Ebola: Timu ya DR Congo kujitenga kwa siku 21 kabla kutua USA kwa Kombe la Dunia
TIMU ya taifa ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DR Congo) itahitajika kujitenga kwa siku 21 nchini Ubelgiji kabla ya kuruhusiwa kuingia nchini Amerika kunogesha Kombe la Dunia, kufuatia mkurupuko wa ugonjwa wa Ebola nchini mwao.
DR Congo kwa sasa inafanya mazoezi nchini Ubelgiji baada ya kambi yake ya maandalizi iliyokuwa ifanyike mjini Kinshasa kufutwa kutokana na hali ya kiafya nchini humo.
Mkurugenzi wa jopo kazi la Ikulu ya White House linalosimamia masuala ya Kombe la Dunia, Andrew Giuliani, alisema wachezaji wa DR Congo wanapaswa kusalia katika mazingira maalum ya kujitenga [‘bubble’ kwa Kimombo] hadi watakapopata ruhusa ya kusafiri.
“Lazima waendelee kusalia kwenye ‘bubble’ hiyo, la sivyo huenda wasiruhusiwe kusafiri kwenda Amerika,” Giuliani alisema.
Hatua hiyo imechukuliwa baada ya Kituo cha Kudhibiti Maradhi (CDC) cha Amerika kupiga marufuku watu wasiokuwa raia wa Amerika ambao wamekuwa DR Congo, Uganda au Sudan Kusini katika kipindi cha siku 21 zilizopita kuingia nchini humo.
Hata hivyo, wachezaji wote wa DR Congo wanaocheza nje ya nchi yao hawataathiriwa moja kwa moja na masharti hayo baada ya kufutwa kwa kambi ya Kinshasa.
Giuliani alionya kuwa watu wengine watakaoungana na kikosi hicho lazima wawe katika bubble tofauti ili kuepusha hatari ya maambukizi.
“Ikiwa mtu yeyote atapatikana na dalili za ugonjwa huo, anaweza kuhatarisha kikosi kizima kushindwa kushiriki Kombe la Dunia,” alisema.
Shirika la Afya Duniani (WHO) mnamo Ijumaa lilipandisha kiwango cha hatari ya mlipuko wa Ebola nchini DR Congo kutoka “kikubwa” hadi “kikubwa sana”.
Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt Tedros Adhanom Ghebreyesus, alisema hatari ya ugonjwa huo kusambaa katika eneo la Afrika Mashariki na Kati bado ni kubwa, lakini kiwango cha hatari duniani kwa sasa kinaendelea kuwa cha chini.
DR Congo imepangiwa mechi za kirafiki dhidi ya Denmark Juni 3 nchini Ubelgiji na Chile Juni 9 nchini Uhispania kabla ya kuanza kampeni yake ya Kombe la Dunia.
Michuano hiyo itachezwa kati ya Juni 11 na Julai 19 nchini Marekani, Mexico na Canada huku DR Congo ikitarajiwa kufungua kampeni yake dhidi ya Ureno Juni 17.