Kindiki apiga kambi Mlimani siasa za Mt Kenya East na West zikichacha
NAIBU wa Rais Prof Kithure Kindiki amekita kambi eneo la Mlima Kenya baada kubainika kuwa ndani ya siku 58 pekee amefanya mikutano 15.
Kuanzia Machi 1, 2026 hadi Aprili 27, 2026, Prof Kindiki alikuwa ameandaa mikutano 15 katika ukanda wa Mlima Kenya Mashariki huku akilenga kumzidia umaarufu aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua.
Kwa mujibu wa Waziri wa Utumishi wa Umma, Geoffrey Ruku, lazima Mlima Kenya Mashariki uamue mustakabali wake wa kisiasa kuelekea 2027.
“Kwa miaka mingi tumekuwa tukiwafuata wenzetu wa Mlima Kenya Magharibi, huwa tunawinda pamoja lakini wao ndio wanakula. Si lazima kuwa Mlima Kenya usalie kuungana,” akasema Bw Ruku.
“Iwapo Bw Gachagua ataendelea kuwepo, tutagawa Mlima Kenya na sisi tunaotoka Mashariki hatutaendelea kumtii,” akaongeza katika mahojiano na TV inayotangaza kwa lugha ya mama.
Waziri huyo alifichua kuwa wanalenga kubuni ‘mlima’ mdogo ambao utakuwa na kura milioni 1.5 na kigogo wao atakuwa Prof Kindiki.
Mlima huo mdogo utajumuisha kaunti za Meru, Tharaka-Nithi, Embu na sehemu za Kaunti ya Kirinyaga.
Ingawa Prof Kindiki amekuwa akitaka Mlima wote uungane nyuma ya Rais Ruto, amekuwa akiendeleza mikutano mingi Mlima Kenya Mashariki akilenga kuwa kigogo wa siasa za eneo hilo.
Hata hivyo, Mbunge wa Manyatta Mukunji Gitonga anasema asilimia 80 ya wakazi wa Mlima Kenya Mashariki hawataingia kwenye mtego wa kutenga eneo hilo na Mlima Kenya Magharibi.
Mnamo Jumapili, Prof Kindiki alikuwa mwenyeji wa Rais Ruto katika Kaunti ya Tharaka-Nithi ambapo wawili hao walihutubia mkutano wa kisiasa mjini Chuka.
“Naibu wangu ni mwanasiasa mwerevu, anajituma na ni rahisi kufanya kazi naye,” akasema Rais Ruto akiashiria kuwa huenda akamuunga mkono Prof Kindiki kwa urais katika uchaguzi wa 2032.
Huku Profesa Kindiki akilenga uungwaji mkono ambao utamzolea Rais William Ruto kura nyingi hasa akilenga kuwa mgombeaji mwenza wake, Bw Gachagua analenga kutumia ushawishi wake kumnyima rais kura za eneo hilo.
Kwa mujibu wa Mchanganuzi wa Masuala ya Kisiasa Malila Munywoki, Profesa Kindiki anastahili kumakinikia kuunganisha Mlima Kenya badala ya kuonekana anasaka kura za Mlima Kenya Magharibi pekee.
“Kura za Mlima Kenya Magharibi zitagawanyika na hawezi kuzipata zote milioni 1.5. Anaweza kushinda Tharakaa-Nithi lakini itakuwa ngumu kwake Embu, Meru na Kirinyaga na akifanya hesabu yake vizuri anaweza kusalia na kura 500,000 pekee,” akasema Bw Munywoki akisisitiza kura hazitoshi kumruhusu kuwa mgombeaji mwenza wa Rais Ruto.
Msomi huyo anamshauri Profesa Kindiki aondoe uoga na akabiliane na Bw Gachagua uso kwa macho ili aongeze umaarufu.
“Tunataka kumwona kwenye kaunti za Mlima Kenya Magharibi kama Murangá, Kiambu, Kirinyaga na Nyeri. Tunataka kuona akitembelea ngome za Bw Gachagua na kufanya mikutano ya kisiasa badala ya kujificha tu maeneo anakoonekana ana uungwaji mkon,” akaongeza.