Akili MaliMakala

Mgomo wa matatu dhidi ya mafuta ulivyonogesha biashara yake ya miwa

Na SAMMY WAWERU May 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MGOMO wa wahudumu wa matatu ambao umesitishwa kwa muda wa siku saba ukiendelea, baadhi ya wachuuzi wa bidhaa za kula katika Kaunti ya Nairobi walitumia jukwaa hilo kuvuna hela.

Mmoja wa wachuuzi hao ni Joshua Makau ambaye huuza miwa na mnamo Jumanne, Mei 19, 2026 kabla mgomo huo wa kitaifa kutangazwa kusimamishwa kwa muda, alidokeza kwamba siku mbili zilizopita mapato yake yalikuwa ya kuridhisha.

Kwenye mahojiano ya kipekee na Taifa Dijitali, Makau alifichua kwamba jana pekee – Jumatatu, Mei 18, mgomo ulipoanza, alimaliza kufanya mauzo mapema.

“Kufikia saa nane mchana, nilikuwa nimekamilisha kuuza stoki ya miwa ya siku,” alisema. Hilo, ni kinyume na siku za kawaida ambapo toroli (wilibaro) moja humchukua siku nzima kukamilisha. “Siku zingine, huuza wilibaro moja kwa muda wa siku mbili,” alidokeza. Kazi nayo hufunga kuanzia saa mbili za jioni.

Wakati wa mahojiano tulimpata kwenye barabara ya Thika, maarufu kama Thika Super Highway, Kasarani, pamoja na wachuuzi wenza wa miwa.

Joshua Makau mchuuzi wa miwa Thika Road, wakati wa mgomo wa matatu dhidi ya bei ya mafuta ya petroli mnamo Jumanne, Mei 19, 2026, akikatakatia wateja wake miwa. picha|Sammy Waweru

Bei, kipande kifupi huuza Sh20 na kile kirefu Sh50. “Wilibaro moja huwa na wastani wa Sh1, 200 na kwa muda wa siku mbili zilizopita (maandamano ya matatu) nimeunda pesa nzuri,” Makau alieleza.

Licha ya usafiri wa umma Thika Road Jumatatu na Jumanne kuathirika, mfanyabiashara huyo rejareja alielezea kuridhishwa kwake na jinsi wateja walijitokeza kwa wingi. Aidha, wengi wao walikuwa waliokuwa wakielekea kazini kwa miguu.

Baadhi ya wanunuzi walisema wametoka Machakos na baada ya kuwekwa na gari lililowabeba eneo la Nyayo, Nairobi, walilazimika kusafiri kwa miguu hadi Juja. “Miwa inatupa nguvu kuelekea kazini,” wakaambia Taifa Dijitali mwendo wa saa nne na dakika ishirini na tatu asubuhi (10:23am).

Maeneo mengi ya nchi kwa muda wa siku mbili mfululizo, ilishuhudia maaandamano dhidi ya bei ya mafuta ya petroli yaliyoandaliwa na wahudumu wa matatu, na wadauhusika wengine kwenye sekta ya usafiri na uchukuzi, wakiwemo sekta ya utalii na matrela ya masafa marefu.

Wachuuzi wa miwa kando kando mwa Thika Road, Kasarani wakati wa maandamano dhidi ya bei ya mafuta mnamo Jumanne, mei 19, 2026. Picha|Sammy Waweru

Jumanne mchana, serikali kupitia Waziri wa Usalama wa Ndani, Kipchumba Murkomen ilitangaza mgomo kusitishwa kwa muda wa siku saba ili kuruhusu mazungumzo kati ya pande zote. Jumatatu usiku, hali ya vute nikuvute ilishuhudiwa huku wahudumu wa matatu wakipinga hadharani pendekezo la Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi kushusha bei ya mafuta kwa Sh10.

Wamiliki na wahudumu wa matatu wanapinga bei ya juu ya petroli ambapo Mamlaka ya Kudhibiti Kawi na Petroli (EPRA) mnamo Alhamisi, Mei 14, 2026 ilitathmini bei itakayotumika kati ya Mei hadi Juni 14.

Aidha, EPRA iliongeza bei ya dizeli kwa Sh46.29 kwa lita, huku bei ya petroli ikiongezeka kwa Sh16.65 kwa lita. Hivyo basi, petroli sasa inauzwa Sh214.25 kwa lita na dizeli kwa Sh242.92, huku bei ya mafuta ya taa ikisalia Sh152.78.