OneTam! Gachagua ajiandaa kujibwaga ulingoni
KATIKA muda wa miezi 18 tangu kufurushwa kwake madarakani kama Naibu Rais, Rigathi Gachagua amejikita katika siasa za ushindani mkali, akiongoza kampeni ya kuunganisha kura za Mlima Kenya dhidi ya Rais William Ruto, huku akimshutumu kwa “usaliti wa kisiasa” na kujitambulisha kama msemaji mkuu wa eneo hilo kuelekea uchaguzi mkuu 2027.
Katika mpango wake mpana wa kuimarisha nguvu za kisiasa katika eneo hilo, Gachagua alianzisha chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP), ambacho amekitumia kama jukwaa la kuunganisha wafuasi wake na kuimarisha ushawishi wake katika siasa za kitaifa.
Chama hicho kimekuwa kivutio kikubwa kwa wanachama wanaotoka vyama mbalimbali, ikiwemo United Democratic Alliance (UDA) ya Rais Ruto na Chama cha Jubilee, hali inayoashiria mabadiliko ya kina katika mwelekeo wa kisiasa wa Mlima Kenya.
Awali, Gachagua alionekana kuchukua msimamo wa tahadhari kuhusu kugombea urais, hasa kutokana na mjadala wa kisheria kuhusu uhalali wake baada ya kuondolewa madarakani. Katika kipindi hicho, alionekana kuelekeza nguvu zake katika kumuunga mkono kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka kama mgombea wa muungano wa upinzani dhidi ya Ruto.
Hata hivyo, mabadiliko ya hivi karibuni ya kisiasa, kesi ya kupinga kuondolewa kwake mahakamani, na ongezeko la ushawishi wake katika Mlima Kenya yameongeza uwezekano wa yeye kuwania urais moja kwa moja.
Bw Gachagua mwenyewe ametangaza kwamba atagombea urais. Hata hivyo, tamko lake hilo limechukuliwa kama sehemu ya mbinu za kawaida za kisiasa ndani ya kambi ya Muungano wa Upinzani, ambao bado unajipanga kumteua mgombea mmoja wa pamoja atakayemkabili Rais Ruto.
Hata hivyo, ni kauli za hivi karibuni kutoka kwa washirika wake ambazo zimeibua mjadala mkali wa kisiasa, wakisisitiza kwamba Bw Gachagua ana nafasi kubwa ya kumshinda Rais Ruto kutokana na wingi wa kura za Mlima Kenya.
Makadirio ya kisiasa yanaonyesha kwamba, Mlima Kenya wana uwezo wa zaidi ya kura7.4 milioni katika uchaguzi wa 2027, kutoka kaunti 10 zikiwemo Kiambu, Murang’a, Nyeri, Kirinyaga, Embu, Meru, Laikipia, Nyandarua, Tharaka-Nithi na Nakuru.
Katika uchaguzi wa 2022, eneo hilo lilimpa Rais Ruto takriban kura milioni tatu. Hata hivyo, idadi ya wapiga kura inaendelea kuongezeka kutokana na usajili mpya wa wapiga kura, jambo linalofanya eneo hilo kuwa na usemi mkubwa zaidi katika siasa za kitaifa.
Gachagua mwenyewe amekuwa akitoa ishara kwamba, anaweza kuwania kiti cha urais, kauli ambazo zimeibua mjadala mkali ndani ya upinzani kuhusu uwezekano wa mgombea mmoja au vinara kugawanyika. Wafuasi wake wanasema ana nguvu ya kipekee ya kuvutia wapiga kura, hasa katika Mlima Kenya, na hivyo anafaa kuwa mgombea mkuu wa upinzani dhidi ya Ruto. Mbunge wa Embakasi Central Benjamin Gathiru alisema Gachagua ndiye “injini ya upinzani” kwa sasa, akisisitiza kuwa ana uwezo mkubwa wa kuvutia kura kuliko viongozi wengine wa mrengo huo.
“Yeyote anayeleta kura nyingi ndiye anapaswa kuwa mgombea. Hatuwezi kuwa na watu wanaosubiri kazi ifanywe na Gachagua kisha wao wachukue nafasi ya uongozi,” alisema.
Naye Seneta wa Nyandarua John Methu alisema Gachagua ana uwezo mkubwa wa kisiasa kuliko wapinzani wake na kwamba, ni “mhusika mkuu” ndani ya muundo wa upinzani.
Aliongeza kuwa mgombea anayevutia kura nyingi anapaswa kupewa tiketi ya moja kwa moja ili kuepuka migawanyiko.
Hata hivyo, hali hiyo imeibua wasiwasi ndani ya upinzani, ambapo baadhi ya viongozi wanaonya kuwa kugombea kwa Gachagua kunaweza kurudia historia ya mgawanyiko kama wa 1992, ambapo upinzani uliogawanyika ulimsaidia Rais wa wakati huo Daniel arap Moi kushinda uchaguzi.
Wachambuzi wa siasa wanasema Gachagua anaweza kuwa na ushawishi mkubwa katika Mlima Kenya, lakini kugombea kwake kunaweza kugawanya kura za upinzani katika ngazi ya kitaifa.
Kwa mujibu wa wachambuzi, upinzani una majina mengine makubwa kama Kalonzo Musyoka, Fred Matiang’i, Eugene Wamalwa na Martha Karua, ambao pia wanaaminiwa kuwa na kura katika maeneo yao, lakini si kwa kiwango cha Mlima Kenya.
Wafuasi wa Gachagua wanasisitiza kuwa, kila mgombea lazima alete kura zake mezani kabla ya mazungumzo kuhusu tiketi ya upinzani, wakisema kuwa si haki kumtaka Gachagua asigombee ilhali yeye anavutia kura nyingi.
“Hatuwezi kusema Gachagua asigombee wakati ndiye anafanya kazi kubwa ya kurai watu. Wengine wanapaswa pia kuonyesha nguvu zao,” alisema Mbunge Gathiru.
Hata hivyo, upande mwingine wa upinzani unasema bado kuna haja ya mazungumzo ya pamoja ili kuepuka kugawanyika.
Seneta wa Makueni Dan Maanzo alisema upinzani utaendelea na mchakato wa kumpata mgombea mmoja atakayemkabili Rais Ruto, akisisitiza kuwa makubaliano bado yanawezekana.
Wakati huo huo, mchambuzi wa siasa Prof David Monda alisema hatua ya Gachagua inaweza kumsaidia Ruto zaidi kuliko kumdhuru, akionya kuwa siasa za kikabila zinaweza kutawala uchaguzi ujao.
Alisema endapo Gachagua ataongoza tiketi ya urais, inaweza kuonekana kama “mamlaka na jamii moja,” hali inayoweza kuimarisha kampeni ya Ruto katika maeneo mengine ya nchi.
Aidha, alionya kuwa upinzani ukishindwa kukubaliana, unaweza kurudia makosa ya miaka ya 1990 ambapo mgawanyiko ulifanya wagombea wa chama tawala kushinda kwa urahisi.