Habari za Kitaifa

Kinachofanya Mwanasheria Mkuu kupinga mswada kuhusu uraia

Na SAMUEL OWINO May 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

OFISI ya Mwanasheria Mkuu imeibua wasiwasi kuhusu Mswada unaopendekeza kuwapa uraia watu wasio na utaifa ambao wameishi nchini kwa kipindi cha miaka saba.

Kupitia Wakili Mkuu wa serikali Shadrack Mose, ofisi hiyo iliambia Kamati ya Bunge la Kitaifa kuhusu Usalama wa Taifa na Utawala kwamba hatua hiyo inaweza kutumiwa vibaya na watu wasiokuwa na nia ya kuishi nchini kwa muda mrefu.

Katika mawasilisho yake mbele ya kamati hiyo, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu ilionya kuwa kutoa haki hiyo kunaweza kuruhusu baadhi ya watu kupata stakabadhi za uraia kwa malengo yasiyojulikana.

“Kwa mtazamo wetu, kuondolewa kwa kifungu kidogo cha (1)(c) kunaweza kuchochea matumizi mabaya ya hadhi hiyo, na taratibu za usajili zinaweza kutumiwa na watu wasiokusudia kuwa sehemu ya jamii kupata stakabadhi kwa madhumuni mengine,” ilisema ofisi hiyo.

Mwanasheria Mkuu alisisitiza kuwa ni muhimu kwa mwombaji kuthibitisha nia ya kuendelea kuishi nchini au kudumisha uhusiano wa karibu na wa kudumu na Kenya kabla ya kusajiliwa kama raia.

Kwa sasa, kamati hiyo inaendesha ushiriki wa umma kuhusu Mswada wa Marekebisho ya Sheria ya Uraia na Uhamiaji wa Kenya, 2025, unaolenga kuondoa muda kwa maombi ya uraia kwa watu wasio na utaifa.

Mtu asiye na utaifa ni yule ambaye hatambuliwi kama raia wa nchi yoyote kwa mujibu wa sheria zake.

Mswada huo, uliowasilishwa na Mbunge wa Kilifi Kaskazini Owen Baya, unapendekeza kuruhusu watu hao kupata uraia baada ya kuishi nchini kwa angalau miaka saba.

Hata hivyo, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu imeonya kuwa kifungu kipya cha 15 kinachopendekezwa hakijaweka muda maalum wa usajili, jambo linaloweza kufanya mchakato huo kuwa wazi.

“Iwapo Mswada utapitishwa ulivyo, usajili wa watu wasio na utaifa na wahamiaji utakuwa wa kudumu bila kikomo. Hali hii inaweza kusababisha ongezeko la madai yasiyo halali ya kutokuwa na utaifa,” ilionya.

Ofisi hiyo pia ilisisitiza umuhimu wa kuweka masharti makali ili kuhakikisha ni wale tu wenye madai halali wanaonufaika.

Aidha, ilishauri kamati kusubiri mwongozo wa sera kutoka kwa Wizara ya Masuala ya Ndani na Utawala wa Kitaifa kabla ya kuendelea na mchakato huo.

Iwapo Mswada huo utapitishwa, watoto wanaozaliwa na wazazi wasio na utaifa pia watasajiliwa kama Wakenya.