Maziwa ya ngamia: Hadithi ya ‘dhahabu nyeupe’ ya mama Zamzam
KAUNTI ya Laikipia ikiwa miongoni mwa maeneo ambayo athari za tabianchi zinaendelea kutatiza mifumo ya jadi ya ufugaji, mabadiliko makubwa yanaibuka kimya kimya yakiongozwa na ngamia na wanawake.
Kati ya wanaofanikisha mageuzi hayo ni kampuni ya White Gold Camel Milk Limited, biashara inayokua kwa kasi na kubadilisha maziwa ya ngamia kuwa chanzo cha mapato, lishe bora na uthabiti kwa jamii za wafugaji.
Kampuni hiyo ilianzishwa na Zamzam Haji, ambaye huchakata na kuuza bidhaa za maziwa ya ngamia kwa wateja mbalimbali wanaoongezeka kila siku. Kutoka familia za mijini zinazotafuta njia mbadala yenye afya ya maziwa ya kawaida hadi watu wenye matatizo ya lactose, kisukari na wazee, bidhaa za White Gold Camel Milk zimeanza kujitokeza kwenye soko lenye ushindani mkuu nchini, la maziwa.
Bidhaa zake ni pamoja na maziwa halisi ya ngamia, brandi ya vanilla na strawberry, pamoja na maziwa yaliyogandishwa yanayojulikana kama “susa” katika jamii za wafugaji – somali. Bidhaa hizo sasa zinapatikana katika baadhi ya maduka makubwa nchini huku kampuni hiyo pia ikitoa huduma kusambazia wateja bidhaa nyumbani.
“Ni kampuni inayonufaisha zaidi wanawake, hasa wanawake kutoka jamii za wafugaji ambao kwa muda mrefu hawakuwa na masoko rasmi ya kuuza maziwa yao,” Zamzam anasema.

Leo hii, wanawake wanawakilisha karibu asilimia 80 ya wasambazaji wa maziwa kwa kampuni hiyo. Wengi wao, Zamzam anasema maziwa ya ngamia si bidhaa tu ya matumizi nyumbani bali ni njia ya kujitegemea kifedha, kujiendeleza kimaisha na kupata heshima katika jamii.
Mama huyu anasema safari ya kuanzisha biashara hiyo ilianza mwaka 2017 baada ya kubaini pengo kubwa katika mnyororo wa thamani wa maziwa eneo la Laikipia.
“Wanawake wengi walikuwa na ngamia na walizalisha maziwa mengi, lakini hawakuwa na mnunuzi wa kutegemewa baada ya kampuni moja kufungwa,” anakumbuka.
Kwa kushirikiana na mumewe aliyekuwa akiishi nchini Amerika wakati huo, walianzisha kiwanda kidogo kwa kutumia akiba yao binafsi na fedha walizokopa kutoka kwa familia kwa sababu hawangeweza kupata mikopo rasmi kutoka kwa benki au mashirika ya kukopesha pesa.
Safari ilianza kwa kuchakata lita 50 pekee za maziwa kwa siku. Leo hii, karibu miaka 10 baadaye, kampuni hiyo huchakata hadi lita 300 kwa siku msimu wa mvua, ingawa kiwango hicho hupungua wakati wa ukame.
Zamzam, aliyelelewa katika jamii iliyotengwa ambapo wanawake walikuwa na nafasi finyu za maendeleo, anasema alitaka sana kujenga biashara inayoinua wanawake katika kila hatua ya uzalishaji.

Jitihada zake sasa zinaonekana wazi. Wanawake waliokuwa wakikosa soko la maziwa yao sasa wanapata kipato cha kudumu. Baadhi yao, Zamzam anaambia Akilimali kwamba wameweza hata kununua ardhi, jambo ambalo hapo awali lilikuwa ndoto kwa wanawake wengi.
Wakati huohuo, biashara hiyo imechangia mabadiliko katika ufugaji huku wafugaji wengi wakihamia ufugaji wa ngamia kutokana na ukame wa mara kwa mara. “Tofauti na ng’ombe, ngamia wanaweza kustahimili mazingira magumu na kuendelea kutoa maziwa hata wakati wa kiangazi,” anasema.
Licha ya mafanikio hayo, Zamzam anasema changamoto bado zipo, ikiwemo; ukosefu wa fedha kupanua biashara, kuelimisha wateja kuhusu maziwa ya ngamia, ushindani mkuu sokoni na ongezeko la wizi wa mifugo katika maeneo jirani kama vile Kaunti ya Isiolo.
Hata hivyo, Zamzam ana matumaini makubwa. Kampuni hiyo sasa inalenga masoko ya kimataifa hususan katika mataifa ya Uarabuni (Gulf).
Aidha, alikuwa miongoni mwa wafanyabiashara, kampuni na wajasiriamali walionufaika kupitia Farm’Innov acceleration programme, mpango uliozinduliwa mwaka 2024 kusaidia ubunifu na ushindani katika sekta ya kilimo na mifugo. Mpango huo wa mwaka mmoja ulifadhiliwa kupitia ushirikiano wa serikali ya Ufaransa na ile ya Kenya.
Kwa sasa, White Gold Camel Milk inamiliki ngamia 23 na inaendelea kufanya kazi na mtandao mkubwa wa wasambazaji wa maziwa – wengi wao wakiwa wanawake kutoka Laikipia na kaunti jirani.