Kinyanjui ashangaza seneti akisema mama mboga na mahasla ndio walitaka viwanda katika kaunti
WAZIRI wa Biashara, Lee Kinyanjui, amefichua kuwa mpango wa serikali wa kujenga viwanda kwenye kaunti kwa thamani ya Sh23.5 bilioni ulianzishwa bila utafiti kufanywa.
Akizungumza mbele ya Seneti Jumatano, Bw Kinyanjui alisema mpango huo ulitokana na mazungumzo aliyokuwa nayo Rais William Ruto na makundi ya “mama mboga” na “mahasla” wakati wa kuandaa manifesto ya Kenya Kwanza kabla ya uchaguzi wa 2022.
Waziri huyo alisema maoni yaliyotolewa na wananchi wakati wa kampeni yalitosha kuchukuliwa kama ushirikishaji wa umma kuhusu miradi waliyoitaka.
“Wakati mwingine tunajificha nyuma ya maneno makubwa kama tafiti za ufaafu ilhali tayari tunajua wananchi wanahitaji nini,” alisema.
Alilinganisha hali hiyo na mpango wa elimu ya bure ulioanzishwa na Rais wa tatu wa Kenya Mwai Kibaki bila utafiti maalum lakini ukafaulu.
Kauli hiyo imeibua mjadala mkali huku maseneta wakionya kuwa baadhi ya maeneo hayo ya viwanda huenda yakageuka miradi hewa isiyo na manufaa kwa wananchi.
Seneta wa Kitui, Enock Wambua alisema ilikuwa kosa kuweka gharama sawa kwa kaunti zote 47 bila kuzingatia tofauti za maeneo.
Kila kaunti ilitakiwa kutoa Sh250 milioni huku serikali kuu ikitoa kiwango sawa, jumla ikiwa Sh500 milioni kwa kila mradi.
Hata hivyo, magavana wamekiri kuwa gharama imeongezeka katika baadhi ya maeneo.
Gavana wa Nyeri, Mutahi Kahiga alisema mradi katika kaunti yake sasa utagharimu Sh589 milioni badala ya Sh500 milioni zilizopangwa awali.
Seneta wa Busia, Okiya Omtatah alisema hakuna hata kaunti moja yenye utafiti wa kisayansi unaoonyesha miradi hiyo inawezekana au itakuwa na manufaa.
Aidha, baadhi ya wakandarasi wameacha kazi huku miradi ikikwama.
Kati ya miradi 17 iliyoanzishwa mwaka 2023, ni mitano pekee iliyo tayari kuzinduliwa, kulingana na Waziri Kinyanjui.
Ripoti ya Afisi ya Bajeti ya Bunge pia inaonyesha baadhi ya kaunti ziko chini ya asilimia 30 ya utekelezaji huku miradi ikikwama kabisa katika kaunti 13.
Licha ya changamoto hizo, serikali inasema mpango huo ulikusudiwa kuongeza thamani ya mazao, kupunguza hasara baada ya mavuno na kuzalisha nafasi za ajira kwa vijana.
na wafanyabiashara wadogo.