Bambika

Hincapie akiri kuchangamkiwa na mademu baada ya kaptura kumtoka uwanjani

Na SINDA MATIKO June 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

PIERO Hincapie amekiri kwamba alipata jumbe nyingi kutoka kwa “wanawake wengi” baada ya suruali yake kudondoka na kuacha wazi makali yake katika ushindi wa 1-0 uliosajiliwa na Arsenal dhidi ya Burnley mnamo Mei 18.

Wakati wa mchuano huo wa mwisho wa nyumbani kwa Arsenal msimu huu, kabla ya kutawazwa mabingwa wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL), Hincapie aliangushwa na suruali yake kuvuliwa.

Mchezaji huyo wa Ecuador alikuwa akikabiliana na Axel Tuanzebe alipoanguka baada ya kupigwa mlazo na kaptura kuacha wazi sehemu kubwa ya makalio yake yakitazamwa na mashabiki.

Kwa haraka, alijiviringisha na kuvuta juu kaptura yake huku akijifunika kwa makini sehemu zake za siri kabla ya kuendelea na mchezo.

Akizungumza na CBS Sports Golazo kabla ya mechi ya kunogesha fainali ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) iliyoshuhudia Arsenal wakifungwa penalti 4-3 na Paris Saint-Germain (PSG) kufuatia sare ya 1-1 mnamo Jumamosi iliyopita, mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 24 alichekesha sana kuhusu tukio hilo.

Alisema: “Ni jambo lililozua ucheshi na aibu. Nataka kuwa mkweli. Kwanza nilikerwa kisha nikaishia kufurahia jambo lenyewe baada ya kuona mijadala katika mitandao ya kijamii.”

Alipoulizwa kuhusu jumbe alizopata kutokana na tukio hilo, Hincapie alisema: “Ni kama waliofurahia sana na picha hiyo ni wanawake. Walinitumia jumbe nyingi za kunitaka kimapenzi. Nahisi kwamba walichokiona au walichotarajia kuona kiliwapendeza sana.”

Hincapie alichezea Arsenal mechi 39 katika mashindano yote msimu huu huku akifunga bao moja na kuchangia mengine mawili.