KINAYA: Kizazi Kizee ndicho kinazuia mabadiliko ya kisiasa nchini
“HIVI umelewa?” Swali hilo hujibiwa kwa jingine pale Mlimani: “Kuna pombe yako ambayo imeibwa?”
Ni mojawapo ya njia nyingi za kumwambia mtu akukome, hasa ukihisi kwamba anajiingiza katika mambo yasiyomhusu ndewe wala sikio.
Ni sawa na kisa nilichokuandikia hapa mara kadha, ambapo kijana anakunywa dawa ya panya, mhisani anakimbia kituo cha polisi kuomba asaidiwe kumnusuru, maafisa nao wanauliza mlalamishi ni nani!
Polisi: “Kesi hii inakuhusuje? Wewe ni paka?”
Mhisani: “Hapana, naomba tu mtusaidie.”
Polisi: “Mlalamishi ni nani? Sisi hatushughulikii kesi ambayo haina mlalamishi.”
Mhisani: “Kwa hivyo nifanye nini?”
Polisi: “Mwambie panya aje aripoti, na siku nyingine ujaribu sana kutoingilia mambo yasiyokuhusu.”
Hizo ndizo hisia ambazo nilipata hivi majuzi maandamano ya kupinga ongezeko la bei za mafuta nchini yalipovutia watu wachache mno.
Nilijua pangekuwa na tatizo yalipotangazwa kuwa maandamano ya kizazi kipya cha Gen–Z; mara nyingi wazee hutafuta visingizio vya kutoshiriki shughuli zozote za kuikomboa nchi.
Ni kwa sababu ya kizazi kizee ambapo nchi hii haiendi mbali, na mapinduzi ya kisiasa hayawezekani.
Kisa na maana? Kizazi kizee huhisi kana kwamba ndicho kinashikilia nchi nzima isianguke.
Kwa hivyo? Kikiona chochote ambacho kinatishia kuvuruga mtindo wa kawaida wa kufanya mambo, kinarudi nyuma hatua moja na hatimaye kususia kabisa.
Kwa nini? Wazee hawataki chochote kitakachowazuia kwenda kazini, kitakachotatiza familia zao kwa vyovyote vile.
Ndio maana juzi waliegesha magari nyumbani na kutumia matatu ili wasijipate pabaya wakati wa maandamano hayo.
Haikosi walijiuliza kwa nini Gen-Z waliandamana ilhali wengi wao hawana magari, na hata labda wanaishi kwa wazazi.
Labda wazee waliuliza bei za mafuta zinawahusu vipi Gen-Z. Kwani kuna mafuta yao ambayo yameibwa?
Katika kadhia nzima ya wazee kutoelewa mambo, au kuwa na mitizamo ya kishamba, unapata kuwa mara zote wao huwa wamenoa sana, yaani misimamo ya vijana ndiyo huwa sahihi.
Mzee anapouliza vijana bei za bidhaa zinawahusuje, ina maana kwamba hataki kizazi hicho changa kidhibiti mambo yanayohusu maisha yao ya usoni, yaani wasihusike kabisa kujiandalia mustakabali wao.
Wazee, ambao wanajiona kafika kwa sababu wana kazi nzuri na vigari vya mikopo, ndio huzuia mabadiliko katika nchi.
Wana mazoea ya kulalamika kuwa maandamano ‘yaishe haraka turudi kazini; watoto warudi shuleni; maduka yafunguliwe’ na kadhalika.
Ikiwa wewe ni mzee, kabla hujapanua kinywa kuwakosoa Gen-Z kumbuka wewe ni mmoja wa matatizo makubwa ya nchi hii.
Imebaki nyuma kwa sababu ya uzembe wako, kutojiamini na kujali sana matokeo ya mambo ambayo huna uwezo wa kudhibiti.
- Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)