Lugha, Fasihi na Elimu

PROF IRIBE: Ilifurahisha kumwona Rais Samia akitumia Kiswahili kuhutubu safu ya kimataifa

Na IRIBE MWANGI June 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JUMA lililopita niliona kanda ya video ambapo Rais wa Tanzania Suluhu Samia Hassan alikuwa akizungumza Kiswahili katika safu ya kimataifa.

Rais Samia alikuwa mshiriki katika mazungumzo ya jopo chini ya mwavuli wa Jukwaa la Kimataifa kuhusu maswala ya Kiuchumi la St Petersburg mnamo tarehe 5, Juni.

Jopo hilo lilijumuisha Rais wa Urusi Vladimir Putin, Rais wa Uzbekistan Shavkat Mirziyoyev, Makamu wa Rais wa Uchina Han Zheng na Rais Samia.

Mdhibiti wa jopo alikuwa mwanahabari anayetajika Geeta Mohan kutoka India.

Mohan alimuuliza Rais Samia namna ambavyo angekwepa vikwazo ilivyowekewa Tanzania kaika azma yake ya kuongeza viwango vya biashara baina ya Tanzania na Urusi.

Rais Samia alimjibu kwamba taifa la Tanzania halikuwa limewekewa vikwazo vya aina yoyote na yeyote.

Bila shaka jibu hili lilimtia aibu huyo mdhibiti na kuashiria hali ya kutokuwa tayari au uchukulizi tu wa mambo bila kuyachunguza kwa kina.

Lakini hilo silo lililonivutia katika mjadala huo. Lililonivutia ni yale maneno aliyoyasema Rais Suluhu kabla ya kutoa jibu hilo.

Mdhibiti aliuliza swali lake kwa Kiingereza lakini kabla ya kulijibu, Rais Samia alimtaarifu kwa lugha iyo hiyo kwamba alivutiwa sana kuwasikia wanajopo wenzake wakichangia kwa kutumia lugha za taifa za nchi zao na kwa sababu hiyo, yeye pia angetumia nafasi yake kuzungumza kwa lugha yake ya taifa.

Baada ya kutoa tahadhari hiyo, Rais Samia alianza kutoa jibu lake kwa lugha ya Kiswahili. Jambo hili lilinichangamsha si haba!

Nimependekeza jambo hili mara nyingi.

Nimekuwa nikisisitiza kwamba viongozi wetu watumie Kiswahili katika makongamano na mikutano ya kimataifa na katika kufanya hivi watawapa nafasi wakalimani kufanya kazi yao.

Takriban mwaka mmoja uliopita niliandika hivi: “Ningetamani sana kuona hali kama hii Afrika: Rais Ruto akizungumza Kiswahili huku Rais wa Misri Abdel Fattah el-Sis akitumia Kiarabu naye Nuhu Bakari akiwa mkalimani wao.”

Niliendelea kuandika kwamba, inasikitisha sana kuwaona viongozi wetu wakitumia Kiingereza huku Mfaransa akitumia Kifaransa chake hivi kwamba mkalimani anayetumiwa ni wa Kiingereza-Kifaransa-Kiingereza.

Mbona asiwe wa Kiswahili-Kifaransa-Kiswahili ilhali Kiswahili ni lugha rasmi nchini?

Hii ndiyo sababu inayofanya nione raha kwamba pale palipotumiwa Kichina, Kirusi, Kiuzbeki na Kiingereza, Kiswahili pia kilipata nafasi yake kutokana na ukakamavu wa Rais Samia.

Mwelekeo kama huu ukichukuliwa na viongozi wengine wa Afrika Mashariki, mbali na kuongeza ajira, uzalendo wa lugha pia utaimarika.

Uzalendo wa lugha huenda sako kwa bako na uzalendo wa kiutamaduni na kijamii.

Mwisho mwisho wa mwaka jana nilipendekeza pia kwamba wanaotuwakilisha katika ulingo wa kimataifa katika jambo lolote lile watumie Kiswahili katika majibu yao pasi kujali kama swali limeulizwa kwa lugha gani.

Hivi, nilieleza, ndivyo tutakavyoheshimiwa na kudhihirishia ulimwengu kuwa tunaweza kuwasiliana kwa ufasaha bila kutapatapa au kuboronga sarufi na kanuni zingine za lugha.

Hivi ndivyo alivyofanya Rais Samia.

Kama wawakilishi wetu wakifanya mazoea ya kutumia Kiswahili, nilisema, basi vyombo vya habari ama vitatumia wakalimani au watafsiri kupata taarifa kwa lugha vinavyoipendelea.

Katika kufanya hivi, wawakilishi hao watakuwa wamechangia pakubwa katika kueneza Kiswahili na kuunda nafasi za ajira kwa wanajumuiya wenzao.