Wanga, Mbarire wavikwa unahodha wa ndoa kati ya UDA na ODM
UAMUZI wa Rais William Ruto na Seneta Oburu Oginga wa Siaya kuteua Gavana wa Homa Bay, Gladys Wanga, na mwenzake wa Embu, Cecily Mbarire, kuongoza mazungumzo kati ya Orange Democratic Movement (ODM) na United Democratic Alliance (UDA) si wa bahati nasibu.
Ni hatua iliyopimwa kisiasa, kimkakati na hata kisaikolojia ikilenga kujenga daraja kati ya pande mbili zenye historia ya ushindani mkali.
Taarifa iliyotiwa saini ya Rais Ruto na Dkt Oburu baada ya mkutano wa maafisa wa ngazi za juu wa vyama vyao mnamo Alhamisi, ilisema kuwa vimeanza rasmi hatua za kuimarisha ushirikiano wao wa kisiasa.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo mkutano ulilenga kuimarisha ushirikiano na kubaini maeneo yenye maslahi ya pamoja kati ya vyama hivyo vikuu nchini.
Moja ya maazimio kuu yaliyoafikiwa ni kuwataka wenyeviti wa ODM na UDA kuendeleza mashauriano ya mara kwa mara na yenye kuzingatia mifumo ya vyama.
Lengo la mazungumzo hayo ni kujenga mwafaka kuhusu masuala ya kipaumbele na kuweka msingi wa kuunda kile kilichoelezwa kama “muungano wa usawa” kati ya ODM na UDA.
“Tunaendelea na mashauriano ya kimfumo ili kujenga mwafaka juu ya masuala muhimu na kuweka msingi wa muungano rasmi wa usawa kati ya vyama hivi viwili,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
Uamuzi huo unaonyesha mkakati mpana wa kisiasa unaolenga kujenga uaminifu, usawa na uthabiti katika ushirikiano wao unaochipuka.
Wachanganuzi wa siasa wanasema, kwanza, wawili hawa ni viongozi wa juu kabisa ndani ya vyama vyao, wakiwa wenyeviti wa kitaifa. Hii ina maana kuwa mazungumzo wanayoongoza yana uzito wa moja kwa moja wa kisera na kisiasa.
“Kwa lugha rahisi, chochote watakachokubaliana kina nafasi kubwa ya kupitishwa bila pingamizi kubwa ndani ya vyama. Hii inapunguza hatari ya mazungumzo kukwama au kupuuzwa na wanachama,” asema mchambuzi wa siasa Dkt Isaac Gichuki.
Anasema hatua hiyo ni njia ya kujenga imani. “Unapoweka wenyeviti wa vyama mezani, unahakikisha hakuna upande unaohisi kudharauliwa. Hii inajenga uhalali wa mazungumzo na kuondoa wasiwasi wa hujuma za kisiasa,” anasema.
Kwa mujibu wa mchambuzi huyu, hili ni chaguo la kimkakati. “Wanga na Mbarire wana uwezo wa kujenga daraja kati ya pande mbili jambo linalowafanya kufaa kusimamia mazungumzo nyeti kama haya,” anasema.
Anasema kuwa mbali na kuwa wenyeviti wa vyama hivyo vikuu nchini, wako karibu na viongozi wa vyama vyao, wanaelewa safari ya ndoa ya ODM na UDA ilivyoanza na wana uzoefu mkubwa wa kisiasa.
“Wanga alikuwa karibu na mwanzilishi wa ODM Raila Odinga katika suala la kuunda Serikali Jumuishi na amekuwa akiitetea chini ya kiongozi wa sasa Oburu Oginga huku Mbarire akiwa mmoja wa waanzilishi wa UDA chini ya Ruto,” asema.
Kulingana na mchanganuzi wa siasa Alfa Oloo, uzoefu huu unawapa uwezo wa kusimamia mazungumzo magumu, kushughulikia tofauti za maslahi na kufikia mwafaka unaokubalika.
“Usisahau kuwa Wanga ni mtetezi wa Ruto eneo la Nyanza na pia amekuwa akimuunga Oburu wakati tofauti zinapozuka hata ndani ya ODM,” asema Oloo.
Aidha, uteuzi wao unapunguza presha ya moja kwa moja kwa Ruto na Oburu. Badala ya wao kuonekana kama wanaosukuma ajenda binafsi, wanaruhusu mazungumzo yaendeshwe na wawakilishi wanaoaminika. Hii huongeza nafasi ya mazungumzo kufanyika kwa utulivu bila mvutano wa moja kwa moja wa kisiasa.
Hata hivyo, Oloo anasema uamuzi wa mwisho kuhusu masuala tata katika mazungumzo hayo utafanywa na Ruto na Oburu.
“Kinachofanyika kinalenga kuzima malalamishi wakati ambao kila chama kina misimamo yake ambayo sio rahisi kubadilika, “ aongeza Gichuki.
Uteuzi wa Wanga na Mbarire, aeleza, unaashiria hatua ya kimkakati kuelekea kuunda “muungano wa usawa” kati ya ODM na UDA.
Ni jaribio la kuonyesha vyama vinazima siasa za makabiliano na kuelekea siasa za maelewano. Hata hivyo, mafanikio ya mkakati huu yatategemea uwezo wa viongozi hawa kusimamia matarajio ya vyama vyao na kushinda shinikizo a kisiasa kutoka kwa wafuasi wenye mitazamo tofauti.