Watu 518 waliangamia katika ghasia Tanzania; idadi huenda ikawa juu – Tume
DAR ES SALAAM, Tanzania:
TUME iliyoundwa Tanzania kuchunguza sababu za ghasia za baada ya uchaguzi zilizosababisha vifo imesema watu 518 walipoteza maisha yao kutokana na machafuko hayo mwaka jana.
Kwenye ripoti yake, tume hiyo Alhamisi ilisema kuwa machafuko hayo yalipangwa na wanasiasa pamoja na wanaharakati waliowalipa waandamanaji ili kuzua vurugu.
Idadi hiyo ni ndogo kuliko ile iliyotolewa awali na wanaharakati wakati wa ghasia hizo zilizoanza mnamo Oktoba 29 mwaka jana.
Tume hiyo ya Uchunguzi iliyoongozwa na Jaji Mkuu Mstaafu Mohamed Chande Othman kwenye ripoti hiyo ilisema idadi hiyo ya vifo ilithibitishwa kuwa ndogo.
Hata hivyo, ilifafanua kuwa huenda ikaongezeka iwapo serikali itathibitisha kuwa baadhi ya familia zilizika miili bila kutoa taarifa kwa serikali.
Ripoti hiyo iliwasilishwa kwa Rais Samia Suluhu Hassan, ambapo ilibainika waliopoteza maisha wengi wao (490) walikuwa wanaume, 28 wanawake, na watoto walikuwa 21 kati ya jumla hiyo.
“Vifo vingi vilikuwa si vya kawaida,” alisema, akiongeza kuwa watu 121 walifariki hospitalini walipokuwa wakipatiwa matibabu kutokana na majeraha.
Hata hivyo, tume ilieleza kuwa maandamano hayo yalikuwa kinyume cha sheria na yalipangwa kuvuruga amani baada ya dhana kuwa kura ziliibwa na upinzani ulikuwa ukikandamizwa nchini humo.
“Yaliyotokea Oktoba 29 hayakuwa maandamano ya amani bali yalikuwa vitendo vya vurugu,” akaongeza.
Aidha, alisema hakukuwa na taarifa iliyotolewa kwa polisi ambapo kawaida hutakiwa kupokea notisi ya saa 48 kabla ya maandamano kufanyika.
“Vurugu zilipangwa na kutekelezwa katika siku iliyotangazwa kisheria kuwa siku ya uchaguzi mkuu jambo ambalo lilinyima wananchi wengine haki zao za kisheria, ikiwemo haki ya kushiriki uchaguzi.”
Ripoti hiyo imetokana na mahojiano na waathiriwa wa ghasia, vyombo vya usalama, madaktari pamoja na kupitia maelezo kutoka kwa washikadau wengine.