SIFUNA ANATOSHA MBOGA! Linda Mwananchi latathmini Sifuna agombee urais 2027
KUNDI la Linda Mwananchi ambalo linahusishwa na Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna na Gavana wa Siaya James Orengo linatathmini mikondo miwili ikiwemo seneta huyo wa Nairobi kuwania urais mnamo 2027.
Huku kundi hilo likiendelea kujijenga nyanjani hasa kwa kuwalenga wanasiasa vijana, Linda Mwananchi imeshatangaza kuwa haitaunga mkono kuchaguliwa tena kwa Rais William Ruto.
“Mikakati yetu ni kuwa na vuguvugu imara ambalo litatikisa nchi na kusababisha Wakenya wayaone mambo kwa njia tofauti,” akasema Bw Sifuna kwenye mahojiano na Taifa Leo.
Kwa sasa kambi ya Linda Mwananchi haionekani hata kuegemea mrengo wa upinzani wa Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua.
Kwa mujibu wa Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Multimedia Profesa Gitile Naituli Bw Sifuna kwa sasa ndiye mwanasiasa wa kutazamwa huku siasa za 2027 zikiendelea kushika kasi.
“Edwin Sifuna ni mwanasiasa ambaye anatazamwa na kila mtu kwa sababu ya kuendelea kupanda kwa nyota yake ya kisiasa,” akasema Profesa Naituli.
Msomi huyo anasema kuwa iwapo Linda Mwananchi itaamua kufanya kazi na upinzani na kuwe na tikiti ya Kalonzo-Sifuna, basi Rais William Ruto atakuwa na mtihani mkubwa wa kutetea wadhifa wake.
Upinzani unaonekana umeanza kumnyemelea Bw Sifuna na jana Msemaji wao Dkt Mukhisa Kituyi alisema wanatathmini kufanya kazi naye katika hesabu zao za kisiasa.
“Lazima tuongee nao na kuona mwelekeo ambao wanauchukua,” akasema Dkt Kituyi akithibitisha kuwa wapo tayari kwa ushirikiano wa kisiasa na kundi la Linda Mwananchi.
Kwa upande wake, Bw Orengo anaonekana analenga kuendelea kuyapigania mageuzi ndani ya ODM akisema kuwa ODM inapoteza falsafa yake ya uongozi kwa kushirikiana na Rais Ruto.
Bw Orengo anaonekana kulenga uimara wa Linda Mwananchi hata baada ya siasa za 2027 akionekana kama mrengo ambao utayaleta mageuzi nchini.
“Sisi bado ni wanachama wa ODM wala hatulengi kuondoka chamani. Tunapambana na kupigana ndani ya chama,” akasema.
Hasa Gavana huyo anasema ushirikiano wa ODM-UDA utalemaza na kudhoofisha chama hicho kabisa kiasi cha kufanya kipoteze maazimio na msingi wake.
“Chama kilianzishwa kuendeleza msingi na uongozi bora lakini kwa sasa hilo halifanyiki. Hatuwezi kusema kuwa hatutakuwa na mgombeaji wa urais kwa sababu ODM ni chama ambacho kimekuwa na mwongozo imara na lazima kisalie dhabiti,” akaongeza.
Viongozi wa Linda Mwananchi wanasema kuwa ODM kuwa na mgombeaji wa urais kutasaidia kufungua njia na mwelekeo mpya baada ya kifo cha Raila.
Aidha bila mwaniaji wa urais, Bw Orengo anasema ODM huenda ikamezwa na vyama pinzani na hata kupoteza idadi yake bungeni.