MAONI: Tuulize wanasiasa watakachotufanyia sababu wanapangia kura zetu kama mahamri
SHUGHULI ya kusajili wapigakura imekamilika hivi majuzi, na idadi ya waliosajiliwa haikai vibaya. Inatamanisha. Inatia moyo. Inaridhisha. Ni mwanga wa matumaini.
Ingawa mwanzoni ilionekana kana kwamba Wakenya wengi wametamaushwa na wanasiasa kiasi cha kutotaka kushiriki shughuli nzima ya uchaguzi, idadi ya waliosajiliwa juzi inaleta taswira tofauti.
Wakenya bado wanataka kushiriki maamuzi ya ni akina nani ambao watawatawala, yaani watu watakaoamua ushuru mkubwa wanaolipa utatumiwa kwa namna gani.
Wananchi wa kawaida tumeshamaliza kazi ya kujisajili, sasa imeingia hatua nyingine ambapo wajanja wanaoitwa wanasiasa wanaketi na kuanza kupanga jinsi watakavyogawana kura zetu. Hakika, wanapanga jinsi watakavyotugawana kama peremende au mahamri.
Wanavyojadili mbinu za kutupanga ili tuwapigie kura, wawashinde wapinzani wao, utadhani sisi ni bidhaa tu, hatuna usemi kuhusu tunakopelekwa, jinsi ya kupelekwa huko, wala hawajali matokeo ya kutuvutania kama fisi wanavyong’ang’ania mnofu wa nyama yatakuwa yepi.
Kitu kinachowazuga akili wanasiasa wa serikali na upinzani ni jinsi watakavyowashawishi maelfu ya wawaniaji wa vyama mbalimbali wanaotaka kujitoma kwenye kinyang’anyiro kwa tiketi za vyama vyao.
Hali inakuwa mbaya zaidi ukizingatia kwamba ipo miungano ya kisiasa iliyoundwa na vyama mbalimbali, ambavyo vinanuia kuwa na wawaniaji katika kila kinyang’anyiro. Hilo linatishia kusambaratisha miungano hiyo.
Hofu ya wanasiasa wanaoongoza miungano yenyewe ni kwamba, iwapo vyama vyote vitawapa wawaniaji tiketi, basi watagawanya kura na kuupa ushindi muungano pinzani.
Hali ni ya mchanganyiko maalum wa maslahi ya kisiasa kote-kote kwa kuwa, mathalan, mungano wa Kenya Kwanza unataka teuzi za wawaniaji ziwe huru, yaani kila chama kiwe na mwaniaji kokote kinachodhani kina umaarufu.
Mtizamo huo unapingwa vikali na chama cha Orange Democratic Movement (ODM) ambacho ni rafiki mkuu, kipenzi hasa, cha Rais William Ruto, kigogo wa Kenya Kwanza.
ODM inahofia kuwa Kenya Kwanza ikiruhusiwa kuwa na wagombea katika maeneo ya Luo Nyanza ambako ODM ni maarufu, basi Kenya Kwanza itaimeza, isahaulike kabisa. ODM inasisitiza iachiwe maeneo iliko maarufu ili itambe pekee bila ushindani, naye Bw Ruto anayamezea mate maeneo hayo.
Tukigeukia muungano wa upinzani unaojiita serikali mbadala, vigogo wake kama Bw Kalonzo Musyoka wa chama cha Wiper Patriotic Front (WPF) na Bw Rigathi Gachagua wa Democracy for the Citizens Party (DCP) wanataka vyama tanzu viruhusiwe tu kuteua wawaniaji katika maeneo ambako vina umaarufu zaidi.
Pendekezo hilo linapingwa na Dkt Fred Matiang’i wa Jubilee, akishirikiana na Bi Martha Karua wa People’s Liberation Party (PLP). Wawili hao wanasisitiza kuwa kila chama kiwe huru kuteua wawaniaji kokote kinakotaka. Migawanyiko hiyo inatishia kupasua chungu kizima kiwe vigae.
Ona, wanasiasa hao wote, wa serikali na wa upinzani, hawajadili chochote kuhusu manufaa ambayo mwananchi atapata kwa kuwachagua. Wanatuchukulia kama mitambo ya kupiga kura tu, kuwapa vyeo ili waendeleze njama zao za tangu jadi za kutenga na kutawala.
Je, kwani sisi hatuna usemi wala maoni kuhusu jinsi tunavyotaka kuongozwa? Hivi kazi yetu ni kutunga foleni, kuwapigia kura na kujiendea nyumbani bila kujua tunachotarajia?
Nafasi ya mpigakura, na hapa narejelea mamilioni ya walio kwenye sajili ya sasa, ni gani katika ugawanaji unaoendelea? Ama unataka kuniambia sisi ni watumwa tu, tunasubiri kuuzwa na kununuliwa kama mifugo sokoni? Mnada huu utaendelea hadi lini?
Ni jukumu letu kuanza kuwauliza wanasiasa maswali magumu, hasa ambao tunakaribia kushawishika kuwapa kura zetu, kwa sababu tusipofanya hivyo watatutenda mara tu baada ya uchaguzi.
Ukikutana na mwanasiasa, hasa hao wanaoongoza miungano, muulize mrengo wake unakuahidi kitu gani ambacho hujawahi kuahiudiwa, unanuia vipi kutimiza ahadi za uongo ambazo zimetolewa miaka mingi iliyopita na mirengo ambako amewahi kuwa mwanachama.
Ni katika kuuliza maswali magumu na ya kuudhi ambapo wanasiasa watajua kuwa hakuna kura zao ambazo tumewawekea mahali tukisubiri kuwapa, sharti wazifanyie kazi. Kura zetu si karanga au mishikaki waitafune watakavyo. Mara hii ni ahadi na kazi!
– Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)