TIFA: Kindiki pazuri kuwa mgombea mwenza 2027
HUKU mjadala ukiendelea kuhusu ni nani anafaa kuwa mgombea mwenza wa Rais William Ruto katika uchaguzi mkuu mnamo 2027, Naibu Rais Kithure Kindiki yupo pazuri kuwahi nafasi hiyo.
Kulingana na kura ya maoni iliyotolewa Alhamisi na Kampuni ya TIFA, Profesa Kindiki anaungwa mkono kwa asilimia 59, akimwacha mbali mpinzani wake wa karibu, Gavana wa Homa Bay, Gladys Wanga, ambaye ana asilimia 12 pekee.
Kiongozi wa ODM, Dkt Oburu Oginga, ana asilimia tatu tu, huku Gavana wa Mombasa, Hassan Joho, akipata asilimia moja pekee.
Licha ya uungaji mkono huo, Profesa Kindiki anakabiliwa na kazi ngumu ya kuhakikisha Rais Ruto anajizolea kura za eneo la Mlima Kenya.
Ingawa hivyo, anaonekana tayari amejizolea uungwaji mkono mkubwa kutoka eneo la Mlima Kenya Mashariki, ambalo lina zaidi ya kura milioni 1.3.
ODM imekuwa ikishikilia kuwa kwenye mazungumzo ya kushirikiana na Rais Ruto lazima wapewe nafasi ya kuwa mgombeaji mwenza wake.
Mnamo Februari 12, mwaka huu Dkt Oburu alibadili msimamo wake na kusema wazi kuwa ODM inamezea mate wadhifa wa Profesa Kindiki.