kwa maelfu ya vijana nchini Kenya, wengi walibaki kwenye njia panda.

Lakini kwa Kevin Mwangi Kamau, changamoto hiyo haikuwa mwisho—bali mwanzo wa safari mpya ya mafanikio katika kilimo cha uyoga, sekta ambayo haijaingiliwa na wengi kikamilifu lakini yenye faida kubwa.

Akiwa amezoea pilikapilika za sekta ya usafiri wa umma tangu mwaka 2016, Mwangi alifanya kazi kama utingo na baadaye dereva wa matatu jijini Nairobi na maeneo jirani.

Kila siku alipata karibu Sh2,000—kipato kilichomwezesha kukimu mahitaji ya familia yake changa. Hata hivyo, mlipuko wa Covid-19 uligeuza kila kitu. “Mlipuko wa virusi vya corona ulipunguza mapato yangu kwa kiwango kikubwa kutokana na vizuizi vya usafiri na kufungwa kwa shughuli nyingi,” anakumbuka.

Mapato yake yalishuka kwa zaidi ya asilimia 75, na hatimaye akapoteza kazi kabisa. Akiwa na stashahada ya Umekanika lakini bila ajira, alijikuta akilazimika kufikiria upya mustakabali wake.

Ndipo wazo la kilimo cha uyoga likazaliwa. Akiwa na umri wa miaka 32 wakati huo, Mwangi alipata ushauri kutoka kwa ndugu yake akimhimiza kutafiti kuhusu kilimo hicho. Licha ya kutokuwa na uzoefu, aliamua kujifunza kupitia mitandao, hasa YouTube, akifuatilia mafunzo ya wakulima wengine.

 

Kwa m

Kevin Mwangi Kamau akionyesha uyoga aliolima Nairobi. Picha|Sammy Waweru

taji wa Sh15,000—uliotokana na akiba yake na msaada kutoka kwa mama yake, Mwangi alianza mradi wake mdogo katika Kaunti ya Nyandarua. Alinunua mbegu za uyoga (spawn) kwa Sh600 kwa lita moja, akianza na lita nne. Akitumia mabua ya ngano kama malighafi, alijenga banda la mita 3 kwa 3 kwa usaidizi wa ndugu yake.

“Nilianza na marobota 25 ya mabua ya ngano na kuvuna kilo 10 za uyoga. Ndani ya wiki moja, uzalishaji uliongezeka hadi kilo 30,” anaeleza. Mafanikio hayo ya awali yalimwezesha kurejesha mtaji wake kwa muda mfupi—ishara kwamba alikuwa kwenye mkondo sahihi.

Hata hivyo, changamoto hazikukosekana. “Miundombinu duni, gharama kubwa za usafirishaji na ukosefu wa soko lenye ushindani zilinilazimu kuhamia Nairobi ili kusogesha bidhaa zangu karibu na wateja,” anaelezea.

Hatua hiyo iligeuka kuwa ya kimkakati. Leo hii, Mwangi ni miongoni mwa wazalishaji wanaokua kwa kasi katika sekta ya uyoga kupitia kampuni yake ya Seattle Organic Farm. Anazalisha aina za oyster na button—aina zinazopendwa zaidi sokoni.

Katika mradi wake ulioko Mukuru kwa Njenga, Embakasi, Kaunti ya Nairobi ana vyumba vinane vya uzalishaji, akizalisha zaidi ya kilo 2,000 za uyoga aina ya oyster na kilo 800 za button kila mwezi.

Uyoga umeendelea kupata umaarufu, hasa mijini, kutokana na thamani yake ya lishe. Una protini, fiber, vitamini B, pamoja na madini muhimu kama selenium—virutubisho vinavyoimarisha afya ya mwili.

Kutokana na ongezeko la magonjwa yanayohusishwa na mtindo wa maisha, watumiaji wengi wanageukia uyoga kama njia mbadala ya protini ya nyama.

“Kwa sasa, gramu 250 za uyoga huuza Sh250, ingawa bei inaweza kushuka hadi Sh150 kulingana na soko,” akaambia Akilimali Dijitali wakati wa mahojiano.

Uyoga ukiendelea kukua kwenye mojawapo ya vyumba ambavyo Kevin Mwangi Kamau hutumia kuzalisha Nairobi. Picha|Sammy Waweru

Ili kupunguza gharama ya uzalishaji, Mwangi amekumbatia teknolojia ya Juncao—mbinu inayotumia nyasi maalum, maganda ya mpunga na chokaa kukuza uyoga.

“Mbinu hii imepunguza gharama kwa zaidi ya asilimia 50 na kuongeza ufanisi,” anasema. Licha ya mafanikio hayo, anakiri kuwa soko bado lina changamoto. Mabroka wameendelea kutawala bei, hali inayopunguza faida kwa wazalishaji.

Aidha, uelewa mdogo wa walaji kuhusu uyoga unaathiri mahitaji ya bidhaa hiyo. Ili kukabiliana na hali hiyo, Mwangi ameanza kuongeza thamani ya bidhaa zake kwa kuzichakata—akikaanga uyoga na kuongeza viungo ili kuvutia walaji wapya. Pia, huuza moja kwa moja kwa hoteli na maduka makubwa, hatua inayomsaidia kuepuka madalali.

Mbali na kujijengea kipato, ameweza pia kuajiri vijana 10, wakiwemo wanawake, katika mradi wake—akitumia biashara hiyo kama chombo cha kuboresha uchumi kwa jamii. Kwa sasa, analenga kupanua soko lake hadi nje ya nchi, hasa katika mataifa ya Uarabuni ambako mahitaji ya uyoga yanaongezeka.

Na je, anaweza kurejea katika sekta ya matatu? “Hata kwa dawa sitaacha kilimo cha uyoga,” anasema kwa msisitizo. Kwa Mwangi, kilimo si tu chanzo cha mapato—ni uhuru. Uhuru wa kujisimamia, kufanya maamuzi, na kujenga maisha kwa masharti yake mwenyewe.

Anatoa wito kwa vijana kubadili mtazamo kuhusu kilimo na kukiona kama fursa halisi ya kujiajiri na kufanikiwa. “Kilimo kina nafasi kubwa sana—kinahitaji tu ubunifu, uvumilivu na uthabiti,” anasisitiza.