Wagonjwa wahangaika baada ya mfumo wa SHA kupata hitilafu tena
KWA siku tatu sasa, wagonjwa katika hospitali za umma kote nchini Kenya wamekuwa wakikwama, wakikosa huduma katika vyumba vya matibabu na kuambiwa watoe fedha taslimu ambazo hawana au wasubiri mfumo ambao hakuna mwenye hakika utarejea kufanyakazi lini.
Mfumo wa Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA) ulipata hitilafu Jumapili, huku kukiwa na ahadi kwamba hakuna Mkenya ambaye atanyimwa matibabu kwa sababu ya kushindwa kulipa.
Mildred Awuor amelazwa katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta (KNH)kwa wiki moja sasa akiwa na maumivu ya tumbo.
Alitarajia kuruhusiwa kuondoka Jumapili, lakini hadi sasa, hati yake ya kuruhusiwa bado haijashughulikiwa, na kila siku ya ziada analala hospitalini inaongeza gharama ya bili yake ambayo tayari ni kubwa kupita uwezo wake.
“Kadri ninavyokaa, ndivyo bili inavyoongezeka. Kwa kuwa nilitumia bima ya SHA wakati wa kulazwa, mfumo lazima urudi kufanya kazi kabla ya kuruhusiwa kuondoka. Sina pesa. Sijui nitatozwa kiasi gani mwisho wa haya yote,” alisema.
Mildred hayuko peke yake.
Katika KNH na hospitali nyingine za umma, wagonjwa wamekuwa wakikwama kwa siku kadhaa kwa sababu ya mfumo uliokuwa umeahidi huduma nafuu za afya, lakini sasa umewaacha wakiwa wamenaswa kati ya mfumo wa kidijitali ulioporomoka na wasimamizi wa hospitali ambao hawawezi kuwaruhusu kuondoka wala kufidia gharama za matibabu yao.
Miongoni mwa walioathirika zaidi ni wagonjwa wa saratani, ambapo kuchelewa kwa matibabu si kero tu bali ni tishio la moja kwa moja kwa maisha.
Jumapili, mamia ya wagonjwa wa saratani waliketi kwa saa nyingi KNH wakisubiri kuidhinishwa kupitia mfumo wa SHA ili waweze kupata tiba na huduma nyingine za onkolojia.
Wengi walisubiri asubuhi yote, lakini hadi mchana bado hawakuwa wameidhinishwa. Wengine walilala nje ya hospitali usiku kucha bila huduma. Wengi walirudi nyumbani bila matibabu.
“Kukosa kipindi cha matibabu kunaweza kupunguza ufanisi wa tiba, kuruhusu uvimbe kuendelea kukua na wakati mwingine kubadilisha kabisa mpango wa matibabu ya mgonjwa,” alisema Phoebe Ongadi, Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Mashirika ya Saratani Kenya.
“Mfumo ulipokuwa chini, nilikosa kumuona daktari aliyepaswa kuamua kama nitaendelea na dawa au la. Tumeambiwa mfumo uko chini, hivyo nitaendelea kutumia dawa nikisubiri,” alisema mgonjwa mmoja.
Mgonjwa mwingine aliyetumwa kupigwa picha ya MRI alielezwa kuwa anahitaji idhini ya SHA kabla ya huduma hiyo.
Hata hivyo, mfumo haukuweza kushughulikia ombi lake. Aliambiwa atalazimika kulipa Sh38,000 fedha taslimu ili kupata huduma hiyo lakini hakuwa na fedha hizo.
Mkurugenzi Mtendaji wa SHA, Dkt Mercy Mwangangi, alithibitisha kuwepo kwa hitilafu ya mfumo lakini akasema tatizo hilo limeshughulikiwa.
“Hata ningekuwa nazo, haina maana kulipa kwa sababu SHA haitanirejeshea. Na SHA haiwezi kunithibitishia idhini kwa sababu mfumo haufanyi kazi,” alisema.
Katika hospitali mbalimbali, wagonjwa wamesalia wakisubiri bila kujua lini mfumo utarejea.
Wakati huo huo, changamoto hiyo imeathiri pia Wakenya wanaolipa michango yao ya kila mwezi ya SHA, ambapo baadhi wameshindwa kufanya malipo, na hivyo kuwanyima ndugu zao kupata huduma.
Katika kisa kimoja Nairobi, familia imekwama kwa siku tatu kushughulikia mwili wa ndugu yao aliyefariki, kwani hospitali haitoi mwili hadi bili ilipwe, lakini SHA haifanyi kazi.
Mkurugenzi Mtendaji wa SHA, Dkt Mercy Mwangangi, alithibitisha kuwepo kwa hitilafu ya mfumo lakini akasema tatizo hilo limeshughulikiwa.
Hata hivyo, hata baada ya taarifa hiyo, wagonjwa na hospitali ziliendelea kuripoti changamoto hizo hizo.