Wabunge wapata afueni Koome akiruhusu rufaa yao ya marupurupu yaliyokanyagiwa na SRC
MAHAKAMA ya Juu imewaruhusu wabunge kukata rufaa dhidi ya marupurupu tata yanayolipwa kwa vikao vya kamati, ambayo hapo awali yalifutwa na Mahakama Kuu na uamuzi huo ukadumishwa na Mahakama ya Rufaa mwaka uliopita.
Jopo la majaji watano wakiongozwa na Jaji Mkuu Martha Koome lilisema limeridhishwa kuwa Tume ya Huduma za Bunge (PSC) imeonyesha sababu za msingi na zinazokubalika zilizofanya ichelewe kuwasilisha rufaa hiyo.
Mahakama ya Rufaa ilikuwa imetupilia mbali rufaa ya wabunge mnamo Februari mwaka jana.
PSC ilikuwa na siku 14 za kuwasilisha rufaa yake lakini iliwasilisha siku saba baada ya muda kuisha.
Tume ya Kutathmini Mishahara na Marupurupu (SRC) ilikuwa imepinga rufaa hiyo ikisema itaanzisha tena kesi ambayo tayari ilikuwa imekamilika.
“Kwa mtazamo wetu, kucheleweshwa kwa siku saba kuwasilisha jibu si kosa, na isitoshe PSC imetoa sababu zinazoeleweka kuhusu kuchelewa huko ambazo hazijapingwa kwa uzito wowote na SRC. Kwenye pingamizi, SRC imetoa tu sababu za jumla,” mahakama ikasema.
Mahakama ilitupilia mbali hofu ya SRC kuhusu kufunguliwa upya kwa kesi iliyokuwa imehitimishwa ikisema kulingana na Katiba, Mahakama ya Juu ina mamlaka ya kusikiliza rufaa na kufunguliwa upya kwa kesi zilizokamilika hazina athari kwa SRC.
Awali, Mahakama ya Rufaa ilikuwa imeamua kuwa hatima ya wabunge ilikuwa tayari imeamuliwa wakati Bunge lilipokutana na SRC na kufikia makubaliano kuhusu mishahara na marupurupu.
Mahakama ilibainisha kuwa katika maelewano yaliyofikiwa na SRC mnamo 2023, Bunge lilikubali kufuata mwongozo wa SRC kuhusu mshahara na marupurupu yao.
Katika rufaa ya pili, PSC inadai kuwa mahakama za chini zilishindwa kushughulikia maswali ya kikatiba yenye umuhimu mkubwa sana kuhusu mamlaka yake na yale ya SRC katika kuamua marupurupu yao.
Mnamo Agosti 2023, SRC iliweka marupurupu ya vikao vya kamati kuwa Sh15,000 kwa kila kikao kwa mwenyekiti wa kamati (Sh240,000 kwa mwezi), naibu mwenyekiti akawekewa Sh12,000 (Sh192,000 kwa mwezi) kisha Sh7,500 kwa mwanachama (Sh120,000 kwa mwezi).
Mzozo huo ulianza kutokana na uamuzi wa Mahakama Kuu wa mnamo 2020 uliobatilisha marupurupu ya nyumba ambayo wabunge walikuwa wamejilipa wenyewe.