Habari

Siasa za uhuni zatanda Kisii uchaguzi wa 2027 ukikaribia

Na RUTH MBULA June 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

SIASA za kutumia makundi ya wahuni kuwashambulia wapinzani zinaonekana kushika kasi katika Kaunti ya Kisii huku visa vya mashambulizi mchana peupe vikizua hofu miongoni mwa wakazi.
Wakazi sasa wanazitaka idara za usalama kuchukua hatua kali dhidi ya wahusika wa mashambulizi hayo yanayodaiwa kufadhiliwa na baadhi ya viongozi wa kisiasa huku uchaguzi mkuu wa 2027 ukikaribia.
Mashambulizi ya hivi punde yalitokea Alhamisi asubuhi wakati diwani wa Wadi ya Ichuni, Wyclife Siocha maarufu kama Embande, aliposhambuliwa na kujeruhiwa na kundi la watu wanaoshukiwa kuwa wahuni wa kisiasa.
Bw Siocha alikumbwa na mkasa huo alipokuwa akisimamia gari lake kutengenezwa katika gereji moja katikati mwa mji wa Kisii. Walioshuhudia walisema watu waliokuwa na silaha butu walimvamia, wakampiga na kumwacha akiwa amepoteza fahamu huku na majeraha mabaya kichwani.
Baada ya shambulizi hilo, washambuliaji walitoroka.
Tukio hilo lilisababisha taharuki katika mji wa Kisii huku wakazi wakihofia kuwa amani eneo hilo iko hatarini iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa.
Takriban wiki mbili zilizopita, Bw Siocha, ambaye hapo awali alikuwa mshirika wa karibu wa Gavana wa Kisii Simba Arati, alitangaza kujiunga na kundi la “Wantam” na kumuunga mkono mgombea urais wa Jubilee, Dkt Fred Matiang’i.
Baada ya kushambuliwa, alilazwa katika hospitali mjini Kisii akiwa na uvimbe mkubwa kichwani, usoni na mdomoni huku familia yake ikifanya mipango ya kumhamishia Nairobi kwa matibabu maalum.
Walioshuhudia walisema mmoja wa washambuliaji alimlaumu MCA huyo kwa “usaliti” kabla ya kuanza kumpiga.
Bw Siocha pia aliwahi kuwa miongoni mwa viongozi waliochangia kufanikisha kuondolewa madarakani kwa aliyekuwa Naibu Gavana wa Kisii, Dkt Robert Monda Onsare. Hata hivyo, alipomuunga mkono Dkt Matiang’i, aliomba msamaha kwa mchango wake katika mchakato huo akidai alipotoshwa.
Baada ya tukio hilo, MCA kadhaa wakiongozwa na aliyekuwa Waziri wa Elimu Ezekiel Machogu walifika Kituo cha Polisi cha Kisii Central wakitaka washukiwa wakamatwe mara moja.
 “Tunapatia polisi saa 12 kuwakamata wahusika ambao wanafahamika. Wakishindwa, wananchi watachukua hatua na kuwapeleka polisi wenyewe,” alionya Bw Machogu.
Bw Machogu aliwashutumu maafisa wa usalama kwa kulegea katika kukabiliana na visa vya vurugu za kisiasa vinavyolenga wapinzani wa Gavana Arati.
Alisema mashambulizi hayo yamekuwa jambo la kawaida huku polisi wakishindwa kuwakamata washukiwa licha ya ahadi nyingi.
“Sisi tumechoka. Hatuwezi kuvumilia tena. Mimi mwenyewe ni mwathiriwa wa mashambulizi kama haya na hadi leo washukiwa wanatembea huru,” alisema.
Waathiriwa wa mashambulizi hayo wamekuwa wakimlaumu Gavana Arati, madai ambayo ameyakanusha vikali.
“Kama unapiga kelele za muhula mmoja na unapigwa, usinilaumu. Sina wahuni. Wale wanaoitwa wahuni ni vijana wenye amani wanaosaidia kudumisha utulivu katika kaunti,” alisema gavana huyo hivi majuzi.
Mapema mwaka huu, msafara wa Bw Machogu pia ulishambuliwa baada ya kuhudhuria hafla ya kanisani katika eneo la Bomachoge Borabu.
Gari lake liliharibiwa na watu wanaoshukiwa kuwa wahuni wa kisiasa.
Ghasia kama hizi zilishuhudiwa hivi majuzi wakati viongozi wa muungano wa upinzani waliposhambuliwa katika mkutano wao katika eneo la Gusii na kundi la watu waliokuwa na mapanga, marungu na silaha nyingine butu.
Wananchi walijibu kwa kuwafukuza washambuliaji hao, huku baadhi yao wakijeruhiwa. Gari aina ya Probox lililodaiwa kutumiwa na wahuni hao lilichomwa moto mjini Keroka na mali nyingine kuharibiwa.
Mwezi uliopita, Obed Mogunda Somoni mwenye umri wa miaka 31 pia alishambuliwa na kulazwa hospitalini kwa zaidi ya wiki moja baada ya kuvunjika nyonga na kupata majeraha kichwani, kifuani, tumboni na mikononi.
Katika tukio jingine, magurudumu ya magari ya MCA watatu wa Kaunti ya Kisii yalitobolewa ndani ya eneo la maegesho ya Bunge la Kaunti wakati kikao kilipokuwa kinaendelea.
Akizungumzia ongezeko la vurugu hizo mapema mwaka huu, Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Lagat aliwaonya wanasiasa wanaowaajiri vijana kufanya vitendo vya uhalifu.
 “Matumizi ya vijana kama wahuni ni jambo linalotutia wasiwasi. Huu ni uhalifu na hatutauvumilia bila kujali anayehusika ni nani,” alisema Bw Lagat.
Aliongeza kuwa vijana wanapaswa kujihusisha na shughuli halali za kiuchumi badala ya kukubali Sh200 au Sh500 ili kutekeleza uhalifu kwa niaba ya wanasiasa.