Jinamizi lavisubiri vyama vikuu nchini
MIEZI 15 kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2027, vyama vya kisiasa vimejikuta katika hali ngumu ya kusawazisha maslahi ya wanachama wao wa muda mrefu na kuwakaribisha wanasiasa wapya wenye ushawishi wanaotaka kuwania nyadhifa mbalimbali.
Katika pande zote za kisiasa, vyama vinaendelea kuimarisha ngome zao mashinani, kuunda upya miundo ya uongozi na kuwatafuta wagombea wanaoonekana kuwa na uwezo wa kuvutia kura.
Hata hivyo, mbio za kupata tiketi za vyama zimeanza kuzua mvutano kuhusu ni nani anayestahili kupewa nafasi ya kupeperusha bendera ya chama.
Kuanzia chama cha United Democratic Alliance (UDA) kinachoongozwa na Rais William Ruto hadi Democracy for Citizens Party (DCP) cha aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, Wiper Patriotic Front cha Kalonzo Musyoka na Jubilee Party, viongozi wamekuwa wakisisitiza hadharani umuhimu wa uchaguzi wa haki ndani ya vyama vyao.
Lakini nyuma ya pazia, mikakati ya kisiasa inaonyesha kuwa viongozi wa vyama wanahangaika kutafuta namna ya kusuluhisha maslahi yanayokinzana bila kusababisha wanachama kuhama au kuasi.
Changamoto hiyo inazidi kuwa kubwa huku mazungumzo ya kuunda miungano na kugawana maeneo ya kisiasa yakianza kushika kasi kuelekea uchaguzi mkuu.
Vyama vinakabiliwa na jukumu gumu la kuwazawidi wanachama waliovijenga kwa miaka mingi huku vikivutia wanasiasa wapya wenye ushawishi ambao wanaweza kuongeza nafasi ya ushindi.
Katika chama kipya cha DCP, Bw Gachagua ameahidi mara kadhaa kuwa mchujo utafanywa kwa uwazi na kwamba umaarufu wa mgombea miongoni mwa wapigakura ndio utaamua atakayepata tiketi ya chama.
Hata alipotangaza kurejea nyumbani kwake Wamunyoro kupanga mikakati ya uchaguzi wa 2027, alisisitiza msimamo huo.
“Kuanzia Jumatatu nitakuwa Wamunyoro kwa siku 45 kufanya mashauriano ya kina na wafuasi, viongozi wa maoni na wadau kuhusu namna ya kumpata mgombea mmoja wa urais atakayemenyana na Rais William Ruto,” alisema.
Bw Gachagua amesema hata washirika wake wa karibu hawatapendelewa katika uteuzi wa wagombea.
Hata hivyo, baadhi ya kauli zake za hivi karibuni zimeibua mjadala kuhusu iwapo kweli wagombea wote watapata nafasi sawa.
Tayari amemtangaza hadharani aliyekuwa Waziri wa Kilimo Mithika Linturi kuwa mgombeaji wa kiti cha ugavana wa Meru kupitia DCP. Pia amemtaja Seneta wa Kirinyaga Kamau Murango kuwa chaguo lake kwa ugavana.
Huko Mombasa, awali alimuidhinisha Mohammed Ali kugombea ugavana kupitia DCP kabla ya mazungumzo na makubaliano na mshirika wake Wiper kubadilisha mwelekeo wa kisiasa.
Katika eneo la Mlima Kenya, maeneo kadhaa ya Nyeri, Murang’a, Kiambu na Kirinyaga yamegeuka uwanja wa ushindani wa kimya kati ya wanasiasa wenye uzoefu wanaomuunga mkono Gachagua na vijana wanaotaka kutumia hisia zinazoongezeka za kupinga utawala wa Rais Ruto.
Kaunti ya Nyandarua pia imeingia kwenye mjadala huo baada ya aliyekuwa MCA Kieru Wambui kutangaza nia ya kuwania useneta, ingawa wengi wanaamini nafasi hiyo imehifadhiwa kwa Seneta wa sasa John Methu Katibu Mkuu wa DCP.
Hali kama hiyo inaonekana pia Naivasha, Murang’a, Laikipia na Kiambu ambako wanaotaka kuwania ubunge na useneta wanajaribu kujipanga huku wakikabiliana na maslahi ya ndani ya chama.
Aliyekuwa Mbunge wa Nyeri Town Ngunjiri Wambugu amewaonya wanaotamani kugombea wasidhani kuwa umaarufu wao mashinani pekee utawapa tiketi za chama.
“Ushauri wangu wa bure ni kwamba Gachagua yuko kwenye biashara. Isipokuwa chapa yako ya kisiasa iwe kubwa kuliko chama eneo lako, anaweza kuuza tiketi yako kwa atakayetoa dau kubwa zaidi mwaka 2027,” alisema.
Kauli yake imeongeza wasiwasi miongoni mwa baadhi ya wanasiasa wanaohofia kuwa maamuzi ya ndani ya vyama na miungano ya kisiasa yanaweza kupewa uzito kuliko uungwaji mkono wa wananchi.
Wakati huo huo, katika Bonde la Ufa, chama cha UDA kinakabiliwa na changamoto zake za uteuzi. Ingawa bado kina nguvu katika kaunti nyingi, kizazi kipya cha wanasiasa wanaomuunga mkono Rais Ruto kinaanza kuwapa ushindani viongozi walio madarakani.
Baadhi ya viongozi walio madarakani wamekosolewa kwa madai ya kutotekeleza wajibu wao ipasavyo au kushindwa kuendana na ajenda ya chama.
Aidha, wataalamu na vijana wengi wanataka kutumia nguvu ya kisiasa ya serikali ya Kenya Kwanza kupata nafasi za ubunge na uongozi wa kaunti, hali inayowatia hofu wabunge na viongozi waliopo.
Katika Kaunti ya Nakuru, Gavana Susan Kihika anakabiliwa na ushindani unaoongezeka kutoka kwa wapinzani na hata ndani ya UDA yenyewe. Hillary Kipngeno na Joseph Rotich tayari wameonyesha nia ya kuwania tiketi ya ugavana, jambo linalotarajiwa kuleta ushindani mkali.
Hali si tofauti ndani ya Wiper ambapo Kalonzo Musyoka atalazimika kufanya maamuzi magumu kusawazisha maslahi ya Mbunge wa Mavoko Patrick Makau na Gavana wa Machakos Wavinya Ndeti.
Bw Makau tayari ametaka mchujo wa chama ufanywe kwa uwazi bila kuingiliwa na viongozi wakuu wa chama au washirika wa muungano wa upinzani.
Mambo yanaweza kuwa magumu zaidi iwapo vyama vya upinzani vitakubaliana kugawana maeneo ya kisiasa ili kuepuka kugawana kura.