Oburu: Mimi ni mzee ndiyo lakini bado niko maarufu ndani ya ODM
KIONGOZI wa ODM Dkt Oburu Oginga amewataka viongozi wanaoshikilia nyadhifa chamani ilhali wanaendelea kuikosoa hadharani, wahame kujiunga na vyama vingine.
Dkt Oginga alisema hataendelea kuvumilia maasi ndani ya chama hicho na kuwaonya wanaofikiria kuwa umri wake mkubwa umelemaza umaarufu wake ndani ya ODM.
Alisema viongozi waasi ndani ya chama hicho wamesahau suala la nidhamu ambalo pia ni msingi wa demokrasia.
Seneta huyo wa Siaya alikuwa akiongea jijini Kisumu wakati wa mkutano na wajumbe wa ODM kutoka Luo Nyanza.
Dkt Oginga aliwaambia wanaompiga vita kwa sababu ya uzee na kusema kuwa waasi hao wakishaondoka chamani, hata wakirejea hawatapata nyadhifa zao.
Kauli yake inaonekana ilikuwa ikimlenga Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi ambaye aliyatoa masharti mapya kwa Dkt Oginga kuhusu mrengo wa Linda Mwananchi kurejea ODM.
Bw Osotsi alikuwa akidai kuwa kambi ya Linda Ground ndiyo ilisababisha mpasuko chamani na kuingia ushirikiano wa kisiasa na Rais William Ruto.