Habari za Kaunti

Kijiji chashtuka kijana, 19, akimuua mwanafunzi, 16, na kisha kujitia kitanzi katika mzozo wa kimapenzi

Na RUTH MBULA May 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAKAZI wa kijiji cha Ntana, Mugirango Kaskazini Kaunti ya Nyamira wanaomboleza kifo cha msichana ambaye alidungwa kisu na mpenziwe kisha baada ya kutekeleza mauaji kijana huyo akajinyonga.

Cheryl Portia Sitima, 16, ambaye alikuwa mwanafunzi wa Kidato cha Nne, alidungwa kisu na Bivon Thomas Obare, 19.

Alikuwa mwanafunzi katika Shule ya Wasichana ya Mwongori katika kaunti hiyo hiyo ya Nyamira.

Obare alifanya mtihani wake wa kidato cha nne katika Shule ya Wavulana ya Gekano mwaka jana na alikuwa akisubiri kujiunga na chuo kikuu.

Obare alijitia kitanzi katika nyumba yao kwa kutumia kamba na mwili wake ulipatikana unaning’inia kutoka kwenye paa.

Babake Portia, Bw James Momanyi alieleza kuwa walikuwa wamemchukua kutoka shuleni mnamo Alhamisi ili ahudhurie mazishi ya babake mnamo Ijumaa.

“Alikuwa na nduguze hadi kitu saa saba usiku alipolemewa na uchovu na akaenda kulala. Binti yangu na nduguze waliamua kuwasindikiza marafiki zao ambao pia ni majirani wetu,” akasema Bw Momanyi.

“Hapo ndipo waligundua kuna mtu alikuwa akiwafuata na waliposimama kuanza kupambana naye, alimdunga Portia kwa kisu kwenye kifua,” akasema. Tukio hilo lilimzuia kuhudhuria mazishi ya babake.

Alisikitika kuwa sasa amezongwa na mauti mara mbili kwa kuwa babake alizikwa mnamo Ijumaa naye bintiye bado yupo katika chumba cha kuhifadhia maiti.

“Tunataka doria izidishwe na vijana wapewe mafunzo jinsi ya kuishi kwa kuzingatia maadili,” akasema Bw Momanyi.

Mamake Portia Zainab Nyarinda Ocharo anasema mwanawe alikuwa mpole na alikuwa akimsaidia majukumu mengi wala haelewi kwa nini uhai wake umekatizwa ghafla.

“Alikuwa na ndoto ya kuwa daktari na kutuondoa kwenye umaskini lakini sasa hayupo. Alikuwa akinisaidia kazi za nyumbani na kunitia moyo kuwa maisha yangekuwa afadhali akimaliza masomo na kupata kazi,” akasema.

Chifu wa Bomwagamo James Ombati alisema alipokea simu mnamo Ijumaa usiku kuhusu tukio hilo na Portia akaaga dunia baada ya kufikishwa katika Hospitali ya Kinara, Nyamira.

Bw Ombati alifichua kuwa aliwaita maafisa wa polisi ambao wanachunguza tukio hilo la huzuni.