Jamvi La Siasa

KINAYA: Nimeona watu wakitishia kutimua wengine eneo lao kana kwamba wakifa wataondoka na ardhi

Na DOUGLAS MUTUA April 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UNASAIDIA Kenya na nini au ni kidomodomo tu? Unamiliki sehemu gani ya Kenya unayoweza kubeba ukaenda nayo kokote unakotaka?

Uliumba mita ngapi za nchi hii tunayoipenda sote? Ukiaga dunia utaondoka na ekari ngapi?

Nimewaona watu kadha mtandaoni na hata kwenye vyombo vya habari wakitishia kuwatimua wengine kutoka maeneo wanayochukulia kuwa ya jamii zao, eti hawaruhusiwi kuishi kokote wanakotaka.

Fikra za kipuuzi kama hizo zilimsababisha marehemu Lucy Kibaki kuuliza: “Mama yako ni nani?” Kimsingi, ni nani aliyekufunza upuuzi huu? Mbona unaonekana kutumia ubongo kama kofia?

Watu wamewahi kufukuzwa kaskazini mwa nchi. Wengine Nyanza, Rift Valley, Pwani, Mlimani na kadhalika. Mwaka 2007.

Nilikuwa mumu humu nikikuandikia makala hizi-hizi, hivyo unafaa kumakinika kuhusu mambo ninayokwambia. Sijigambi lakini.

Nchi hii si ya mama wa mtu, ni yetu sote. Tunaishi, kufanya kazi, kuanzisha biashara na kuwania nyadhifa zozote tunakotaka, na wapuuzi wachache wanaodhani wanamiliki Kenya hawawezi kutufanyia chochote.

Ukisikia hutaki kuishi na Wakenya wenzako, basi hamia kwingine utuachie nchi yetu. Hiyo unayoita ardhi yako au ya jamii yako itamilikiwa na mtu mwingine miaka 100 ijayo. Utasahaulika.

Labda hata kaburi lako litafanywa tambare, hapo papandwe mihogo au mahindi, watu wakinge njaa kwa mbolea ya mifupa yako.

Ikiwa unaweza kwenda mbinguni au jehanamu na ardhi, basi wabague watu na kuwafukuza unakoita kwenu.

Wazuie na wanasiasa kufanya kampeni huko. Jehanamu inakuita. Nenda huko kwa wepesi wa kumeza maji.

Katika enzi hii ya ugatuzi, kila sehemu ya nchi inapaswa kukua kwa kasi ili tutangamane na kukuzana kimawazo. Hakuna aliye na akili timamu anayepaswa kutishia mwingine eti atamfukuza kokote.

Sitaki kutukana mtu, niseme eti kaskazini mwa Kenya ni jangwa, hakuna anayetaka chochote kutoka huko. Siwezi kufanya hivyo, ni makosa. Daima nikiwa na kuepuka makosa. Yanaudhi. Huko ni Kenya pia.

Ajabu ya mazuzu wabaguzi kuishi Nairobi kwa watu, ila wanatishia kuwafukuza Wakenya wenzao kutoka kokote nchini. Waambie mgeni akija, mwenyeji hupona.

Turuhusu tuje kwenu tukujengee shule ambazo umeshindwa kujenga, ukahamia Nairobi na kuwatelekeza jamaa zako jangwani.

Tukifika tutakujengea na choo cha kisasa ili uache kuchimba dawa porini kama hayawani.

Tutakuongezea na shashi, uache kutumia majani na udongo kujisafisha ukishamwona mjomba. Ondokana na mawazo ya porini.

Tutakuchimbia na maji, tukujengee shule, vituo vya afya na huduma nyinginezo, kisha tukuachie vvyote hivyo tukirejea tulikozaliwa, ubaki navyo ili angaa utoke porini.

Muhimu zaidi, kumbuka Kenya si ya mama yako, ni ya kila Mkenya.

– Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)