Mpango wa elimu bila malipo unazongwa na shida tele, hakuna pesa – Katibu Bitok
KATIBU wa Elimu ya Msingi, Julius Bitok, amewaambia wabunge kwamba sera ya serikali ya kugharimia elimu katika shule za umma haifanyi kazi kama ilivyokusudiwa, akitoa ishara kuwa wazazi wanapaswa kujiandaa kwa ada na michango “isiyo rasmi” shule zitakapofunguliwa wiki ijayo kwa muhula wa pili.
Bitok alieleza Kamati ya Bunge ya Hesabu za Umma (PAC) kuwa changamoto kubwa ni upungufu wa fedha, ambapo serikali inakosa takribani Sh7,000 kwa kila mwanafunzi.
Alisema hali hiyo imeathiri utekelezaji wa sera ya elimu bila malipo.
“Ni kweli inafanya kazi, lakini si kikamilifu kutokana na changamoto za ufadhili,” alisema Bitok.
Alifafanua kuwa serikali itatoa Sh23.4 bilioni kwa shule za umma kabla ya muhula wa pili kuanza, lakini akakiri kuwa kiasi hicho bado hakitoshi kukidhi mahitaji ya shule.
Chini ya mfumo huo, serikali hufadhili shule kulingana na idadi ya wanafunzi.
Viwango vya sasa ni: Sh22,244 kwa sekondari, Sh15,043 kwa shule za sekondari msingi, Sh1,420 kwa shule za msingi, na Sh57,974 kwa elimu ya mahitaji maalum.
Hata hivyo, Bitok alisema wanafunzi wa sekondari hupokea kwa uhalisia Sh15,244 pekee, hivyo kusababisha pengo kubwa la fedha.
Wabunge katika kamati hiyo akiwemo Marianne Kitany, Wilberforce Oundo, Joseph Namuar na Mary Emase, walikosoa serikali wakisema wazazi wamebeba mzigo mkubwa kutokana na upungufu huo.
Bi Kitany alisema walimu wakuu hupanga bajeti kwa kutumia takwimu rasmi lakini fedha halisi huwa zimepungua, hali inayosababisha madeni kuongezeka shuleni.
Bw Oundo alihimiza serikali kueleza ukweli kama elimu ya msingi bado ni bure au la, akisema wazazi wanapaswa kuambiwa mapema ili kupanga maisha yao.
Kwa upande wake, Emase alisema mfumo wa sasa unatoa taswira isiyo ya kweli kuhusu elimu bila malipo nchini.
Wabunge hao pia walionya kuwa ukosefu wa uwazi katika ufadhili wa elimu unazidisha mzigo kwa familia na kudhoofisha uaminifu kwa sera ya elimu ya bure.
Ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Nancy Gathungu ilionyesha kuwa mabilioni ya shilingi yalipotea kupitia wanafunzi hewa na shule hewa katika miaka minne iliyopita, huku shule zikiendelea kukosa fedha.
Mkurugenzi wa ukaguzi Justus Okumu alisema tatizo kuu ni ukosefu wa fedha, huku akibainisha kuwa baadhi ya shule hazipo lakini zinaonekana kwenye mfumo wa serikali.