Kimataifa

Iran yafunga tena Mkondo wa Hormuz

Na MASHIRIKA April 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

IRAN imefunga tena Mkondo wa Hormuz muda mfupi baada ya kuifungua kutokana na kile kilichotaja kama vitisho na vikwazo vya Rais Donald Trump.

Tehran ilikuwa imefunga kwa kiasi kikubwa njia hiyo muhimu ya usafirishaji wa mafuta tangu Amerikani na Israeli zilipoishambulia nchi hiyo Februari 28.

Makubaliano ya kusitisha mapigano kati ya Amerika na Iran yanatarajiwa kkukamilika Aprili 22.

Rais wa Amerika, Donald Trump alisema kuwa kizuizi kwa wanajeshi wa bandari za Iran kitaendelea hadi makubaliano ya amani yatakapofikiwa kati ya nchi hizo mbili.

“Hii ni siku nzuri na ya kipekee kwa dunia,” alisema Trump.

Makundi ya usafirishaji baharini yalisema bado yanathibitisha kama ni salama kwa meli kupita katika Mkondo huo, huku ufuatiliaji ukionyesha kuwa ni meli chache tu ndizo zimeonekana.

Tangazo hilo la Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Abbas Araghchi, ilitolewa Ijumaa, siku ya kwanza kamili ya usitishaji mapigano wa siku 10 kati ya Israeli na Lebanon.

“Kwa kuzingatia usitishaji mapigano nchini Lebanon, Mlango wa Hormuz uu wazi kabisa kwa kipindi kilichobaki cha usitishaji mapigano kupitia njia iliyoratibiwa kama ilivyotangazwa tayari na Shirika la Bandari na Masuala ya Bahari la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran,” aliandika kwenye mtandao wa X.

Baadaye, runinga ya taifa ya Iran ilinukuu afisa mwandamizi wa kijeshi akisema kuwa meli hizo zitaruhusiwa kupita kupitia njia maalum, na kwamba kupita kwa meli za kijeshi katika Mkondo huo bado kumepigwa marufuku.

Inaaminika kuwa taarifa hiyo inarejelea ramani na njia mbili zilizobainishwa na Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC), ambazo ziliripotiwa kwa upana na vyombo vya habari vya Iran wiki iliyopita.

Baadhi ya vyombo vya habari vya Iran vilikosoa ujumbe wa Araghchi.

Shirika la Habari la Tasnim, linalohusishwa na IRGC, lilitaja ujumbe huo kuwa mbaya na usio na ukamilifu.

Wengine walitaka mamlaka za Iran kutoa ufafanuzi zaidi.

Spika wa Bunge la Iran, Mohammad Bagher Ghalibaf, ambaye aliongoza ujumbe wa Iran katika mazungumzo ya hivi karibuni na Amerika mjini Islamabad, alisema kwenye X kuwa Donald Trump alitoa madai saba ndani ya saa moja, na yote saba yalikuwa ya uongo.

Kuhusu Mkondo wa Hormuz, alisema kuwa iwapo utazuiliwa na Amerika basi hautabaki wazi.

Iran ni mshirika wa Hezbollah, kundi la kisiasa na kijeshi la Waislamu lililoko kusini mwa Lebanon.

Israeli ilianzisha mashambulizi nchini Lebanon machi 2 kujibu mashambulizi ya Hezbollah, ambayo yalikuwa ya kulipiza kisasi dhidi ya Amerika na Israeli kwa mashambulizi yao dhidi ya Iran.