TAHARIRI: Kionjo cha maandamano kinafungua dirisha kwa Serikali kusikiza raia
SERIKALI inastahili kusikiza kilio cha raia kuhusu masuala mbalimbali badala ya kusubiri waandae maandamano.
Jumanne, japo madogo, kulikuwa na maandamano ya kulalamikia bei ya juu ya mafuta nchini.
Maandamano ya jana japo hayakuwa makubwa ya kutikisa nchi ikilinganishwa na miaka ya nyuma hayafai kusababisha serikali ilegeze na kuona kama imepata ushindi.
Mwanzo, huenda wengi hawakujitokeza kwa sababu baada ya bei hizo kupanda maradufu, serikali kupitia Mamlaka ya Kudhibiti Kawi na Petroli (EPRA) iliangazia upya na kushusha bei hizo.
Itakumbukwa kuwa maafa ambayo yalishuhudiwa mnamo 2004 yalitokana na maandamano dhidi ya Mswada wa Fedha ambao ulisheheni ushuru mwingi na ulikuwa unawaumiza raia.
Kilichofanya watu wajitokeze barabarani ni walihisi mswada huo ungetekelezwa basi ungewaumiza kiuchumi.
Hii ndiyo maana serikali inastahili kumakinika sana kuwa raia nafuu kiuchumi badala ya kukumbatia sera ambazo zinawaumiza au kuwahangaisha raia.
Aidha maandamano haifai kuwa lugha ambayo inasukuma serikali kuwajibikia majukumu yake.
Kila mara ambapo taifa linashuhudia fujo, wawekezaji wanahamia nchi ambazo zina mazingira tulivu ya kufanya biashara.
Kwa upande mwingine, kuna wale ambao wangependa kufika nchini na kuwekeza lakini hawawezi kufanya hivyo, iwapo kuna ghasia zinazoendelea.
Mfano, ni jinsi ambavyo Amerika ilitoa tahadhari kwa raia wake nchini kuzuia maeneo yenye watu wengi.
Amerika mara nyingi ikitoa onyo na kwa kuzingatia hadhi yake, mataifa mengine huwa yanafuata mkondo.
Kwenye maandamano ya jana, ni wazi kuwa serikali bado haijajifunza kutokana na kuwatumia maafisa wa usalama kuwakabili waandamanaji.
Hapo jana, polisi walimwagwa katika miji mbalimbali baadhi wakiwa wamevalia nguo za kiraia ili kupambana wale ambao wangejitokeza.
Maandamano ni haki ambayo ipo kwenye katiba na mradi yanafanyika kwa amani, jukumu la polisi ni kutoa ulinzi tu.
Mara nyingi maandamano yameishia mauti na uharibifu wa mali kwa sababu polisi huingilia kati na kuwapiga raia.
Viongozi wetu, asasi za kisheria wanastahili kufahamu kuwa maandamano hufanyika katika hata katika nchi ambazo zimeendelea na yamehusishwa sana na mageuzi ya kisiasa katika mataifa hayo.
Iwapo serikali ingekuwa ikiwajibika ipasavyo, basi hakungekuwa na haja ya maandamano na hata Rais William Ruto hangelalamika mitandao inatumika kusawiri nchi vibaya.