Wakora wageuza maandamano uwanja wa kukamua raia ‘ushuru’
KILICHOANZA kama maandamano kote nchini kuhusu bei ghali za mafuta na janga la usafiri kiligeuka upesi kuwa matukio ya kutisha, upunjaji na ghasia zilizopangwa kote katika barabara kuu, maeneo ya makazi na miji nchini.
Kufikia alfajiri, matatu zilitoweka barabarani Nairobi, Kiambu, Kajiado, Eldoret kaunti nyinginezo huku wahudumu wakilalamikia bei mpya za mafuta zilizotangazwa.
Waendeshaji magari waliojaribu kufika kazini licha ya maandamano hayo, barabara ziligeuka nyanja za mawindoni.
“Ulipata wapi mafuta?” Waandamanaji waliwauliza madereva waliokwama kwenye vizuizi.
Kama jibu halikuwaridhisha, waendeshaji magari waliagizwa kulipa kilichoitwa na magenge “ushuru” Kikuyu na “ada” Ruiru.
Malipo hayo yalianzia Sh50 hadi Sh1,000 kutegemea na walivyohisi wanaume waliolinda vizuizi vya barabarani.
Barabara ya Southern Bypass, Kikuyu, maandamano yaligeuka uhalifu hadharani.
Stendi ya mabasi ambayo kwa kawaida hujaa matatu zinazopakia abiria kutoka alfajiri hadi jioni, ilifanana mahame.
Hakukuwa na magari kituoni humo. Badala yake, mamia ya vijana, wengine wakiwa wamevalia fulana zenye kofia na maski, waliobeba vijiti na mawe waliketi hapo.
Kufikia saa moja asubuhi, barabara ya Southern Bypass haikupitika. Tairi ziliteketezwa huku miamba ikitapakaa kwenye barabara kuu na magari yaliyodhubutu kuingia eneo hilo yalijihatarisha.
Mwendo wa saa tano kasoro dakika ishirini Katibu wa Wizara ya Usalama wa Ndani, Raymond Omollo alisimama kwa dakika chache karibu na Southern mkabala na mji wa Kikuyu, kuzungumza na maafisa waliotumwa kurejesha utilivu eneo hilo.
Polisi waliposonga kuelekea makutano ya Kikuyu Gitaru kuwatawanya waandamanaji waliofunga barabara kuu ya Nairobi-Nakuru, makundi mapya ya vijana yalizuka ghafla na kuwasha moto na kuweka vizuizi vya barabarani kama waliopanga.
Matukio sawia yalishuhudiwa kote nchini.
Kitengela, mamia ya waandamanaji walivamia bohari ya Coca-Cola adhuhuri na kuharibu majengo, kupora bidhaa na kuwazidi nguvu maafisa wa polisi.
Kwenye barabara kuu ya Namanga na vijia vinavyounganishwa nayo, waandamanaji waliangika mabango na kulemaza usafiri.
Mwihoko, mwendeshaji gari alisimulia jinsi alivyolazimishwa kulipa Sh200 ili kupita kizuizi kilichodhibitiwa na vijana.
Kwenye barabara ya Thika Road, gari nyeusi aina ya Mazda iliteketezwa Githurai.
Eldoret, polisi wa kuzima ghasia walikabiliana na waandamanaji waliofunga barabara kuu ya Eldoret-Huruma-Kitale, huku magenge yakiweka vizuizi vipya kwenye barabara ya Eastern Bypass na Kamaki Road, Nairobi.
Wote, Makueni, waandamanaji waliteketeza afisi za chama tawala, UDA.
Kamanda wa Polisi, Nairobi, Issah Mohamud baadaye aliiri kuwa hali iligeuka kinyume cha maandamano ya amani.
“Walianza kufunga barabara kwa kutumia miamba na mawe,” alisema katika mkutano na vyombo vya habari akisema makundi yaliyojihami yalitatiza biashara na utulivu wa umma.