Habari

Katibu Sing’Oei sasa atetea utoaji paspoti kwa waasi wa Sudan

Na WINNIE ONYANDO May 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KATIBU wa Wizara ya Masuala ya Kigeni, Korir Sing’Oei ametetea hatua ya serikali kuwapa paspoti ya Kenya baadhi ya waasi nchini Sudan akisema ilifanya hivyo kwa misingi ya kibinadamu sio kuunga mkono waasi hao.

Akiongea Jumatano,Mei 13, 2026, usiku kwenye kipindi cha JKLive kwenye runinga ya Citizen katibu huyo alifafanua kuwa Kenya ingali inaunga mkono juhudi za kuleta amani nchini humo kupitia Shirika la Maendeleo la Ukanda huu (IGAD).

“Vita vinavyoendelea vimechangia wanasiasa na viongozi wa makundi ya kijamii kuhamia mataifa jirani, ikiwemo Kenya, ambako wamesaka usaidizi. Watu kama hawa walioko kwenye shida wanaweza kuruhusiwa kusafiri kwa kutumia paspoti zetu, nyakati fulani. Na hii haimaanishi kuwa paspoti zetu hutolewa kiholela,” Dkt Sing’Oei akaeleza.

Katibu huyo alikariri kuwa Rais William Ruto ataendelea kushirikiana na marais wenzake wa mataifa wanachama wa IGAD kusaka suluhu kwa vita nchini Sudan.

Kauli ya Dkt Sing’Oei ilijiri baada ya serikali kulaumiwa kwa kutoa paspoti kwa raia wa kigeni kwa njia ya kutatanisha.

Hii ni baada ya ripoti kuibuka kuwa Algoney Hamdan Dagalo Musa, kaka mdogo wa kiongozi wa kundi la waasi nchini Sudan Rapid Support Forces (RSF) Mohamed Hamdan Dagalo, ni miongoni mwa wanachama wa kundi hilo waliopewa paspoti za Kenya.

Musa, ambaye ni mmoja wa viongozi wakuu wa RSF amewakewa vikwazo na Amerika na Umoja wa Ulaya.

Vinara wa upinzani wakiongozwa na kiongozi wa chama cha Democracy for Citizen’s Party (DCP) Rigathi Gachagua, na viongozi wa makundi ya kijamii, wameisuta serikali kwa kutoa paspoti kwa wafuasi wa RSF; kundi ambalo limetajwa na Amerika kuwa la kigaidi.