Habari

Caroli Omondi awakejeli viongozi wa Linda Ground akisema wamekaribishwa Linda Mwananchi

Na CECIL ODONGO April 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MBUNGE wa Suba Kusini, Caroli Omondi amewakejeli viongozi wa Linda Ground kutokana na masaibu wanayoyapitia mikononi mwa UDA, na kusema wapo tayari kuwakaribisha tena ila kwa masharti makali.
Bw Omondi alisema kuwa viongozi wa ODM ambao wana ukuruba na UDA wanaweza kuruhusiwa tu kuungana na wale wa Linda Mwananchi iwapo wataachilia viti vyote vya uongozi ODM.
“Sasa Linda Ground wamekwama wanataka kupiga kona na kurejea hapa kwetu kwa sababu wamekaa kwa mawe. Hawa wamekuwa wakituimbia ‘Tu tam’ na kuenda kinyume na jinsi ambavyo Baba alituambia tusiimbe,” akasema Bw Omondi.
“Wakitaka kuongea na sisi lazima waachilie au kujiuzulu nyadhifa zao. Watambue katibu halisi wa ODM ni Edwin Sifuna ambaye ataitisha Kongamano la Kitaifa la Wajumbe wa Chama (NDC) kisha viongozi wapya wachaguliwe,” akaongeza Bw Omondi.
Mbunge huyo anayehudumu muhula wa kwanza alisema bila kutimizwa kwa masharti hayo hawawezi kukubali kuungana na kundi la Linda Ground.
“Kama si hivyo wakwame na wakwende huko na Ruto ambaye hawapeleki mahala popote. Hata wanadanganywa kuwa watapelekwa Singapore lakini sisi umakinifu wetu si kwenye uongoa kama huo bali tunanyemelea kura za vijana wa Gen Z na tuna imani tutazipata,” akasema Bw Omondi.
Linda Mwananchi inatarajiwa kuandaa mkutano wa kisiasa Kisumu na Vihiga wikendi hii na wamesema hawatatereshwa na vitisho kuwa mikutano yao itasamabaratishwa na wahuni.
“Tuko tayari kuwakabili kwa sababu sisi si waoga. Kisumu ni ngome ya baba na tutafanya mkutano wetu kwa amani na watu wajitokeze kutukaribisha,” akasema Bw Omondi.
Mkutano huo wa Nakuru ulihudhuriwa na viongozi wa Linda Mwananchi wakiongozwa na Gavana wa Siaya James Orengo, Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino miongoni mwa wanasiasa wengine.
Kabla ya kuhutubia mkutano wa kisiasa uwanja wa Mazembe Nakuru Magharibi, viongozi hao kwanza walihudhuria ibada kwenye Kanisa la PAG Kivumbini ambapo walisema kuwa kundi hilo linalenga kukomboa Kenya kutoka kwa utawala mbaya ambao umewasababishia maisha magumu.
“Tunapitia changamoto tele ikiwemo gharama ya juu ya maisha, ukosefu wa ajira na tunawaomba Wakenya watuzidishie dua ili tukomboe taifa hili,” akasema Bw Owino.