Habari Mseto

Huenda mshukiwa wa mauaji KNH Kalombotole akachunguzwa akili Afrika Kusini

Na RICHARD MUNGUTI May 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MSHUKIWA wa mauaji ya wagonjwa hatika hospitali ya kitaifa ya Kenyatta, Nairobi, Kennedy Kalombotole sasa atafanyiwa uchunguzi wa afya ya akili na jopo la wataalamu watatu wa magonjwa ya akili katika hospitali ya Mathari ili kubaini iwapo yuko sawa kushtakiwa mahakamani.

Mahakama Kuu ya Kibera ilitoa agizo hilo baada ya kuwasilishwa kwa ripoti mbili zinazokinzana kuhusu hali ya akili ya mshukiwa huyo.

Jaji alisema kuwa ikiwa madaktari hao watashindwa kukubaliana kuhusu hali yake ya kiakili, basi mahakama itazingatia uwezekano wa kumpeleka Afrika Kusini kwa uchunguzi zaidi.

“Ikiwa jopo la wataalamu wa Mathari halitafikia uamuzi wa pamoja kuhusu uwezo wake wa kujibu mashtaka, basi mahakama inaweza kuomba tathmini ya nje kutoka Afrika Kusini,” alisema jaji huyo.

Kalombotole anakabiliwa na mashtaka ya kuwaua wagonjwa wawili katika Hospitali ya Kenyatta mnamo Februari na Julai 2025. Hata hivyo, bado hajajibu mashtaka kutokana na wasiwasi kuhusu hali yake ya akili.

Mahakama iliambiwa kuwa ripoti kutoka KNH ilionyesha mshukiwa huyo hana akili timamu na anahitaji uangalizi wa muda mrefu.

“Anapaswa kubaki hospitalini kwa muda mrefu kwa sababu ripoti iliyowasilishwa mahakamani inaonyesha kuwa ni mgonjwa,” jaji alisema.

Upande wa mashtaka ukiongozwa na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma uliomba mshukiwa huyo afanyiwe uchunguzi mpya mbele ya jopo la wataalamu watatu wa magonjwa ya akili katika hospitali ya Mathari.

“Tunaamini jopo la wataalamu wa magonjwa ya akili katika Mathari linafaa kumchunguza ili suala hili lipate hitimisho,” upande wa mashtaka uliambia mahakama.

Jaji alikubaliana na ombi hilo akisema mahakama haiwezi kutegemea ripoti zinazokinzana bila uchunguzi wa kina.