Habari

Akaunti za Analo ambaye alipatikana na Sh65m zimefungwa

Na RICHARD MUNGUTI June 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MAHAKAMA Kuu imefunga akaunti za benki za aliyekuwa Afisa Mkuu wa Mipango wa Serikali ya Kaunti ya Nairobi, Patrick Analoh Akivaga, baada ya maafisa wa Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) kupata Sh65 milioni nyumbani kwake Juni 4, 2026.
Amri hiyo pia inahusisha akaunti za mke wake, Damaris Sindavi Kayugira, ambaye ameajiriwa na Serikali ya Kaunti ya Vihiga, na inahusu akaunti katika Benki za KCB, Equity na Co-operative.
Jaji Rose Ougo wa Kitengo cha Ufisadi cha Mahakama Kuu alitoa amri hiyo kufuatia ombi la EACC, akisema uchunguzi wa awali unaonyesha wanandoa hao hawawezi kueleza chanzo cha fedha hizo zilizopatikana katika makazi yao ya Syokimau, Kaunti ya Machakos.
EACC iliambia mahakama kuwa, inaendelea kuchunguza madai ya mgongano wa maslahi, matumizi mabaya ya ofisi, rushwa na kumiliki mali isiyoelezeka dhidi ya Akivaga na mkewe.
Tume hiyo ilibaini kuwa wote wawili ni maafisa wa umma wanaohudumu katika kaunti za Nairobi na Vihiga mtawalia.
Baada ya kupatikana kwa fedha hizo, Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja alimsimamisha kazi Akivaga.
Wakati huo huo, Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) Renson Ingonga ameagiza Akivaga na wengine kufikishwa mahakamani kufuatia kuporomoka kwa jingo mtaani South C, Nairobi, ambalo lilisababisha vifo vya watu kadhaa.