Habari

Mkaguzi afichua wastaafu wanaendelea kupokea mishahara katika kaunti

Na ERIC MATARA June 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MKAGUZI Mkuu wa Hesabu za Serikali, Nancy Gathungu, amefichua jinsi mamia ya wafanyakazi wastaafu wa serikali za kaunti katika kaunti nane wanavyoendelea kupokea mishahara.

Ukaguzi wa hivi karibuni unaohusu mwaka wa kifedha uliomalizika Juni 30, 2025, umebaini kuwa licha ya wafanyakazi hao kufikia umri wa kustaafu, wanaendelea kulipwa mishahara na marupurupu kinyume cha sheria.

Kwa mujibu wa Kanuni ya 70(1) ya Kanuni za Tume ya Huduma za Umma ya mwaka 2020, umri wa lazima wa kustaafu katika utumishi wa umma ni miaka 60, na miaka 65 kwa watu wanaoishi na ulemavu.

Hata hivyo, ripoti hiyo ya ukaguzi inaonyesha kuwa wafanyakazi katika kaunti husika waliokuwa wakipokea mishahara na marupurupu kinyume cha sheria si watu wanaoishi na ulemavu wala hawakuwa na ujuzi maalum.

Kaunti hizo hazikutoa ushahidi wowote kuonyesha kuwa wafanyakazi hao walikuwa katika makundi maalum, jambo linaloibua uwezekano wa kuwepo kwa udanganyifu mkubwa wa mishahara na ufisadi katika serikali za kaunti.

Kaunti zilizoathirika ni Bomet, Garissa, Isiolo, Samburu, Nyeri, Migori, Nyamira na Embu.

Kwa mfano, huko Bomet, ripoti ilibaini kuwa wafanyakazi 27 katika utawala wa Gavana Hillary Barchok bado wako kwenye orodha ya malipo ya kaunti hiyo, wakipokea mishahara na marupurupu ya thamani ya mamilioni licha ya kufikia umri wa kustaafu.

“Ukaguzi wa orodha ya malipo uliofanyiwa uchunguzi ulibaini kuwa wafanyakazi 27 waliokuwa wamefikia umri wa kustaafu wa miaka 60 bado walikuwa kwenye orodha ya malipo. Katika mwaka uliokaguliwa, maafisa hao walilipwa Sh3 milioni. Hii ilikuwa kinyume na Kanuni ya 70(1) ya Kanuni za Tume ya Huduma za Umma ya mwaka 2020,” inasema sehemu ya ripoti ya Bi Gathungu.

Kaunti hiyo haikutoa sababu za kuridhisha kuhusu kuendelea kuwahifadhi wafanyakazi hao ambao hawakuwa watu wenye mahitaji maalum wala walioteuliwa kisiasa baada ya kufikia umri wa kustaafu.

Huko Garissa, ukaguzi wa orodha ya malipo kwa mwaka wa kifedha 2024/2025 ulifichua kuwa maafisa watano walikuwa wamefikia umri wa lazima wa kustaafu wa miaka 60 lakini bado walikuwa wanalipwa mishahara.

“Ukaguzi wa rekodi za ajira ulionyesha kuwa maafisa watano walikuwa wamefikia umri wa kustaafu wa miaka 60 lakini bado waliendelea kuwa kwenye orodha ya malipo hadi kufikia Septemba 2025. Kaunti haikutoa sababu za msingi kuhalalisha hatua hiyo,” inasema ripoti hiyo.

Katika Kaunti ya Isiolo, wafanyakazi 33 na washauri wanne wa kaunti walikuwa na umri zaidi ya miaka 60 lakini waliendelea kulipwa mishahara.

Wafanyakazi hao kwa pamoja walipokea mshahara wa jumla wa Sh3.7 milioni katika mwezi wa Juni 2025.

Aidha, wanne kati ya wafanyakazi hao walikuwa wakihudumu kama wakurugenzi katika kundi la kazi la R, lakini hakuna ushahidi wa maandishi uliowasilishwa kueleza majukumu, wajibu na maelezo ya kazi za nyadhifa walizoshikilia.

Ripoti hiyo pia ilibaini kuwa Kaunti ya Embu ilikuwa na idadi kubwa zaidi ya wastaafu wanaoendelea kufanya kazi na kupokea mishahara kinyume cha sheria.

Utawala wa Gavana Cecily Mbarire ulikuwa na maafisa 76 waliokuwa wamefikia umri wa kustaafu lakini bado walikuwa kazini kufikia Mei 30, 2025.

Huko Nyeri, ukaguzi huo ulionyesha kuwa wafanyakazi 15 bado walikuwa kazini licha ya kufikia umri wa kustaafu.

Wafanyakazi hao waliendelea kupokea mishahara hata baada ya kustahili kustaafu.

Katika Kaunti ya Migori, ukaguzi kufikia Julai 2025 ulionyesha kuwa kati ya wafanyakazi 3,159, jumla ya 26 walikuwa wamezidi umri wa kustaafu wa miaka 60 lakini bado walikuwa wakifanya kazi na kulipwa mishahara na marupurupu.