Chuki na mashambulizi dhidi ya wageni yachacha Afrika Kusini
KLEINMOND, Afrika Kusini:
SIKU nne zilizopita, mhamiaji kutoka Msumbiji, Lado Amido, alifungua mlango wake baada ya kusikia hodi katika mji wa Kleinmond nchini Afrika Kusini.
Alipofungua, alikutana na umati wenye hasira uliomwambia kuwa wageni kama yeye walipaswa kuondoka. Kundi hilo lilikuwa likizunguka nyumba kwa nyumba likitoa ujumbe huo huo.
Amido alikimbia na kujificha milimani kwa siku mbili. Sasa anaishi katika ukumbi wa mji huo pamoja na wahamiaji wengine kutoka Malawi na Msumbiji katika Mkoa wa Western Cape.
Wote wamelazimika kujificha kutokana na makundi yenye chuki dhidi ya wageni yaliyoshambulia miji kadhaa ya maeneo ya pwani.
Kisa chake kinaonyesha tu jinsi Afrika Kusini inaendelea kukumbwa na wimbi la maandamano dhidi ya wahamiaji.
Kutokana na hatari iliyoko, serikali ya Msumbiji ilisema raia wake watano waliuawa katika mji wa Mossel Bay.
Amido anaishi Kleinmond, takriban kilomita 300 kutoka Mossel Bay.
“Mei 31, watu walifika nyumbani kwangu, wakagonga mlango na kisha wakachukua mali yangu yote,” akasema Amido, 49.
Amekuwa Afrika Kusini tangu Februari baada ya kuwasili nchini humo kutafuta kazi.
Katika ukumbi wa mji wa Kleinmond, anaishi pamoja na takriban wahamiaji 100 wengine, baadhi yao wakitarajia kurejea makwao.
Mashambulizi dhidi ya wageni yamekuwa yakiendelea Afrika Kusini kutokana na madai kuwa wamechangia matatizo ya kiuchumi kama ukosefu mkubwa wa ajira na uhalifu.
Hii ni licha ya kutokuwepo ushahidi unaothibitisha madai hayo.
Wanasiasa kutoka karibu vyama vyote vya siasa nao wamekuwa wakitoa kauli zinazounga mkono mtazamo huo ili kuvutia kura za wananchi.
Haya yanafanyika kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwaka huu.
“Tunapoendelea kujenga jamii salama na yenye ustawi zaidi, tunapaswa kushughulikia changamoto ya uhamiaji,” Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa akigusia suala hilo ambalo limekashifiwa na mataifa mengi Afrika.