Dimba

Orodha ya kugutusha ya silaha kali zitakazolikosa Kombe la Dunia

Na MASHIRIKA June 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

BAADHI ya wanasoka bora duniani watakosa Kombe la Dunia la FIFA la 2026 kutokana na majeraha mabaya, kupuuzwa na makocha wa timu zao za taifa au vikosi vyao kushindwa kufuzu.

Michuano hiyo inayoshirikisha timu 48 itafanyika Mexico, Amerika na Canada; na itaanza Alhamisi, Juni 11, 2026 kwa pambano la Kundi A kati ya Mexico na Afrika Kusini ugani Estadio Azteca.

Khvicha Kvaratskhelia (Georgia)

Wing’a huyu wa Paris Saint-Germain (PSG) hajawahi kunogesha Kombe la Dunia. Atakosa makala ya mwaka huu baada ya Georgia kushindwa kufuzu.

Kipute chake cha mwisho cha haiba kubwa akivalia jezi za timu ya taifa kilikamilika katika hatua ya 16-bora ya Euro 2024.

Robert Lewandowski (Poland)

Alidokeza uwezekano wa kustaafu soka ya kimataifa mnamo Machi baada ya Poland kushindwa kufuzu kwa Kombe la Dunia.

Amecheza Poland mara 165 na kuifungia mabao 89 tangu 2008. Ametandaza Kombe la Dunia mara mbili pekee, akitambisha timu yake ya taifa hadi hatua ya 16-bora mnamo 2022 nchini Qatar.

Gianluigi Donnarumma, Sandro Tonali (Italia)

Kutofuzu kwa Italia kwa Kombe la Dunia kwa mara ya tatu mfululizo kutanyima fursa baadhi ya wanasoka bora wa Azzurri, akiwemo kipa Donnarumma na kiungo Tonali.

Italia ndio mabingwa wa kwanza wa zamani kukosa fainali tatu mfululizo za Kombe la Dunia. Mara yao ya mwisho kunogesha kipute hicho ni 2014 nchini Brazil.

Victor Osimhen, Ademola Lookman (Nigeria)

Baada ya Italia, Nigeria ndilo taifa jingine kubwa zaidi kukosa kushiriki Kombe la Dunia 2026.

Kutofuzu kwao kunamaanisha kuwa mashabiki watakosa kumtazama Lookman aliyeibuka mchezaji bora katika AFCON 2025 na Osimhen ambaye ni miongoni mwa wavamizi matata zaidi barani Afrika.

Nigeria sasa wamekosa fainali za Kombe la Dunia mara mbili mfululizo kwa mara ya kwanza baada ya miaka 36.

Hugo Ekitike (Ufaransa)

Ndoto ya Ekitike kucheza Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza ilivurugika alipopata jeraha la mguu akichezea Liverpool dhidi ya PSG katika mkondo wa pili wa robo-fainali ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) ugani Anfield mnamo Aprili.

Jeraha hilo linatarajiwa kumweka mkekani hadi Januari 2027. Hadi alipoumia, alikuwa amefungia Liverpool mabao 17.

Estevao Willian, Rodrygo Silva (Brazil)

Estevao, 19, alitarajiwa kunogesha Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza kabla ya jeraha la paja alilopata akichezea Chelsea mnamo Aprili kukatiza ndoto yake. Alijiunga na Chelsea kutoka Palmeiras mnamo Mei 2024 na akafunga mabao manane na kuchangia mengine manne.

Rodrygo, ambaye ni fowadi wa Real Madrid, alichezea Brazil mechi tano katika Kombe la Dunia la 2022. Hatanogesha makala ya mwaka huu baada ya kupata jeraha la goti lake la kulia akichezea Madrid mnamo Machi na anatarajiwa kuwa mkekani hadi mwisho wa 2026.

Xavi Simons (Uholanzi)

Hatakuwa sehemu ya kikosi cha Uholanzi baada ya kupata jeraha la goti akichezea Tottenham Hotspur dhidi ya Wolves katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL).

Makala ya Kombe la Dunia mwaka huu yangekuwa yake ya pili baada ya 2022 nchini Qatar. Amechezea Uholanzi mara 34, akishiriki mechi kadhaa za kirafiki mnamo Machi.

Bryan Mbeumo (Cameroon)

Kushindwa kwa Cameroon kutinga Kombe la Dunia kulishangaza wengi kwani ndio wanaoshikilia rekodi ya Afrika ya kufuzu kwa kipute hicho mara nyingi zaidi (nane).

Mbeumo amekuwa na msimu mzuri kambini mwa Manchester United, akifunga mabao 10 na kuchangia matatu mengine katika michuano yote.

Cole Palmer na Phil Foden wa Uingereza walipuuzwa na kocha wao sawa na ambavyo Joao Pedro, Richarlison Andrade (Brazil) na Eduardo Camavinga (Ufaransa) walifanyiwa.

Jan Oblak (Slovenia) na Dominik Szoboszlai watakosa Kombe la Dunia baada ya mataifa yao kutofuzu.

Fermin Lopez (Uhispania), Serge Gnabry (Ujerumani), Takumi Minamino, Kaoru Mitoma (Japan), Eder Militao (Brazil), Matthijs de Ligt (Uholanzi), Marc-Andre ter Stegen (Ujerumani) na Mohammed Kudus (Ghana) nao wanauguza majeraha tofauti.