Seneta apinga mpango wa KPA kuhusu ajira bandarini
SENETA wa Mombasa, Bw Mohamed Faki, amepinga mpango wa Mamlaka ya Bandari za Kenya (KPA) wa kuajiri wafanyakazi wenye ujuzi na vibarua kupitia kwa mkataba na mashirika ya kibinafsi.
Zabuni hiyo ya miaka mitatu, ambayo KNA imeiona, inatarajiwa kusababisha zaidi ya wafanyakazi 4,625 wenye ujuzi na wa kiwango cha kati cha ujuzi kuajiriwa, watafanya kazi kwa zamu tatu.
Wafanyakazi hao watahitajika kurefushiwa mikataba yao kila mwaka.
Kulingana na nyaraka za zabuni, wanatarajiwa kusaidia shughuli za bandari ikiwemo kushughulikia makontena na mizigo, huduma za baharini, uendeshaji wa vifaa na kazi za ukarabati ndani ya maeneo ya bandari.
KPA ilisema kuwa zabuni hiyo inalenga kuhakikisha mizigo inashughulikiwa bora zaidi, na kuharakisha muda wa kuhudumia meli bandarini, kudumisha kiwango cha juu cha uzalishaji na upatikanaji wa vifaa, kuhakikisha shughuli za bandari zinafanyika kwa usalama na kwa kuzingatia sheria.
Vilevile, mpango huo unalenga kuwezesha kuwepo kwa wafanyakazi wenye sifa bora, uwezo na nidhamu, na kusaidia kufikia malengo ya ongezeko la mizigo na mapato.
Akizungumza wakati wa kikao na jamii ya Wachangamwe, ambayo inapakana na Bandari ya Mombasa upande wa magharibi, seneta huyo alisema kuwa zabuni hiyo itamaliza kwa kiasi kikubwa ajira za moja kwa moja zinazofanywa na mamlaka hiyo.
“Hatari yake ni kwamba hatutakuwa na watu wanaojenga taaluma zao wakifanya kazi bandarini. Jambo lingine ni kwamba wafanyakazi wa sasa wanaweza kupoteza kazi zao siku zijazo kwa sababu wakichukua nafasi hiyo, hakutakuwa na haja ya KPA kuajiri,” alisema Bw Faki.
Bw Faki alisema kuwa jamii ilitoa ardhi kwa ajili ya ujenzi wa Bandari na Uwanja wa Ndege, hatua ambayo kihistoria ilisababisha kupatikana kwa nafasi za ajira kwa wakazi wa eneo hilo.
Hata hivyo, alibainisha kuwa, hali hiyo inabadilika, akitaja ajira za hivi karibuni za mafunzo ya usimamizi.
“Wengi wao hawakuwa wenyeji, ingawa watu wanasema hii ni mali ya taifa. Lakini ni ardhi yetu tuliyoitoa kwa ajili ya ujenzi wa bandari. Zamani, kabla ya uhuru, wazee wetu walilipwa mrabaha kwa sababu ya ardhi iliyochukuliwa na kujengwa bandari,” alisema Bw Faki.
Aliahidi kufanya uchunguzi katika Kumbukumbu za Taifa ili kupata ushahidi ambao unaweza kuwasilishwa kwa serikali kuunga mkono kurejeshwa kwa malipo ya mrabaha, akisema kuwa jamii inaendelea kutengwa katika ajira za bandarini.
Wakati huo huo, kundi moja la kijamii limewasilisha kesi mahakamani kupinga mpango wa KPA wa kukodisha vifaa na kuhamisha huduma za shughuli za bandari kwa kampuni za nje, likidai kuwa hatua hiyo ni sawa na kuigeuza bandari kuwa shirika la kibiashara bila kushirikisha umma ipasavyo.
Zabuni hiyo, ambayo ilichapishwa kwenye tovuti ya KPA mnamo Mei 8, 2026 na kufungwa tarehe Mei 25, inalenga utoaji wa pamoja wa vifaa vya kukodishwa na huduma za uendeshaji wa shughuli za bandari.
Mwenyekiti wa Chama cha Taireni cha Wamijikenda, Bw Peter Kadzeha, alisema kuwa mpango huo kwa kiasi kikubwa unahamisha udhibiti, matumizi na manufaa ya kiuchumi ya mali muhimu za umma kwa taasisi binafsi.