Lugha, Fasihi na Elimu

Waunda sera waliofifisha fasihi katika shule zetu wajue wanabomoa jamii

Na VINCENT OBUYA May 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SOTE tujuavyo, fasihi ni kioo cha jamii—huakisi maisha yetu, maadili yetu, changamoto zetu, na matarajio yetu.

Ni kupitia fasihi ambapo jamii hujiona ilivyo, hujirekebisha, na kujielekeza kwenye mustakabali unaofaa.

Dhima ya fasihi si haba; huelimisha, huonya, huburudisha, huunganisha, na zaidi ya yote, hujenga fikra pevu kwa vizazi vyote.

Hivyo basi, ni jambo la kushangaza kuona kwamba, katika mfumo wa elimu, fasihi imegeuzwa kuwa somo la kuteua.

Je, serikali inatupeleka wapi? Kufuatia hatua hiyo, wanafunzi wanaochagua fasihi ni wachache, hali inayotia shaka kuhusu mustakabali wa utamaduni na utambulisho wetu wa kitaifa.

Bila fasihi, tunapoteza sauti ya jamii, kumbukumbu za historia, na dira ya maadili.

Kumbukeni kuwa mabadiliko mengi chanya katika nchi yetu yamechochewa na fasihi.

Waandishi wamekuwa manabii wa jamii—wameibua maovu, wakakosoa uongozi mbovu, na hata kutabiri masuala ibuka tunayoyaona leo.

Fasihi si anasa; ni nguzo muhimu ya maendeleo ya kiakili na kijamii.

Serikali, serikali, serikali—tafakarini upya! Tuthamini fasihi, tuipe nafasi yake stahiki katika mfumo mzima wa elimu.

Sera za elimu zinapaswa kuitambua fasihi si kama somo la pembeni bali kama mhimili mkuu wa kukuza lugha, utamaduni na fikra huru.

Uwekezaji katika vitabu vya kisasa, mafunzo ya walimu na utafiti wa kifasihi ni hatua muhimu zinazoweza kufufua hadhi ya fasihi nchini.

Vilevile, ni wajibu wa jamii nzima—wazazi, walimu na wanafunzi—kukuza utamaduni wa kusoma na kuthamini kazi za kifasihi.

Shule ziandae mijadala ya vitabu, mashindano ya uandishi na maonyesho ya tamthilia ili kuifanya fasihi kuwa hai na yenye mvuto kwa kizazi cha sasa.

Bila juhudi hizi, tutakuwa tunalea kizazi kisicho na mizizi ya kiutamaduni

MWALIMU OBUYA, hufunza katika shule moja mjini Migori