Tumia bakora kwa hao Gen Z, Rais Samia amshauri Ruto
KAULI ya Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kuwa watashirikiana na Rais William Ruto kuendelea kuwaadhibu vijana wa Gen Z wanaoandamana imezua mjadala iwapo tawala hizi mbili zinaheshimu haki za kibinadamu na demokrasia.
Bi Suluhu alikuwa mwenyeji wa Rais Ruto kuanza Jumatatu hadi Jumanne kilele cha ziara hiyo kikiwa ni Rais Ruto kuhutubia Bunge la Tanzania jana.
Rais Ruto ni rais wa pili Mkenya kuhutubia bunge hilo baada ya marehemu Rais Daniel Arap Moi kufanya hivyo Novemba 22 2002 akiwa na mwezi mmoja kabla ya kung’atuka madarakani.
Mnamo Oktoba 6 2015, Rais Jakayo Mrisho Kikwete naye alihutubia kikao jumuishi cha Bunge la Kitaifa na lile la Seneti.
Wakati huo kampeni zilikuwa zimechacha Tanzania kati ya John Magufuli na Kiongozi wa upinzani Edward Lowassa.
Kwenye kikao cha pamoja, Rais Samia jana alikemea wimbi la mageuzi ambalo limekuwa likiandama Afrika Mashariki, akiwarejelea Gen Z kama vijana wakosa adabu ambao wanastahili kuadhibiwa.
“Tulikuwa tukiongea jinsi ya kupambana na hawa watoto wetu watovu wa adabu sijui wanajiita aje? Eti wenyewe wanajifanya ni wa Afrika Mashariki na popote wanakwenda kupigania demokrasia, popote wafanye fujo huku, wachome huku wasumbue serikali zao,” akasema Rais Suluhu.
“Niliambia Ruto lazima tusimame kidete kuhusu hili kwa watovu wa adabu hawa. Tusiwachague Watanzania au Wakenya, wakija kwangu nachapa mikwaju, wakija kwako wachape mikwaju ili wakae sawa,” akaongeza.
Kauli hiyo ilifasiriwa kuwa Kenya na Tanzania sasa zinashirikiana kuwakandamiza vijana ambao wamekuwa wakilalamikia uongozi duni na kupinga baadhi ya sera za kiuchumi zinazokumbatiwa.
Kenya ilishuhudia mawimbi makali ya maandamano ya Gen Z mnamo Juni 2024 wakipinga Mswada wa Fedha wa wakati huo ambao ulikuwa na mapendekezo mengi ya kuongeza ushuru.
Bi Suluhu alisema vijana wanastahili kukumbushwa kuhusu heshima kwa uongozi kwa kuwa demokrasia wanayopigania ni tofauti na ile ambayo ipo kwenye mataifa ya Ulaya.
“Hapo tutapata Jumuiya ambayo ina heshima na watu walionyooka. Demokrasia isituchafulie mila zetu au desturi, demokrasia yetu haina fomula. Naambia mwenzangu tusimame kulinda hizi desturi zetu,” akaongeza.
Kauli yake iliwasha ghadhabu kwenye mitandao ya kijamii nchini hasa ikizingatiwa kuwa imesalia miezi 14 kabla ya Kenya kuelekea uchaguzi mkuu ujao.
Vijana wameapa kutumia wingi wao kuamua matokeo ya uchaguzi huo.
Tanzania iliandaa uchaguzi wake mnamo Oktoba mwaka jana lakini kulikuwa na maandamano makubwa siku ya uchaguzi na baada ya matokeo kutangazwa.
Rais Suluhu alitangazwa mshindi kwenye uchaguzi huo kwa asilimia 98 na Tume ya Uchaguzi Tanzania.
Hata hivyo, waangalizi wa kimataifa walitilia shaka matokeo hayo, na kusema uchaguzi huo ulikosa kufikia viwango vya kimataifa vya uwazi.
Waangalizi kutoka mashirika mbalimbali walitaja kuendelea kuzuiliwa kwa Kiongozi wa upinzani Tundu Lissu kama jambo ambalo lilimwondolea Bi Suluhu ushindani.
Aidha, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres alizua maswali kuhusu kupotea kwa watu kiholela, raia kunyakwa kiholela na kuzuiliwa na viongozi wa upinzani kuandamwa kwa kushukiwa kufadhili maandamano.
Wakenya hawakusazwa kwa kuwa Mkenya John Okoth Ogutu ni kati ya walioripotiwa kuaga dunia katika ghasia za siku ya uchaguzi na baada ya uchaguzi huo.