Jamvi La Siasa

Orengo asisitiza ODM imetolewa pumzi

Na BENSON MATHEKA April 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Gavana wa Siaya James Orengo ameikosoa vikali mipango inayoendelea ya kuhifadhi ngome za kisiasa ndani ya Orange Democratic Movement (ODM), akisema ni ishara tosha kuwa chama hicho kimepoteza nguvu zake za awali.

Akizungumza katika mahojiano kwenye Herman Manyora TV, Orengo alisema hapo awali ODM ilipokuwa imara, vyama vingine ndivyo vilivyokuwa vikilalamikia mfumo huo na hata kuomba nafasi ya kushindana kwa haki. Hata hivyo, alieleza kuwa hali hiyo imebadilika kabisa kwa sasa.

“Takwa hili linaonyesha kwamba ODM imelegea na imepoteza makali yake,” alisema Orengo.

Alionyesha masikitiko kuhusu hali ya sasa ya ODM, akitaja kushuka kwa umaarufu wake katika maeneo yaliyokuwa ngome zake.

Gavana huyo alirejelea chaguzi ndogo za hivi majuzi katika wadi ya Kisii Mashariki na Narok Mjini, ambapo Democracy for the Citizens Party ilishinda viti ambavyo, kulingana naye, ODM ingeweza kushinda kwa urahisi hapo awali.

Kuhusu mustakabali wa chama hicho, Orengo alisema licha ya hali kuonekana ngumu, bado kuna nafasi ya kurekebisha mambo ikiwa hatua sahihi zitachukuliwa.

Pia, alishutumu Kaunti ya Kakamega, iliyokuwa ngome kuu ya ODM na wabunge 12, akisema inasikitisha kuona wengi wao wakihama na kujiunga na United Democratic Alliance (UDA).

Matamshi ya Orengo yanajiri siku chache baada ya Pauline Odhiambo Oginga, dadake wa kambo wa marehemu Raila Odinga, kuonyesha wasiwasi wake kuhusu hali ya ODM.

Akizungumza pia kwenye kipindi cha Herman Manyora Podcast, Pauline alisema kuwa Rais William Ruto sasa anaweza kuingia na kufanya siasa katika eneo la Nyanza bila msaada wa viongozi wa ODM.

Alilaumu viongozi wa chama hicho kwa kumruhusu Rais kupenya katika ngome zao za kisiasa bila wao kutambua mapema, hadi alipofanikiwa kujijengea ushawishi mkubwa.

“Ni jambo la kusikitisha kwamba Ruto anaweza kufika mashinani Nyanza bila viongozi wa ODM. Hata wananchi wa kawaida wanasema wanataka maendeleo kutoka kwa serikali hii, iwe kwa msaada wa viongozi wa ODM au la,” alisema Pauline.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna naye ameonyesha kutoridhishwa na hali ya chama. Alisema maeneo kama Homa Bay yalikuwa ngome imara ya ODM kiasi kwamba hakukuwa na haja ya mazungumzo ya  kutetea ngome.

Hata hivyo, alikiri kuwa mambo yamebadilika na chama sasa kinalazimika kujadiliana na vyama vingine kuhusu kugawana maeneo ya kisiasa, jambo ambalo halikuwahi kutokea hapo awali.

“Kwa mara ya kwanza ninasikia vilio katika Homa Bay. Tulipokuwa na nguvu, hatukujali nani anagombea dhidi yetu,” alisema Sifuna.

Kauli hizi zinaashiria changamoto kubwa zinazokumba ODM, huku wachambuzi wakisema kuwa chama hicho kinakabiliwa na mtihani mgumu wa kurejesha umaarufu wake katika ngome zake za jadi kuelekea uchaguzi wa 2027.