Dimba

Jnr Starlets kupambana na Uganda leo mechi ya kufuzu Kombe la Dunia U17

Na TOTO AREGE May 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Timu ya Junior Starlets ya wachezaji chini ya miaka 17 Ijumaa, itamenyana na Uganda katika mechi ya mkondo wa kwanza wa raundi ya pili ya kufuzu Kombe la Dunia la Wanawake la mwaka huu. 

Mechi hiyo itachezwa katika Uwanja wa FUFA Kadiba mjini Kampala Uganda kuanzia saa kumi jioni. Kisha mechi ya marudiano itachezwa tarehe 30 mwezi huu katika Uwanja wa Kitaifa wa Nyayo jijini Nairobi saa tisa mchana.

Mshindi wa jumla ya mabao atafuzu raundi ya tatu na ya mwisho na atakutana na mshindi kati ya Tanzania na Afrika Kusini mwezi ujao. Mshindi katika raundi hii, atafuzu Kombe la Dunia ambalo litaandaliwa nchini kuanzia Oktoba 17 hadi Novemba 7.

Taifa hilo kutoka Afrika Kaskazini pia, litakuwa mwenyeji wa mashindano hayo kwa miaka mitano mfululizo kuanzia 2025 hadi 2029.

Kenya chini ya kocha Mildred Cheche, ilitinga hatua hii baada ya kuinyorosha Namibia kwa jumla ya mabao 7-1 katika raundi ya kwanza mwezi jana ambapo walishinda 2-1 ugenini na 5-0 nyumbani. Huku Uganda ikisonga mbele baada ya kuiondoa Zimbabwe kwa jumla ya mabao 6-1, 0-2 ugenini na 4-1 nyumbani.

Kuelekea mechi hii, Kenya inapigiwa upato kushinda ikilinganishwa kwamba, Kenya iliinyorosha Uganda 5-0 kwa jumla ya mabao (0-2, 0-3) mwaka jana, katika raundi sawa na hii ya kufuzu Kombe la Dunia U17 na kubandiliwa nje ya michuano hiyo ya kufuzu.

Ingawa wachezaji kama washambuliaji Edinah Nasipwondi, Joan Ogola, Patience Asiko ambao walifunga katika mechi hizo mbili dhidi ya Uganda, hawako kwenye kikosi cha mwaka huu kwani, wameingia kwenye timu ya Rising Starlets ya wachezaji wasiozidi miaka 20.

Mchezaji ambaye amesalia ni mshambuliaji Brenda Achieng’ ambaye alichangia bao katika ushindi wa nyumbani wa 3-0. Achieng’ pia atakuwa tegemeo katika mechi hii ikilinganishwa kwamba, alifunga mabao matatu (hattrick) dhidi ya Namibia mwezi jana.

Kikosi cha Starlets cha wachezaji 23, kilifanya mazoezi yake ya mwisho katika uwanja wa FUFA jioni jana kuelekea mechi hii. Uganda almaarufu Teen Cranes nao waliamilisha mazoezi yao mapema jana katika uga huo huo.

Cheche, ambaye aliandika historia kwa kuipeleka Kenya katika Kombe la Dunia la U17 katika Jamhuri ya Dominican kwa mara ya kwanza 2024, kabla ya kuondoka nchini Jumanne wiki hii, alidhibitisha mabadiliko matatu kwenye kikosi kutokana na majeraha ya wachezaji wawili muhimu.

“Rose Nangila aliumia akiwa shuleni Uganda nae Lindey Weey ana jeraha la kiuno linalomzuia kukimbia vizuri. Anahitaji angalau wiki mbili za matibabu,” alielezea Cheche.

Mapengo hayo yamejazwa na Daisy Adongo ambaye ataongeza nguvu kwenye safu ya ulinzi, na Grace Wangari ambaye ataimarisha mashambuliaji. Noelina Akuku ni sura mpaya kwenye kikosi kama kiungo kutokana na uwezo wake wa kucheza nafasi tofauti.