Habari za Kitaifa

Bajeti ya madeni na ukopaji zaidi kuziba pengo la ukosefu wa fedha serikalini

Na BENSON MATHEKA June 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SERIKALI inapanga kukopa zaidi ya Sh1 trilioni kufadhili bajeti ya mwaka wa kifedha ujao ya Sh4.8 trilioni, huku pengo la bajeti likikadiriwa kufikia takriban Sh1.1 trilioni, Waziri wa Fedha John Mbadi amekiri.

Akitoa hotuba yake ya bajeti, Mbadi alieleza kuwa makadirio hayo yatafadhiliwa kupitia mikopo ya ndani na nje ya nchi, ambapo Sh116.2 bilioni zitakopwa kutoka kwa wahisani na taasisi za kimataifa, huku Sh1 trilioni zikitarajiwa kupatikana kupitia mikopo ya ndani.

Hatua hii inaonyesha hatua ya serikali ya kutegemea pakubwa kukopa ili kuendesha shughuli na mipango yake, licha ya changamoto zinazohusiana na deni la taifa linaloendelea kuongezeka.

Katika sekta ya elimu, serikali imependekeza kutoa Sh7 bilioni kwa mpango wa elimu ya msingi bila malipo, Sh54.6 bilioni kwa elimu ya sekondari ya kutwa bila malipo, na Sh30.7 bilioni kwa ufadhili wa sekondari msingi (JSS).

Aidha, Sh4.9 bilioni zimetengwa ili kuajiri walimu 20,000 vibarua kuwa wa kudumu na pensheni kuanzia Januari 2027.

Kwa mara ya kwanza, serikali imependekeza pia kutenga Sh3.9 bilioni kulipa posho wazee wa vijiji, hatua inayolenga kuimarisha utawala wa mashinani na kutambua mchango wao katika kuhakikisha usalama na utatuzi wa migogoro ya kijamii.

Katika sekta ya afya, Mbadi alipendekeza kutenga Sh20.9 bilioni kwa Mamlaka ya Usambazaji wa Dawa (KEMSA), Sh3.1 bilioni kwa Taasisi ya Utafiti wa Kimatibabu (KEMRI), na Sh9.3 bilioni kwa wahitimu wa mafunzo ya udaktari.

Vilevile, Sh10.9 bilioni zimetengwa kwa Chuo cha Mafunzo ya Afya (KMTC), huku wahudumu wa afya wa jamii wakipangiwa Sh3.2 bilioni za posho na Sh396 milioni kwa bima ya afya.

Serikali pia imeweka kipaumbele sekta ya kilimo kwa kutenga Sh64 bilioni ili kuongeza uzalishaji, thamani ya mazao na kuimarisha uthabiti wake dhidi ya changamoto kama mabadiliko ya tabianchi.

Katika juhudi za kukuza uchumi wa baharini, Sh8.2 bilioni zimetengwa kusaidia uvuvi na shughuli nyingine za baharini.

Aidha, sekta ya ubunifu imenufaika na mgao wa Sh8.6 bilioni kukuza filamu, muziki, mitindo, sanaa na teknolojia ya kidijitali, huku sehemu ya fedha hizo zikienda kuimarisha miundombinu ya mtandao wa kitaifa.

Katika masuala ya ardhi, serikali imepanga kutenga Sh9.4 bilioni kusaidia kuwapa makazi wananchi wasio na ardhi, hatua inayolenga kupunguza migogoro ya ardhi na kuboresha usawa katika umiliki.

Mbadi alisema kwamba uchumi wa taifa unatarajiwa kukua kwa asilimia tano mwaka 2026, kiwango kilichopungua kutoka makadirio ya awali ya asilimia 5.3 kutokana na athari za mizozo ya kimataifa, hususan Mashariki ya Kati.

Hata hivyo, aliongeza kuwa uchumi unatarajiwa kuimarika tena mwaka 2027 na kukua kwa asilimia 5.2.

Serikali pia inaendelea kutekeleza miradi ya maendeleo kama vile masoko ya kisasa, ambapo masoko 476 yanapangwa kote nchini huku 354 tayari yakitekelezwa.

Miradi hii inalenga kuwapa wafanyabiashara mazingira bora ya kufanyia kazi na kukuza ujasiriamali.

Bajeti hii inaonyesha juhudi za serikali kusawazisha kati ya maendeleo ya kiuchumi, utoaji wa huduma za kijamii na changamoto za kifedha, huku ikiendelea kutegemea mikopo.